Tuesday, April 25, 2017

JENISTA MHAGAMA AWATAKA WATANZANIA KUWA WAZALENDO NA KUDUMISHA AMANI ILIYOPO

Waziri Mhagama akikagua maandalizi ya kuadhimisha sherehe za miaka 53 ya Muungano katika viwanja vya Jamhuri leo mjini Dodoma.

Na Immaculate Makilika,

Maelezo Dodoma.

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu, Ajira na Wenye ulemavu, Jenista Mhagama amewaasa Watanzania kuwa wazalendo pamoja na kudumisha amani na utulivu uliopo nchini.

Alisema hayo leo wakati alipokuwa akizungumza mjini Dodoma wakati akifuatatilia maandalizi ya maadhimisho ya miaka 53 ya Muungano yatakayofanyika Aprili 26 mwaka huu kwenye uwanja wa Jamhuri uliopo mjini hapa.

“Tunapoadhimisha miaka 53 ya Muungano ninawaomba watanzania kuwa wazalendo pamoja na kulinda amani ya nchi”, alisema Waziri Mhagama.
Waziri Mhagama aliwaomba watanzania hasa wakazi wa Dodoma, kuhudhuria pia kwa wingi katika maadhimisho hayo yatakayofanyika Aprili 26 mwaka huu.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Jordan Rugimbana alisema kuwa mkoa wake umejipanga vizuri katika kufanikisha maadhimisho hayo ambapo pia alivishukuru vyombo vya habari kwa kuhamasisha wananchi juu ya sherehe hizo.


“Wananchi wamehamasika kushiriki katika maadhimisho haya ya miaka 53 ya Muungano, ninawashukuru kwa kazi kubwa mliyoifanya na tunaamini mtaendelea kuhamasisha wananchi kushiriki katika maadhimisho haya”, alisema.

Maandalizi ya maadhimisho ya miaka 53 ya Muungano yamehudhuriwa pia na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma mjini Christina Mndeme pamoja na viongozi mbalimbali wa Serikali.

Aidha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho hayo, ambapo pia yatahudhuriwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein na viongozi mbalimbali wa dini na Serikali.

Maadhimisho hayo ya miaka 53 ya Muungano yanatarajiwa kupambwa na maonesho kutoka kutoka vikosi mbalimbali vya ulinzi na usalama, burudani za vikundi vya ngoma pamoja na maonesho ya halaiki.


Baadhi ya wananchi wakifuatilia maonesho ya maandalizi ya maadhimisho ya miaka 53 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yanayotarajiwa kufanyika Aprili 26 kesho mjini Dodoma kwa mara ya kwanza tangu Serikali ilipohamia Dodoma.

Vikosi vya ulinzi na usalama vikiwa kwenye gwaride la maandalizi ya maadhimisho ya miaka 53 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yanayotarajiwa kufanyika Aprili 26 kesho mjini Dodoma.

Vikosi vya ulinzi na usalama vikiwa kwenye gwaride la maandalizi ya maadhimisho ya miaka 53 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yanayotarajiwa kufanyika kesho Aprili 26 mjini Dodoma.

Vikosi vya ulinzi na usalama vikiwa kwenye gwaride la maandalizi ya maadhimisho ya miaka 53 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yanayotarajiwa kufanyika Aprili 26 mjini Dodoma.
Askari wa Pikikipi maalum wakionesha namna pikipiki hizo zitakavyopamba maonesho hayo.
Makomandoo wa Jeshi la wananchi wa Tanzania wakionesha umahiri wao wa kuvuta gari lenye tani 7 ikiwa ni moja ya mbinu ya medani katika uwanja wa mapambano.
Askari wa kikosi cha Farasi wakionesha umahiri wao katika kutumia farasi kupambana na uhalifu.
Wanafunzi wa halaiki wakipita kwa ukakamavu mbele ya jukwaa kuu.

No comments: