Monday, July 17, 2017

MKURUGENZI HALMASHAURI MJI WA MBINGA APEWA MWEZI MMOJA KUKARABATI JENGO LA UPASUAJI

Naibu Waziri wa wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala akizungumza na umati wa watu uliokusanyika kumsikiliza mara baada ya kukagua mazingira ya hospitali ya Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.
Naibu Waziri wa wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala akisisitiza jambo wakati akiwa katika ziara yake ya kikazi kukagua maeneo ya hospitali ya Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,    
Mbinga.

NAIBU Waziri wa Wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala amempa mwezi mmoja Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Robert Mageni ahakikishe kwamba jengo la upasuaji katika hospitali ya halmashauri ya mji huo linafanyiwa ukarabati haraka ili liweze kuwa katika hali nzuri.

Agizo hilo limetolewa juzi na Dokta Kigwangala alipokuwa katika ziara yake ya kikazi ambapo kufuatia jengo hilo kuwa chakavu katika maeneo mbalimbali ya ndani na nje hususan kwa yale yanayotumika kuoshea vifaa vya kutibu wagonjwa ameagiza pia yajengewe marumaru ili kuweza kuzuia uzalishaji wa wadudu ambao ni hatari kwa afya ya binadamu.

Vilevile ametaka pia chumba cha kunawia pamoja na miundombinu ya maji katika jengo hilo nayo vifanyiwe ukarabati mapema ikiwemo milango yake ili iweze kufunguka upande wa ndani na nje.


Dokta Kigwangala alisisitiza pia katika maeneo ya ndani ya jengo kuwepo na alama maalumu ili kuweza kuzuia watu wasiweze kuingia hovyo hasa muda ambao shughuli mbalimbali za upasuaji zinafanyika.

“Milango ya jengo hili ifanyiwe ukarabati upya ili iweze kufunguka vizuri ndani na nje, chumba cha kunawia na masinki ya maji nayo yafanyiwe ukarabati”, alisisitiza.

Pamoja na mambo mengine alipoingia katika jengo la maabara katika hospitali hiyo ya halmashauri ya mji wa Mbinga, alipongeza miundombinu ya jengo hilo ikiwa katika hali nzuri na kuwataka iendelee kuwa katika hali hiyo ili wagonjwa waweze kuhudumiwa katika mazingira mazuri.
 

No comments: