Wednesday, March 14, 2018

UWT TUNDURU WAONESHA MSIMAMO WAO


Na Muhidin Amri,      
Tunduru.

JUMUIYA ya Wanawake Tanzania (UWT) Wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma imepata Mwenyekiti wake, Zuhura Maftari baada ya kumchagua kwa ushindi wa kishindo kuongoza jumuiya hiyo.

Msimamizi wa  uchaguzi huo ambao ni wa marudio uliofanyika kwenye ukumbi wa UWT Wilayani humo, ambaye ni Mjumbe wa Kamati tendaji ya Mkoa huo, Maristela Mapunda akitangaza matokeo ya uchaguzi huo alisema kuwa Maftari alishinda kwa kupata kura 367.

Alifafanua kuwa katika ushindi huo, Maftari aliongeza idadi ya kura na kwamba katika uchaguzi uliofanyika hapo awali wagombea walioshindwa, walikata rufaa huku akiwa na ushindi wa kura 346.


Katika uchaguzi huo jumla ya wajumbe 493 wa jumuiya hiyo walijitokeza kupiga kura, ambapo kura halali zilikuwa 453 na kura 40 ziliharibika.

Alisema kuwa kutokana na matokeo hayo wagombea wengine, Zainabu Ligola alipata kura 42 ambaye katika uchaguzi huo wa awali alipata kura 150 hivyo alishuka kwa kura 108.

Mapunda aliwataja Wagombea wengine kuwa ni, Fatu Hemed Kaisi ambaye katika uchaguzi huo alipata kura 21 akiwa ameshuka kwa kura 15 ikilinganishwa na kura 36 alizopata katika uchaguzi wa awali, Sophia Said Mtuchi ambaye alipata kura 18 na kupungukiwa kura 5 ikilinganishwa na kura 23 alizopata katika uchaguzi wa awali.

Alimtaja mgombea mwingine ni  Asha Alli Mpinga aliyeshika nafasi ya mwisho huku akiwa amepata kura 5 na kupunguza kura moja ikilinganishwa na kura 6 alizopata katika uchaguzi wa awali.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya wajumbe wa mkutano huo walisema hizo ni salamu tu kwa baadhi ya wanachama ambao wamekuwa waking’ang’ania kupata madaraka kwa kulazimisha.

Aidha wajumbe hao ambao hawakutaka majina yao yatajwe walisema kuwa waliwashauri viongozi wao, ambao wamekuwa wakifanya upendeleo kwa wanachama hao kuheshimu maamuzi ya wajumbe katika mikutano ya uchaguzi husika na sio vinginevyo.

Awali akisoma kanuni na maelekezo ya uchaguzi huo, Katibu wa UWT Wilaya ya Tunduru, Mariam Kasembe aliwataka wajumbe hao kufanya uchaguzi huo kwa kutumia utashi wao na kwamba kufanya uchaguzi kwa mashinikizo kutoka kwa baadhi ya viongozi, kutawaharibia jumuiya yao.

No comments: