Wednesday, March 14, 2018

ACT WAZALENDO TUNDURU WAPATA PIGO WANACHAMA WAKE 1,630 WAHAMIA CHAMA TAWALA


Na Muhidin Amri,         
Tunduru.

VIONGOZI na Wanachama 1,630 wa Chama cha ACT– Wazalendo katika Wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma, wamefunga milango ya chama chao na kukihama chama hicho huku wakijiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Wanachama hao walifikia maamuzi hayo juzi mbele ya Naibu Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Rodrick Mpogoro katika kijiji cha Mtina Wilayani Tunduru Mkoani hapa kwa kile walichodai kwamba wanaunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dokta John Pombe Magufuli ambaye amekuwa akionesha kupambana kwa vitendo hasa katika matukio ya ufisadi, rushwa wizi na dhuluma.

Akizungumza kwa niaba ya Wanachama wenzake Afisa wa ACT, Amani Ramadhan Kawawa alisema kuwa yeye na wanachama wenzake katika Wilaya hiyo wamefikia maamuzi hayo, baada ya kubaini kuwa viongozi wa vyama vya upinzani wamekuwa wakiwatumia wao kama daraja la kuweza kufikia mafanikio yao binafsi.


Kawawa alisema kuwa kutokana na maamuzi hayo, amejiudhuru nafasi zake zote alizokuwa anaziongoza kupitia chama hicho cha ACT.

Alisema mbali na viongozi hao wa vyama vya siasa kuahidi kufikia malengo ya kuchukua dola, lakini hali halisi ya utekelezaji wa malengo hayo umekuwa hauendani na utekelezaji wake jambo ambalo linawafanya wajitambue na kuwaona kuwa viongozi hao ni matapeli.

Alisema kuwa chama chochote ambacho kinahitaji kuchukua dola kinatakiwa kuwa karibu na jamii, lakini vyama vingi vya siasa hapa nchini kwa muda mrefu havijaonesha kuwa na mahusiano ya karibu na wanachama wake hasa katika kushiriki shughuli za kimaendeleo, badala yake vimekuwa vikitumia muda mwingi kuchochea chuki na uhasama kati ya wananchi na Serikali yao.

Kawawa aliwataja viongozi wengine ambao wameunga mkono maamuzi hayo kuwa ni pamoja na Mohamed Kisonga Zuberi (Mwenyekiti na mgombea udiwani kata ya Nampungu), Rashid Hashim Mbalamula (Katibu Mwenezi Act – Wilaya) Wenyeviti, Makatibu kata zote Wilayani humo pamoja na wanachama katika vijiji vyote vya Wilaya hiyo.

Mbali na Kawawa, Wanachama wengine wa ACT waliojiunga na Chama Cha Mapinduzi ni pamoja na Alli Daimu Abdalah ambaye alikuwa Mwenyekiti wa ACT – Wazalendo na mgombea Ubunge katika jimbo la Tunduru Kusini katika uchaguzo Mkuu uliopita wa mwaka 2015.

Akiwakaribisha wanachama hao Naibu Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Mpogolo pamoja na kuwapongeza kwa maamuzi hayo waliyofanya aliwataka Watanzania, ambao bado wapo katika vyama vya upinzani kurudi katika Chama Cha Mapinduzi ambacho kimepigania Uhuru wa nchi hii.

Mpogolo alieleza kuwa utekelezaji wa Serikali ya awamu ya tano inashughulika na kero za wananchi wake kwa kasi ya ajabu na kuwaletea maendeleo hivyo haoni sababu ya wao kupoteza muda na kuhangaika na vyama vyenye ukakasi.

Aliongeza kuwa hivi sasa Tunduru imefunguka kwa kuwa na miundombinu mizuri na yenye uhakika ya barabara, mawasiliano, nishati ya umeme, maji na afya.

No comments: