Tuesday, March 3, 2015

RAIS WA MALAWI ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KWENYE MAZISHI YA KAPTENI KOMBA, WENGINE WAFANYA KAMPENI WAKATI WA MAZISHI















Makada mbalimbali Chama Cha Mapinduzi wakiweka mashada katika kaburi la Kapteni Komba, mara baada ya mazishi kufanyika kijijini Lituhi wilaya ya Nyasa mkoa wa Ruvuma.

Na Mwandishi wetu,
Nyasa.

WAKATI Rais Kikwete akiongoza watanzania, katika mazishi ya Mbunge wa Jimbo la Mbinga Magharibi, Kapteni John Komba kijiji cha Lituhi wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, Rais mstaafu wa Malawi Dokta Bakili  Mluzi ametuma salamu za rambirambi kwa familia ya marehemu na wananchi wa jimbo hilo, kwa kumpoteza mbunge huyo ambaye ni kipenzi cha watanzania na wanamalawi. 

Katika salaam zake alizotuma kwa njia ya barua pepe na kusomwa makaburini hapo mbele ya Rais Kikwete na waombolezaji wengine, Dokta Mluzi alisema kuwa anatambua mchango mkubwa wa marehemu Komba hasa enzi ya uhai wake.

"Nimepokea taarifa hii ya kifo cha mbunge wetu Komba kwa masikitiko makubwa, nipo pamoja na familia na wananchi wote wa jimbo la Mbinga Magharibi katika maombolezo haya", alisema.

Spika wa Bunge, Anne Makinda alieleza kusikitishwa kwake na manabii wa uongo ambao wamekuwa wakiendelea kueneza uongo katika Taifa hili, kwamba lengo lao kuona halitawaliki kwa utulivu na amani.


Alisema kuwa baadhi ya manabii hao ambao  wamekuwa wakizunguka huku na kule kwa wananchi, kazi yao ni kupandikiza chuki juu ya katiba mpya iliyopendekezwa kwa kudanganya umma kuwa ndani ya katiba hiyo, kumeingizwa kipengele kinachoonyesha ndani ya katiba hiyo kuna jambo lenye kuona waislamu wanafanya mambo yao manne, likiwemo la talaka, mirathi na mengine kama ambavyo dini nyingine zinafanya. 

"Jambo kubwa hapa linalosumbua ni juu ya manabii wa uongo wengi wao wanavumisha tu jambo hili halina ukweli, nasema kwa sababu nafsi yangu inanituma niseme hapa hivi sasa, linalosumbua ambalo litakuja katika bunge na mswada tayari ninao ni uwazi wa kufanya mabadiliko ya sheria ya kiislamu iliyopo katika vitabu vya kiislamu mwaka 1964", alisema.

Mwaka 1964 wakoloni walifanya marekebisho na kuwa mahakama za mwanzo ndizo zilianza kufanya shughuli hizo.

Alisema mswada huo si mpya kinachofanyika ni kuona waislamu wanaendelea kufanya mambo yao yanayowahusu kama vile mirathi, talaka, vifo na ndoa wafanye wenyewe na sheria hiyo ipo tayari na sio kwamba inatungwa upya.

" Ila wataalam wa manabii wa uongo wanaeneza kuwa mambo haya yapo katika katiba inayopendekezwa nawaomba sana msiwasikilize...........na lilifanyiwa kazi karibu wiki tatu usiku na mchana kuona suala hilo haliwepo lakini wapo watu wanaotangaza kuwa lipo huo ni uongo mkubwa, CCM ilijadiliana na makundi yote na halipo katika katiba inayopendekezwa", alisema.

Spika Makinda alitaka dini zote kuendelea kufanya Kazi zake kwa uhuru, bila kusikiliza hao wanaofanya kazi ya kueneza uongo huo, kwa kutaka kuona nchi haitawaliki kutokana na uongo wanaoeneza.

Katika mazishi hayo yaliyoshirikisha mawaziri mbalimbali akiwemo Waziri mstaafu, Edward Lowassa ambaye aliambatana na mbunge wa Korogwe vijijini Steven Ngonyani maarufu kwa jina la Profesa Maji Marefu, alitumia msiba huo kujipambanua zaidi kuhusu urafiki wake na Lowassa kuwa kamwe hataacha kumuunga mkono Lowassa, popote atakapokwenda. 

Profesa maji marefu ambaye alisafiri na ndege moja na Lowassa, alisema anajisikia faraja kuendelea kujenga urafiki na rafiki yake huyo, kwani hata kama atagombea urais kamwe hatacheza mbali na Lowassa. 

"Mimi na Lowassa ni marafiki wa siku nyingi, hatujaanza leo urafiki wetu wa damu ni mengi amenisaidia hivyo nipo pamoja na Lowassa, kama mnavyoniona leo tupo hapa kumzika rafiki yetu Komba", alisema.

Kwa upande wake mwakilishi wa kambi ya upinzani bungeni Lindi mjini, Salum Baruan (CUF) mbali ya kumlilia mbunge Komba, bado alisema kuwa Komba alikuwa ni msaada mkubwa katika vita dhidi ya mauwaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi nchini, na siku zote bungeni alikuwa mpambanaji wa watu wanaoua albino. 

Mbali ya mbunge huyo pia wabunge zaidi ya sita waliokuwa katika kamati ya maendeleo ya jamii, makamu mwenyekiti wakiongozwa na mbunge Said Mtandi alisema kifo chake kimekuja wakati wakiwa mbioni kwenda ziara ya kimafunzo nchini Ephiopia.

Wabunge wengine walioshiriki ni pamoja na mbunge wa jimbo la Ludewa, Deo Filikunjombe ambaye alisema kifo cha Komba si tu ni pigo kwa wananchi wa Mbinga Magharibi pekee, bali hata katika wilaya hiyo ambapo mara kadhaa wameungana katika kuwatoa hofu wananchi wa mwambao wa ziwa Nyasa, juu ya kuwa na hofu ya vita kutokana na chokochoko za mipaka kati ya Malawi na Tanzania. 

Filikinjombe alisema, kwa umoja wao walipata kusogeza maendeleo katika wilaya ya Nyasa na Ludewa na kuwa kifo chake ni pengo kubwa.

Akitoa salamu za serikali Waziri wa nchi ofisi ya waziri mkuu, sera na uratibu wa bunge, Jenista Mhagama alisema serikali imempoteza mtu muhimu katika Taifa hili, ambaye alitumia kipaji chake kutoa elimu kwa watu mbalimbali.

Huku Katibu mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Abdulahman Kinana akieleza kuwa, Komba alikuwa ni hazina kubwa ya chama hichona kwamba kifo chake ni pigo kwao.

Mawaziri wengine walioshiriki mazishi hayo ni pamoja na Steven Wassira, Profesa Mark Mwandosya, Dokta Fenela Mkangala, pia mbunge wa Chalinze Ridhiwan Kikwete na Ritta Kabati ambaye ni mbunge wa viti maalum mkoa wa Iringa.

Wakati huo huo wananchi wa Jimbo hilo la Mbinga Magharibi walishindwa kujizuia kutokwa na machozi wakati mwili wa Komba ukishushwa kaburini. 

Huku wananchi hao wakitokwa na machozi, baadhi ya makada wa CCM wanaotaka ubunge katika jimbo hilo, na wale wanaotaka urais wapambe wao walionekana kutumia msiba huo kupiga kampeni waziwazi huku fulana za wagombea zikiwatibua nyongo, watu wa usalama na baadhi yao kutolewa mbele ya waombolezaji wakiwataka kwenda kuvua fulana hizo za kampeni.


No comments: