Monday, March 2, 2015

TCRA YAZINDUA MITAMBO YA KISASA RUVUMA

Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MAMLAKA  ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imewasha rasmi  mitambo ya kurushia matangazo ya digitali mkoani Ruvuma, ili kuendana na mfumo wa kisasa wa mabadiliko ya sayansi na teknolojia na kuachana na mfumo wa analogia.

Tukio hilo la uzinduzi limefanyika  jana katika kituo cha televisheni ya taifa TBC mjini songea, ambapo ndipo  ilipo mitambo hiyo ya kurushia matangazo ya dijitali na mgeni rasmi wakati wa ufunguzi huo alikuwa Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Thabit Mwambungu.


Katika tukio hilo Mkurugenzi huyo wa TCRA, Habbi Guze amewaagiza watoa huduma za usambazaji wa ving’amuzi  walioko mjini songea, kuhakikisha wanakuwa na ving’amuzi vya kutosha ili kuwafanya wananchi, waweze kupata matangazo na taarifa mbalimbali za habari kwa wakati.

Pia alisema, serikali inatarajia kupata ushirikiano wa karibu wa kutoa huduma kwa wadau wa sekta ya utangazaji na wananchi kwa ujumla, katika kuhakikisha kwamba wakazi wa mjini songea na mkoa huo kwa ujumla, wanapata  huduma mpya ya matangazo ya televisheni kwa mfumo wa digitali bila bugudha ya aina yoyote ile.

Guze alisema pamoja na kufikia hatua ya kutumia mitambo hiyo mipya, lakini kuna vyombo vingine havitaguswa na mfumo huo kama utangazaji wa satelaiti waya (cable)na radio, hivyo wakazi  wa Songea wasitupe TV  zao au  luninga za analojia kwa kuwa chanel tano za kitaifa zitakuwa zinaendelea kupatikana, ingawa siyo kwa viwango vya ubora kama vya dijitali.

Alisema katika mikoa yote iliyozimwa mitambo ya analojia na kuwashwa mitambo ya dijitali, Ruvuma peke yake ndiyo iliyopata mitambo ya kisasa zaidi kwa kuwa imeboreshwa ikiwemo kuwepo kwa ving’amuzi  vidogo na vyenye uwezo mkubwa, wa kurusha matangazo.

Kwa upande wake, Said Mwambungu aliipongeza mamlaka hiyo pamoja na makampuni ya usambazaji wa mitambo hiyo, kwa kufanikisha kuweka matangazo ya mfumo wa kisasa ndani ya mkoa  wa Ruvuma na kuufanya ufunguke kimaendeleo zaidi.

Alisema japokuwa mkoa huo umechelewa sana kupata mitambo ya digitali, lakini bado wananchi wamelipokea kwa nguvu kubwa kwani wengi wao walishaanza kutumia teknologia hiyo, hata kabla ya uzinduzi huu kufanyika mjini hapa juu ya matumizi mapya ya mitambo hiyo.

No comments: