Thursday, February 18, 2016

KIKONGWE AVAMIWA NA NYUKI MAKABURINI AFARIKI DUNIA



Na Mwandishi wetu,
Songea.

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, bibi mmoja ambaye alifahamika kwa jina la Amaliya Mbawala (91) mkazi wa kijiji cha Liula A kata ya Matimila wilayani Songea mkoa wa Ruvuma, amefariki dunia baada ya kuumwa na nyuki alipokuwa kwenye mazishi ya mwanae, Sixmund Komba (60) katika eneo la makaburi ya kijiji hicho.

Marehemu Komba katika uhai wake, alikuwa ni mwanajeshi mstaafu wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) kikosi cha Nachingwea mkoa wa Mtwara, ambapo baadaye alipatwa na maradhi ya muda mrefu na kufariki dunia.

Mashuhuda wa tukio hilo walisema kuwa tukio hilo la kushambuliwa na nyuki lilitokea Februari 13 mwaka huu, majira ya alasiri huko Liula A mara baada ya kiongozi wa Kanisa katoliki ambaye pia ni naibu Askofu wa jimbo la Songea, Camilius Haulle kubariki kaburi na jeneza la marehemu huyo kushushwa kaburini na kuanza kuwekwa udongo, tayari kwa ajili ya kukamilisha shughuli ya mazishi.

Walisema kuwa wakati zoezi linafanyika la kuanza kufukia udongo kaburini, ndipo nyuki ambao walikuwa kwenye mti mkubwa mita chache karibu na kaburi hilo walijitokeza na kuanza kushambulia waombolezaji, kwa kuwauma maeneo mbalimbali mwilini.


Hali hiyo iliwafanya waombolezaji hao na  viongozi wa dini kushikwa na taharuki huku Maparoko watatu waliokuwa wakiongozwa na Askofu huyo, wakiwemo na Masista wa kanisa hilo walianza kutimka mbio kwa lengo la kujiokoa na shughuli ya mazishi ilisimama kwa muda, wakisubiri nyuki hao watoweke.

Bibi Mbawala alishindwa kukimbia wakati nyuki hao walipotokea katika eneo hilo, kitendo ambacho kilimfanya ashambuliwe na wadudu hao wa kali ambapo baadaye walipotoweka waombolezaji walirudi tena, karibu na kaburi hilo kwa ajili ya kukamilisha kazi ya mazishi na kumkuta kikongwe huyo akiwa ana hali mbaya, ndipo walipofanya jitihada ya kunusuru uhai wake na wakati wakiwa njiani anakimbizwa kwenda katika zahanati ya kijiji cha Liula kwa ajili ya matibabu alifariki dunia.

Vilevile mashuhuda wa tukio hilo walifafanua kuwa katikati ya mwezi Januari mwaka huu, liliwahi kutokea tena tukio kama hilo la kuvamiwa nyuki wakati walipokuwa wanashiriki mazishi ya mkazi mmoja wa kijiji hicho, ambaye jina lake hawakumtaja ambapo kundi hilo la nyuki lilizunguka kwa dakika chache juu yao na kutokomea kusikojulikana lakini hawakuleta madhara yoyote.

Ofisa mtendaji wa kijiji cha Liula, Norasco Mapunda alisema wameshtushwa na tukio hilo la nyuki kuwashambulia waombolezaji makaburini na kusababisha mtu mmoja kufariki dunia na wanne ambao walijeruhiwa, na kwenda kupumzishwa kwenye zahanati ya kijiji hicho wakiwa wanapatiwa matibabu.

Mapunda alisema kuwa kufuatia kuwepo kwa tukio hilo wapo watu wengine wanalihusisha na imani za ushirikina, lakini yeye alisema anamfahamu marehemu kwa matendo mema na kwamba alikuwa anaishi naye kwa karibu, hivyo wananchi wanapaswa kupuuza na kuachana na imani hizo.

Aliongeza kuwa mara baada ya tukio hilo kutokea, baadhi ya wananchi wa kijiji hicho walirudi tena makaburini nyakati za usiku kwa ajili ya kuukata mti huo ambao nyuki hao walikuwa wameweka maskani yao, na kuwateketeza kwa kuwachoma moto wakitumia mafuta ya taa.

Kadhalika Ofisa mtendaji huyo alieleza kuwa siku ya pili baada ya nyuki hao kuteketezwa mazishi ya Bibi Amaliya Mbawala yalifanyika, huku katika makaburi hayo kulikuwa na mahudhurio ya watu wachache wakihofia kuumwa na wadudu hao.

Akizungumza kwa niaba ya familia mtoto wa mwisho wa bibi huyo, Sista Scholastica Komba wa kanisa hilo katoliki Jimbo la Songea, alisema kuwa katika mazishi hayo ambayo yalikuwa na ukimya mwingi wazee siku hiyo walizuiliwa kwenda makaburini, wakihofia kutokea tena kwa nyuki hao ili wasiweze kuleta madhara.

Sista Komba alisema kuwa amepokea kwa masikitiko makubwa kifo cha mama yake na kwamba, katika familia yao walikuwa sita na sasa wanabaki watano wakiwa hawana baba wala mama licha ya kufanya jitihada za kumuokoa mama yao.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma, Zuberi Mwombeji amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa Februari 14 mwaka huu alikwenda katika eneo la tukio na kufanya mahojiano na mashuhuda mbalimbali, wakiwemo viongozi wa serikali ya kijiji hicho na ndugu za marehemu.

“Siku ya tukio kulikuwa na mazishi ya Sixmund Komba, ambaye katika uhai wake alikuwa ni mwanajeshi mstaafu wa Jeshi la wananchi Tanzania (JWTZ) kikosi cha Nachingwea, baada ya kustaafu alikuwa akiishi Liwale mkoani Lindi baadaye alipatwa na maradhi ya muda mrefu na alifariki dunia”, alisema Mwombeji. 

Alieleza kuwa Komba baada ya kufariki dunia jitihada zilifanywa za kuusafirisha mwili wake kutoka Liwale hadi kijijini kwake Liula, nje kidogo ya Manispaa ya Songea mkoani hapa kwa ajili ya taratibu za mazishi.

Kamanda huyo wa Polisi alisema watu waliokuwepo kwenye eneo hilo la tukio walikimbia na kutokomea kusikojulikana lakini kwa bahati mbaya, bibi Amaliya alishindwa kukimbia kwa sababu hakuwa na uwezo wa kutembea na nyuki walimshambulia na baadaye alipokuwa akikimbizwa kwenye zahati ya kijiji cha Liula, baada ya kupokelewa alithibitishwa kuwa amekufa.

No comments: