Saturday, February 20, 2016

SERIKALI YA CHAMA CHA MAPINDUZI KUTEKELEZA AHADI ZAKE KWA VITENDO



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

RAJABU Mtiula ambaye ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, amesema serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoani humo itahakikisha inatekeleza ahadi zote zilizopo katika ilani yake kwa vitendo, ili kila mwanachi aweze kuwa na maisha bora hapa nchini.

Katika kipindi cha miaka mitano ijayo, kuanzia mwaka 2015 hadi 2020 alisema kuwa Halmashuri hiyo imekusudia kutoa huduma bora na wananchi kuwezeshwa ili kuwa na nguvu kubwa ya pamoja katika kufanya maamuzi, yanayokidhi mahitaji yao kwa lengo moja la kuleta maendeleo badala ya kazi hiyo kufanywa na upande mmoja wa serikali.

Mtiula alisema kuwa, nguvu hiyo ya uwezo wa kukusanya mapato na kufanya maamuzi ya ugawaji na matumizi sahihi, ni pamoja na kupanga mipango ya miradi ya maendeleo ambayo itatekelezwa kwa ufanisi mkubwa katika maeneo yao.


Kiongozi huyo wa Halmashauri ya wilaya ya Songea, alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa na kuongeza kuwa kati ya mambo yatakayopewa kipaumbele ni uwezeshwaji  wa wananchi, kwa kile alichoeleza kuwa tayari serikali imeweka sera ya ugawaji wa madaraka kwao.

Aliongeza kuwa, hatua hiyo inakusudia kumwezesha kila Mtanzania kupitia uimarishaji wa serikali za mitaa ambazo zitawekwa kwa utashi mkubwa na watu wenyewe katika maeo yao, sambamba na kuangalia vipaumbele na mahitaji halisi ya mipango katika uboreshaji  huduma na  uchangiaji ili kupunguza umaskini wa kipato uliokithiri kwenye jamii miongoni mwao.

Aliwaeleza  Madiwani na watumishi wa halmashauri hiyo kwamba, sera ya ugawaji wa madaraka kwenda kwa wananchi itapeleka rasilimali na nguvu ya kisiasa kushuka hadi ngazi ya vijiji,  jambo ambalo litaboresha maamuzi juu ya ugawaji na matumizi sahihi ya rasilimali kwa njia ya ushirikishwaji na umiliki wa wananchi, hususan kwenye maendeleo husika.

Mtiula ambaye pia ni diwani wa kata ya Mpitimbi kupitia CCM alibainisha kwamba, kwa kutumia sera madhubuti zilizoainishwa ndani ya ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi  mwaka 2015 ambayo inatekelezwa kupitia kauli mbiu ya “Hapa kazi tu” na ushiriki wa dhati  wa wananchi kwa umoja wao, Halmashauri itafanikiwa kuboresha huduma za kijamii na kupunguza umaskini.

No comments: