Saturday, February 13, 2016

WATENDAJI WAPANDISHWA KIZIMBANI TUNDURU KWA WIZI WA PEMBEJEO ZA KILIMO



Na Steven Augustino,
Tunduru.

HALMASHAURI ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, imewafikisha Mahakamani watendaji wake sita wa wilaya hiyo, wakituhumiwa kuhujumu mfumo wa ugawaji wa pembejeo za kilimo kwa wakulima.

Watendaji hao wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya wilaya hiyo, na kwamba kila mmoja wao, anatuhuma ya kujibu makosa mawili yanayowakabili Mahakamani hapo.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka yao, watuhumiwa hao wanakabiliwa na makosa ya kula njama kinyume na kifungu cha sheria namba 384 cha sheria za kanuni ya adhabu sura ya 16, kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Vilevile kwa kosa la pili linalowakabili ni kwamba, watendaji hao wametumia mbinu za wizi kuiba vocha za serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zilizopangwa kuwapelekea wanufaika yaani wakulima, kupitia mfumo wa ruzuku wa pembejeo za kilimo.


Akiwasomea mashtaka hayo mlinzi wa amani  Hakimu wa Mahakama ya mwanzo Mlingoti iliyopo mjini hapa, Abdallah Mponda mbele ya mwendesha mashtaka mkaguzi msaidizi wa Polisi, Inspekta  Songelael Jwagu alisema kuwa katika matukio hayo watuhumiwa hao walifanya makosa hayo ya kula njama na kuwaibia wakulima, ambao walitakiwa kunufaika na mfumo huo wa pembejeo.

Inspekta Jwagu alisema kuwa watuhumiwa hao kwa nyakati tofauti, mwezi Januari 2015 na mwaka huu 2016, watuhumiwa walitenda kosa la kwanza na la pili kwa kufanya udanganyifu kwa wananchi ambao walitakiwa kunufaika na mbolea za ruzuku ya serikali, kulingana na maelekezo waliyopewa na mwajiri wao wa halmashauri ya wilaya ya Tunduru.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka hayo, watuhumiwa hao walitajwa Mahakamani hapo kuwa ni mtendaji wa kijiji cha Nangunguru kata ya Nandembo,  Zainabu Twaha Issa (38) ambaye anadaiwa kutenda kosa la wizi kupitia vocha za pembejeo mbolea  za wakulima 29, ambao walipangwa kunufaika na mpango huo  zenye thamani ya shilingi 260,000.

Wengine ni  mtendaji wa kijiji cha Ligoma Zawadi Abdallah Mbeweka (48)  na mtendaji wa kata ya Namasakata Zawadi Halson Msole (30) wanaokabiliwa na kosa la wizi wa shilingi 370,000 kupitia vocha namba 01145271 hadi namba 01145308 mali ya wanufaika 37 wa kata hiyo.  

Aidha shitaka hilo pia lilimtaja mtendaji wa kijiji cha Msinji, Zawadi Hemed Hassan (28) kwamba anakabiliwa na kosa la wizi wa shilingi 4,025,000 na kwamba tukio hilo alilifanya kupitia vocha namba 01146221, 01146222, 01146224 na 01146225 mali ya wanufaika watano kutoka katika kijiji hicho.

Sambamba na watendaji hao, pia hati hiyo ya Mahakama ilimtaja  mtendaji wa kata ya Lukumbule Hassan Hemed Lusenda (64) kuwa yeye anakabiliwa na kosa la wizi wa shilingi 585,000  ambazo anadaiwa kuiba kupitia vocha mbalimbali zilizopangwa kwa ajili ya wanufaika 39, ambao ni wananchi wa kutoka katika kata hiyo.

Pia mtendaji wa kata ya Mchesi tarafa ya Lukumbule Yassin Hilali Mohamed (38) anakabiliwa na kosa la wizi wa shilingi 570,000 ambazo mwendesha mashtaka Inspekta Jwagu aliieleza Mahakama kuwa aliziiba kupitia vocha hizo za ruzuku huku akijua zililenga kuwanufaisha wakulima 38 kutoka katika  vijiji vya Mwenge, Mchesi  na Mrusha wilayani Tunduru.

Watuhumiwa hao walifikishwa katika Mahakama hiyo, kufuatia agizo lililotolewa na Waziri wa Kilimo, Chakula na  Mifugo,  Mwigulu Nchemba baada ya kubaini uwepo wa uchakachuaji mkubwa uliofanyika wa mfumo ugawaji wa vocha za ruzuku ya pembejeo za kilimo, na kwamba watuhumiwa hao wapo nje kwa dhamana hivyo shauri hilo litatajwa tena Mahakamani hapo Februari 20  mwaka huu.

No comments: