Thursday, February 11, 2016

MAHABUSU ALIYEJINYONGA NAMTUMBO UTATA MTUPU



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MTUHUMIWA mmoja ambaye aliwekwa rumande katika mahabusu ya kituo kidogo cha Polisi kata ya Lusewa wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma, amekutwa akiwa amejinyonga na kufariki dunia, ndani ya chumba cha mahabusu hiyo.

Taarifa za tukio hilo zinafafanua kuwa, Vumi Issa Kasumali (30) ambaye ni mkazi wa kata ya Msisima wilayani humo, ndiye aliyepoteza uhai wake kwa kujinyonga kwa kutumia suruali, aliyokuwa amevaa mwilini  mwake.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Zuberi Mwombeji amethibitisha juu ya tukio hilo na kueleza kwamba, lilitokea majira ya mchana Februari 9 mwaka huu.

Mwombeji alieleza kuwa mtuhumiwa huyo, alikuwa anakabiliwa na tuhuma ya kuvunja nyumba na kuiba na kwamba wakati anachukua maamuzi magumu ya kujiua, askari Polisi walikuwa wanajiandaa kumsafirisha kwenda Mahakama ya wilaya Namtumbo ili aweze kujibu tuhuma zinazomkabili.


“Kwa ujumla hatujaweza kutambua huyu mtuhumiwa amejinyonga kwa sababu gani, hakuna hata ujumbe wowote wa maandishi ambao ameuacha wakati anajinyonga kwenye chumba hiki cha mahabusu”, alisema Kamanda Mwambeji.

Kamanda huyo wa Polisi hapa mkoani Ruvuma, alisema kuwa jeshi hilo linaendelea na uchunguzi kuhusiana na tukio hilo, ili kuweza kubaini sababu ya msingi iliyopelekea mtuhumiwa huyo aweze kujinyonga.

Awali wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, ndugu wa marehemu huyo kwa nyakati tofauti walifafanua kuwa wamesikitishwa na kifo cha ndugu yao wakieleza kwamba, yeye hakuvunja nyumba wala kuiba.

“Ndugu yetu tunajua alikuwa akituhumiwa na kosa la kupatikana na betri ya pikipiki ya wizi na sio kuvunja nyumba na kuiba”, walisema.  

Hata hivyo marehemu Kasumali amezikwa leo Februari 11 mwaka huu, majira ya mchana kijijini kwao Msisima wilayani Namtumbo, baada ya kuwepo kwa mvutano mkali na utata mkubwa juu ya kifo chake.

No comments: