Thursday, October 12, 2017

FUMANIZI LADAIWA KUSABABISHA GARI KUTEKETEZWA MOTO

Gari aina ya Noah linalodaiwa kuteketea kwa moto eneo la Peramiho wilayani Songea baada ya fumanizi.  
Na Albano Midelo,   
Songea.

GARI aina ya Noah limeteketea kwa moto katika eneo la Peramiho wilayani Songea mkoa wa Ruvuma.

Taarifa za awali za mashuhuda waliohojiwa katika eneo la tukio walidai kuwa gari hilo liliteketezwa, kutokana na sababu za fumanizi la mke wa mtu ambaye inadaiwa kuwa mwenye mume aliamua kuteketeza gari hilo.

Uchunguzi umebaini kwamba ubavuni mwa gari hilo ambalo limeteketea yameandikwa maneno kwa rangi nyeusi, kuwa mke wa mtu ni sumu ambapo akinamama wanne waliokutwa katika eneo hilo walidai kuwa tukio hilo lilisababishwa na fumanizi.


Mashuhuda wengine waliohojiwa walidai kuwa gari hilo liliteketea kwa sababu ya hitilafu katika injini ya gari hali iliyosababisha gari kuwaka moto na kuteketea.

Bado haijafahamika madhara ambayo wameyapata watu waliokuwemo ndani ya gari hilo iwapo walitoka salama au wamepata majeraha katika tukio hilo.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma, Gemini Mushy amethibitisha kutokea kwa tukio la gari hilo kuteketea moto katika eneo la Peramiho ambapo amesema tukio hilo lilitokea Septemba 27 mwaka huu.

“Hadi sasa Jeshi la Polisi halijui sababu ya kuteketea kwa gari hilo namba za gari hili hazifahamiki na hata mmiliki wa gari hajajitokeza Polisi kutoa maelezo ili tuweze kufanya upelelezi wa tukio hili’’, alisema Kamanda Mushy.

Mushi alisisitiza kuwa maelezo ya mmiliki wa gari hilo kwa Jeshi la Polisi yatasaidia mchakato wa bima ya gari lililoteketea, kwa sababu bima haiwezi kutolewa bila kupitia Polisi ambao wanatakiwa kufanya uchunguzi wa tukio hilo.

Kamanda Mushy ameagiza mabaki ya gari hilo yaliopo katika eneo la Peramiho jirani na Seminari kuu ya Peramiho yaondolewe kwa kuwa hayastahili kuendelea kuwepo katika eneo hilo.


Pia amemtaka mmiliki wa gari hilo kujitokeza ili kusaidia upelelezi na uchunguzi kuhusiana na tukio hilo.

No comments: