Wednesday, October 4, 2017

WAZEE MANISPAA SONGEA WALIA NA MATIBABU

Eliezer Nyoni Mwenyekiti Baraza huru la wazee Manispaa ya Songea.
Na Albano Midelo,
Songea.

WAZEE katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wameiomba Serikali kutatua kero ya kupata matibabu bure, ambayo inaongoza kwa wazee wa Manispaa hiyo hali ambayo inasababisha wengi wao kukosa matibabu.

Akisoma risala ya maadhimisho ya siku ya wazee duniani Oktoba Mosi mwaka huu, Makamu Mwenyekiti wa Baraza Huru la Wazee wa Manispaa ya Songea Sophia Hasara, alisema ni muhimu sasa kwa Serikali kuwapatia wazee hao kadi za matibabu bure kama ilivyoelekezwa hapo awali ili waweze kuondokana na kero hiyo pale wanapokwenda kupatiwa matibabu katika vituo vya serikali.

Hasara alisema kuwa kuna umuhimu kwa Manispaa hiyo kuharakisha mchakato wa upatikanaji wa kadi hizo kwa wazee wote ili kuweza kumaliza kero hiyo ambayo imedumu kwa muda mrefu na sasa inasababisha baadhi ya wazee kupoteza maisha kutokana na wakati mwingine wanashindwa kugharamia matibabu.


Wazee hao pia wameipongeza Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dokta John Magufuli kwa kuongeza bajeti ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa mwaka wa fedha wa 2017/2018 ambapo walisema bajeti hiyo itawanufaisha kwa kuweza kupata matibabu wazee wa hapa nchini.

Vilevile katika risala yao wazee hao wamelaani matukio ya mauaji ya wazee, utekaji nyara wa watoto na mashambulio mbalimbali yanayotokea kwa viongozi na kwamba ili kukabiliana na matukio hayo wameshauri Serikali kukaa na wazee ili waweze kupata mawazo ya nini cha kufanya  katika kuondoa changamoto hizo.

Walisema kuwa Serikali inapaswa kuwashirikisha wazee wa kada mbalimbali ili waweze kutumia ujuzi, uzoefu na michango ya mawazo yao katika kufanikisha malengo ya serikali.

Kadhalika walifafanua kuwa ingawa wazee hao hawana nguvu nyingi, hata hivyo kwa kutumia hekima na busara zao wanaweza kuelekeza, kushauri na kusimamia kwa ufanisi lengo kuu la awamu ya tano la kuwa na Serikali ya viwanda ili kuleta maendeleo kwa Watanzania.

Wazee hao wamesisitiza mshikamano, umoja na juhudi ili kufikia lengo lililowekwa na Serikali la Hapa kazi tu na kusisitiza kwamba itunge sheria ya wazee ili kuwezesha kunufaika na sheria hiyo kwa kuwa sera ya wazee pekee yake haina uwezo wa kutatua changamoto zao.

“Sisi wazee wa Manispaa ya Songea hatujanufaika lolote na sera ya Taifa ya wazee ya mwaka 2003 kwa sababu sera hiyo haina meno kwa kuwa haijatungiwa sheria yenye nguvu’’, walisema kupitia risala yao.

Pia wamemuomba mgeni rasmi katika maadhimisho hayo Mbunge wa Songea mjini, Leonidas Gama kuwafikishia kilio chao Bungeni na kwamba hawaoni sababu ya msingi ya kucheleweshewa kutungiwa sheria hiyo wakati sera imedumu kwa muda mrefu.


Kulingana na takwimu za wazee mwaka 2016, Manispaa hiyo ina zaidi ya wazee 11,000 hivyo katika maadhimisho hayo ya mwaka huu 2017 ni ya 19 ambapo maadhimisho ya kwanza yalifanyika mwaka 1999 na kauli mbiu ya mwaka huu ni kuelekea Uchumi wa Viwanda, Tuthamini Mchango, Uzoefu na Ushiriki wa Wazee kwa Maendeleo ya Taifa.

No comments: