Wednesday, October 4, 2017

WIZARA YA AFYA YATOA TAHADHARI UWEPO UGONJWA WA TAUNI MADAGASCAR



Imeelezwa kuwa kati ya wagonjwa 104 walioripotiwa, 20 wamefariki dunia, ambapo taarifa iliyotolewa jana Jumanne na Ofisa Habari wa Wizara hiyo, Catherine Sungura imesema kuwa Shirika la Afya Duniani (WHO) limeeleza nchini Madagascar mikoa minane  imeripotiwa kuwepo wagonjwa ukiwemo mji mkuu wa nchi hiyo, Antananarivo.

Ugonjwa huo ulianza kuripotiwa Agosti 23 hadi Septemba 28 mwaka huu.

“Wengi walioripotiwa wameonyesha kuwa na uhusiano kwa njia moja au nyingine na mgonjwa wa kwanza jambo linalothibitisha yapo maambukizi ya ugonjwa wa tauni kati ya binadamu na binadamu.

Hivyo kwa mujibu wa WHO, ipo hatari ya wastani (Moderate risk) ya ugonjwa huo kusambaa katika nchi jirani na Madagascar,” imesema taarifa hiyo.


Wizara imesema tahadhari hiyo inatolewa kwa kuzingatia kwamba, Madagascar haiko mbali sana na Tanzania na inawezekana kukawa na mwingiliano kati ya wananchi wa nchi hizi mbili.

“Serikali inasisitiza kuwa mpaka sasa ugonjwa wa tauni haujaingia nchini. Kwa kuwa magonjwa hayaangalii mipaka, tunahitaji kuchukua tahadhari madhubuti ili kuzuia ugonjwa huu usiingie nchini.

Hivyo wananchi wanahimizwa kuzingatia kanuni za afya za kuzuia ugonjwa huu, pia wanatakiwa kuripoti haraka kwenye vituo vya huduma za afya waonapo dalili zozote za ugonjwa huu,” imesema wizara.

Sungura amesema hatua zilizochukuliwa baada ya kupata taarifa ya tahadhari ya Shirika la Afya Duniani, Septemba 29 mwaka huu wamesambaza barua za tahadhari ya ugonjwa huo kwa Makatibu tawala wa mikoa yote ya Tanzania Bara.

Makatibu tawala katika barua hizo wametakiwa kuchukua tahadhari ikiwa ni pamoja na kuimarisha ufuatiliaji wa ugonjwa katika viwanja vya ndege, mipakani na bandari ili kubaini wagonjwa waingiao nchini wakiwa na dalili za ugonjwa huo.

“Kupitia kwa waganga wakuu wa mikoa na wilaya, Wizara inatoa maelekezo ya kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji na utambuzi wa magonjwa katika vituo vya kutolea huduma,” amesema.

Pia, Wizara itatoa elimu kwa jamii kuhusu ugonjwa huo.

Kuhusu tauni;

Ugonjwa huu husababishwa na bakteria anayejulikana kitaalamu, “Yersinia pestis” ambaye hupatikana katika baadhi ya wanyama wadogo kama vile panya, paka, mbwa na viroboto.

Taarifa hiyo imezitaja njia kuu tatu ambazo mtu anaweza kupata maambukizi kuwa ni kung’atwa na viroboto vyenye maambukizi ya bakteria hao kutoka kwa wanyama kama vile mbwa na paka ambao huweza kubeba viroboto.

“Kugusana bila kuwa na kinga mwili na majimaji yenye vimelea vya bakteria kutoka kwa mtu au mnyama aliyeathirika kwa njia ya kugusa sehemu zenye vimelea zilizochafuliwa na mgonjwa au mnyama na kisha mtu huyo kujigusa mdomoni au puani”, imesema taarifa hiyo.


Njia nyingine ni kugusana na majimaji yanayotoka kwa mgonjwa kwa njia ya kukohoa au kupiga chafya bila ya mgonjwa kufunika pua au mdomo. (Muungwana Blog)

No comments: