Sunday, October 8, 2017

NAMSWEA MBINGA WAFANYA TAMASHA LA MICHEZO KUHAMASISHA MAENDELEO

Upande wa kushoto mdhamini wa tamasha la michezo ikiwemo nyimbo za asili katika tarafa ya Namswea wilayani Mbinga, Thotnant Ezekiel Kayombo ambaye alikuwa mgeni rasmi katika tamasha hilo akiwa na diwani wa kata ya Namswea wilayani humo, Angelus Mbilinyi ambaye yupo katikati amevaa suti rangi nyeusi.
Washiriki wa mchezo, mpira wa miguu wakiwa katika picha ya pamoja siku ya tukio la tamasha la michezo katika tarafa ya Namswea wilayani Mbinga.
Na Mwandishi wetu,
Mbinga.

KATIKA kuenzi utamaduni wa kiafrika, Wananchi wanaoishi katika tarafa ya Namswea wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma wamefanya tamasha la michezo mchanganyiko ndani ya tarafa hiyo, ikiwa ni lengo la kuhamasisha shughuli mbalimbali za maendeleo.

Tamasha hilo lilizinduliwa hivi karibuni katika viwanja vya michezo Namswea likiwa limebeba kauli mbiu “Ujana ni hazina tuutumie vizuri kwa manufaa ya sasa na baadae” ambapo lilifadhiliwa na Thotnant Ezekiel Kayombo ambaye alikuwa mgeni rasmi huku michezo iliyokuwa ikichezwa siku hiyo ni mpira wa miguu na ngoma mbalimbali za asili.

Akizungumza na mwandishi wetu, Kayombo alifafanua kuwa lengo la tamasha hilo ni kufikisha ujumbe huo kwa jamii hasa vijana juu ya wajibu wao katika kushiriki kwenye shughuli za kimaendeleo katika maeneo yao wanayoishi.


Kayombo alisema kuwa msisitizo umewekwa pia katika shughuli za upandaji miti ya mbao na ile ambayo inatunza mazingira hasa katika vyanzo vya maji.

“Lengo ni kupanda miti laki tatu kila mwaka katika tarafa hii kwa miaka sita kuanzia sasa hadi mwaka 2022, muda ambao mimi binafsi nikiwa ndiye mdhamini nitawezesha fedha shilingi milioni 13,000,000 ambazo zitasaidia shughuli ya upandaji huu wa miti”, alisema.

Aliongeza kuwa lengo ni kufikia idadi ya upandaji miti milioni mbili katika kipindi chake cha miaka sita ya udhamini wa tamasha hilo, ili iweze kuwanufaisha wananchi hao kufanya biashara hasa pale watakapofikia hatua ya kupasua mbao na kuuza waweze kupata fedha za kufanyia maendeleo yao.

Ifikapo mwezi Disemba mwaka huu uhamasishaji wa upandaji miti hiyo kwa mfumo wa shamba darasa utafanywa pia katika shule za msingi na sekondari zilizopo kwenye tarafa hiyo ya Namswea kwa kushirikiana na wananchi ambao wameteuliwa na kwamba kufikia Januari mwaka 2018 vitalu vya kuzalisha miche ya miti vitaanzishwa.

Katika tamasha hilo washindi mbalimbali wa mchezo wa mpira wa miguu waliweza kuibuka washindi na kujinyakulia kikombe na fedha taslimu ikiwemo pia na wale walioshiriki michezo ya ngoma za asili nao waliweza kupewa zawadi na fedha taslimu ambapo kufikia mwakani michezo zaidi itajumuishwa ikiwemo mbio za baiskeli na mpira wa pete.


Hata hivyo kwa upande wao wananchi walioshiriki tamasha hilo walipongeza jitihada hizo na kueleza kuwa wapo tayari kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ikiwemo upandaji miti ili waweze kunufaika kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.

No comments: