Tuesday, September 20, 2016

SONGEA PRIVATE DISPENSARY YAFUNGIWA KUTOA HUDUMA

Na Muhidin Amri,            
Songea.

UONGOZI wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, kupitia idara yake ya afya, umeifungia zahanati moja inayomilikiwa na mtu binafsi mjini hapa kutokana na kutoa huduma za matibabu chini ya kiwango.
Damas Kayera Mganga Mkuu mkoa wa Ruvuma.

Zahanati hiyo ambayo inafahamika kwa jina moja maarufu la Songea Private Dispensary, ilifungiwa juzi kuendelea kutoa huduma hizo kutokana na kukiuka miongozo ya Wizara ya afya.

Ofisa habari wa Manispaa hiyo, Albano Midelo alisema hayo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, ambapo alifafanua kuwa hatua hiyo ilifikiwa baada ya timu ya wataalamu wa afya kubaini dosari husika.

Midelo alizitaja baadhi ya sababu zilizosababisha kufungwa kwa zahanati hiyo kuwa ni kufanya kazi ambazo haziendani na miongozo ya Wizara ya afya Ustawi wa Jamii Wanawake, Jinsia, Wazee na Watoto, kutokuwa na ikama ya watumishi ya kutosha na kukosa watumishi wenye sifa ya kutoa huduma za afya.


“Zahanati hii imefungiwa kutoa huduma hadi hapo mmiliki husika atakapokamilisha na kukidhi vigezo vya kuendesha kutoa huduma ya afya, kulingana na miongozo ya Wizara husika”, alisema Midelo.

No comments: