Monday, September 5, 2016

MKUU WA MKOA RUVUMA AZITAKA HALMASHAURI KUWATUMIA JKT KWA AJILI YA UJENZI WA MIUNDOMBINU MBALIMBALI

Kaimu mkuu wa kikosi cha 842 Kj -Mlale JKT Meja Absolomon Shausi kulia, akimkaribisha mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge kikosini hapo kwa ajili ya kufunga mafunzo ya miezi mitatu kwa vijana 1,365 kwa mujibu wa sheria, Operesheni Magufuli mwaka 2016.
Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Dkt. Binilith Mahenge akikagua gwaride rasmi la vijana 1,365 waliojiunga na mafunzo ya  kijeshi ya miezi mitatu katika kikosi cha 842 Kj- Mlale JKT kwa mujibu wa sheria Operesheni Magufuli mwaka 2016 wilayani Songea mkoani humo.



Na Kassian Nyandindi,        
Songea.

MKUU wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge amezitaka Halmashauri za wilaya mkoani humo, mpaka kufikia mwishoni wa mwezi Disemba mwaka huu zihakikishe kwamba zimekamilisha zoezi la ujenzi wa vyoo katika shule za msingi na sekondari.

Aidha ameagiza utekelezaji wa kuboresha miundombinu ya sekta ya afya ambapo kila kijiji na kata wataalamu husika, wanatakiwa kusimamia na kutekeleza ujenzi wa majengo ya zahanati na vituo vya afya.
 
Dkt. Mahenge alitoa agizo hilo juzi alipokuwa mgeni rasmi katika sherehe za kufunga mafunzo ya miezi mitatu kwa mujibu wa sheria, Operesheni Magufuli kwa vijana waliomaliza kidato cha sita katika maeneo mbalimbali hapa nchini katika kikosi cha Jeshi Mlale 842KJ zilizofanyika mkoani hapa.

“Pia naagiza halmashauri zote katika mkoa huu, watumie jeshi hili kwa ajili ya kufanya shughuli mbalimbali za ujenzi wa majengo ya maabara, shule na hata ujenzi wa matundu ya kisasa ya vyoo ili tuweze kuwafanya watoto wetu mashuleni waweze kuepukana na magonjwa ya mlipuko”, alisema Dkt. Mahenge.


Mkuu huyo wa mkoa alifafanua kuwa lengo la serikali kuanzisha mafunzo hayo kwa vijana wanaohitimu kidato cha sita, ni kuwaandaa kuwa wazalendo kwa nchi yao na kuitumikia kwa dhati katika nyanja zote za kiuchumi, siasa na kijamii.

Aliongeza kuwa mafunzo hayo huwafanya waweze kuondoa tofauti za kielimu, kikabila, kidini, kudumisha umoja, upendo na mshikamano wa kitaifa kwa lengo pia la kuthamini na kupenda kazi za mikono na kujiajiri wao wenyewe na sio kuwa na mawazo ya kupata ajira serikalini tu.

Kwa upande wake akitoa salamu kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) hapa nchini, Kanali John Mbungo wa kikosi cha JKT Mlale mkoani Ruvuma aliwataka vijana hao huko waendako waache kushabikia mambo yenye kujenga mgawanyiko katika jamii kwa sababu ya itikadi za kisiasa.

Kanali Mbungo alieleza kuwa huko waendako wakashirikiane na wananchi kupambana na wakwepa kodi na kulijenga taifa katika kutekeleza kauli mbiu ya Hapa kazi tu, na kuleta mabadiliko chanya miongoni mwa jamii.

Alisema kuwa serikali itaendelea kuboresha na kushughulikia changamoto mbalimbali zilizopo katika vikosi vya mafunzo ya Jeshi, ikiwemo kununua vifaa husika vya mafunzo kwa ajili ya kuweza kuwafanya vijana waweze kushiriki vyema wanapokuwa katika mafunzo hayo.

No comments: