Wednesday, September 21, 2016

ASKOFU AWANYOSHEA KIDOLE WANASIASA HAPA NCHINI

Na Mwandishi wetu,      
Tunduru.

ASKOFU wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Masasi mkoani Mtwara, Dkt. James Almasi amekemea tabia ya baadhi ya wanasiasa hapa nchini kutumia migongo ya waumini kupitia mashirika ya dini, kwa ajili ya manufaa yao binafsi na kuwataka kuacha mara moja tabia hiyo kwa kile alichoeleza kuwa kufanya hivyo ni dhambi na kumchukiza mwenyezi Mungu.

Badala yake alifafanua kuwa ni vyema wanasiasa wakatafuta njia nyingine mbadala ambayo itawafanya waweze kuwa salama mbele ya Mungu, kwa kutumia kipato wanachopata kwa ajili ya kuchangia na kusaidia shughuli mbalimbali za maendeleo ya wananchi katika maeneo yao.

Dkt. Almasi alitoa kauli hiyo hivi karibuni wakati alipokuwa akikabidhi  vifaa tiba, vitanda pamoja na baiskeli za magurudumu matatu  kwa ajili ya zahanati, vituo vya afya na hospitali katika vijiji 66 kwa Mkuu wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Juma Homera.

Alisema kuwa Dayosisi hiyo imekuwa mstari wa mbele kutekeleza shabaha yake kuu ya pili ya kumwezesha na kumwendeleza kila binadamu kujikomboa kifikra na kuondokana na umaskini, ikiwemo kuboresha maisha yake kwa kutumia rasilimali zinazomzunguka katika mazingira yake.


Aliongeza kuwa shabaha hiyo ndiyo inayoifanya Doyasisi ya Masasi, kushughulika na huduma za kijamii kwa kuanzisha miradi ya maendeleo katika jamii ili kuweza kuboresha afya na maisha yao.

Kwa mujibu wa Askofu Dkt. Almasi alieleza kuwa katika kipindi cha miaka 10 kuanzia mwaka 2006 Dayosisi hiyo imeweza kushughulikia miradi mikubwa ya kijamii ikiwemo pia mradi wa ufugaji bora wa ng’ombe wa maziwa ambao huwapatia wananchi waliojiunga katika vikundi vya ujasiriamali.

Dkt. Almasi alisema mradi huo ulitekelezwa katika kipindi cha miaka mitano kunzia mwaka 2006 hadi 2011 na kwamba ulihusisha usambazaji wa ng'ombe wa maziwa, mbuzi wa maziwa, ng’ombe wanaotumika kwa ajili ya  kazi za kilimo cha maksai, ufugaji samaki na nyuki kwa wananachi wenye kipato cha chini.

Alisema kuwa katika kipindi hicho familia zipatazo 12,640 zenye jumla ya watu 398,160 katika wilaya za Mtwara Mikindani, Tandahimba, Newala, Masasi, Nanyumbu, Kilwa, Lindi mjini na vijijini, Ruangwa, Nachingwea na Liwale zilinufaika na mradi huo.

Pia aliongeza kuwa mradi wa pili ni wa huduma  ya afya ya jamii na uboreshaji wa mazingira ulioanza kutekelezwa kuanzia mwaka 2012  na utamalizika mwaka 2017 ambapo unalenga kuboresha afya ya jamii katika vijiji 20 vya wilaya ya Nachingwea.

Alisema kuwa huduma zinazotolewa ni elimu ya afya, vifaa tiba na madawa katika zahanati 18 ambazo ni za serikali na usambazaji wa mifugo ikiwemo ng’ombe wa maziwa, mbuzi na uendelezaji  kuku wa kienyeji.


Pamoja na mambo mengine Askofu Dkt. Almasi alitaja miradi mingine kuwa ni usambazaji mbegu za nafaka ili kuongeza kiwango cha uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara, katika jamii na familia unaokwenda pamoja na uchimbaji visima virefu 28 vya maji safi na salama ambapo umekusudia kuwanufaisha wananchi wapatao 64,560 wa vijiji hivyo.

No comments: