Saturday, September 17, 2016

BENKI YA CRDB YAKABIDHI MSAADA WA MADAWATI NAMTUMBO

Meneja wa benki ya CRDB tawi la Songea mkoani Ruvuma, Enock Lugenge upande wa kushoto akikabidhi madawati 90 yenye thamani ya shilingi milioni 5 kwa Makamu Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani hapa, Titus Ng'oma ikiwa ni msaada uliotolewa na benki hiyo kwa ajili ya kunusuru wanafunzi wa shule za msingi  wilayani humo wasiweze kukaa chini.
Na Muhidin Amri,          
Namtumbo.

BENKI ya CRDB tawi la Songea mkoani Ruvuma, imetoa msaada wa madawati 90 yenye thamani ya shilingi milioni 5 kwa halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani humo, ili yaweze kusaidia kukabiliana na tatizo la upungufu wa madawati kwa watoto wa shule za msingi wilayani humo.

Akikabidhi madawati hayo juzi Meneja wa tawi hilo, Enock Lugenge alisema kuwa msaada huo uliotolewa ni utaratibu waliojiwekea benki hiyo ambapo  kila mwaka inagawa faida inayopatikana kwa wanahisa wake na sehemu ya faida inayobaki inarudishwa katika nyanja mbalimbali kwa kuchangia huduma za afya, elimu, maji na shughuli nyingine za maendeleo hapa nchini.

Lugenge alifafanua kuwa katika kusogeza huduma karibu na wananchi pia benki hiyo ya CRDB imefungua tawi dogo mjini Namtumbo, ambapo  hutoa huduma za kifedha wakati wote wa masaa ya kazi.


Alisema kuwa benki hiyo imelazimika kufungua tawi hilo kwa lengo la kuwawezesha wananchi kupata huduma  mbalimbali za kibenki kama vile kufungua akaunti, kuweka na kutoa fedha, huduma za ATM, bima kwa mali na magari pamoja na huduma za mikopo kwa ajili ya kuanzisha na kuendeleza miradi ya wananchi kiuchumi.

Pia Lugenge alieleza kuwa mbali na huduma hizo, CRDB inatoa mikopo kwa ajili ya watumishi, wafanyabiashara sambamba na mikopo ya pembejeo za kilimo kwa wanachama wa vyama vya kuweka na kukopa (SACCOS).

Kwa upande wake akipokea msaada wa madawati hayo Makamu Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Namtumbo, Titus Ng’oma ameishukuru benki hiyo kwa kutoa madawati hayo ambayo yatamaliza tatizo la wanafunzi kukaa chini kwa shule za msingi wilayani humo.


Ng’oma alitoa wito kwa wadau wengine kujitokeza kwa wingi kusaidia wananchi wa wilaya hiyo hasa katika sekta ya afya, maji, miundombinu ya barabara, maji na kilimo ambayo ujenzi wake bado haujakamilika.

No comments: