Wednesday, September 21, 2016

JAMII YATAKIWA KUHAKIKISHA INAPELEKA WATOTO WAO SHULE

Kutoka kulia ni Makamu Mwenyekiti wa halmashauri wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Kassim Ntara akisisitiza jambo katika sehemu ya ziara zake za kikazi wilayani humo.
Na Mwandishi wetu,          
Namtumbo.

JAMII hapa nchini imetakiwa kuhakikisha kwamba watoto wao wanawapeleka shule na kuhakikisha kwamba wanahudhuria masomo yao kikamilifu, ukizingatia kwamba elimu ndiyo urithi uliobora maishani mwao na wenye manufaa makubwa hasa katika ulimwengu wa sasa wa sayansi na teknolojia.

Mwenyekiti wa Kamati ya elimu, afya na maji baraza la Madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Kassim Ntara alisema hayo wakati alipokuwa akizungumza na madiwani wenzake wa halmashauri hiyo katika hafla fupi ya kupokea msaada wa madawati  90 yaliyotolewa na benki ya CRDB tawi la Songea kwa ajili ya shule za wilaya hiyo.

Ntara alisema kuwa kutokana na mabadiliko ya ulimwengu wa sasa ni muhimu kwa wazazi na walezi wilayani humo, wakati wote kuwekeza zaidi katika elimu kwa watoto wao, badala ya kuwarithisha vitu ambavyo baadaye vitakuwa tatizo na kuleta mifarakano katika  familia zao.


Alisema kuwa lengo la serikali  ya awamu ya tano inayoongozwa na Dkt. John Magufuli kutangaza mpango wa elimu bure kuanzia darasa la kwanza,  hadi kidato cha nne ni kutaka kuona kila Mtanzania anapata elimu ambayo  itamwezesha kukabiliana na changamoto mbalimbali katika maisha yake.

“Madawati haya yamefika kwa  muda muafaka ambapo tuna mahitaji makubwa kwa ajili ya kumaliza upungufu wa madawati kwa shule zetu za msingi na sekondari hapa Namtumbo, tunawashukuru wenzetu hawa wa CRDB kwa msaada huu”, alisema Ntara.

Ntara alieleza kuwa pamoja na kupata msaada huo lakini bado wilaya hiyo inakabliwa na changamoto ya upungufu wa miundombinu ya umeme, maabara, vyoo, nyumba za walimu madarasa na upungufu mkubwa wa walimu katika baadhi ya shule za msingi na sekondari.

Kwa upande wake Ofisa elimu msingi wa wilaya hiyo, Albert Mbilinyi ambaye pia ni Kaimu mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo ameishukuru benki hiyo katika kuunga mkono juhudi hizo huku akiwataka wadau wengine kuiga mfano huo ili kuweza kumaliza tatizo hilo la upungufu madawati wilayani humo.


Mbilinyi aliupongeza pia uongozi wa CRDB kwa kufungua tawi lake mjini Namtumbo, kwani hatua hiyo inawarahisishia wananchi wa wilaya hiyo kuweza kupata huduma za kibenki kwa ukaribu zaidi.

No comments: