Thursday, August 25, 2016

MANYANYA: SERIKALI ITAENDELEA KUSHIRIKIANA NA MADHEHEBU YA DINI AITAKA JAMII KUONA UMUHIMU WA KUPELEKA WATOTO SHULE

Na Kassian Nyandindi,              
Mbinga.

NAIBU Waziri wa Elimu, Sayansi na Tekinolojia Injinia Stella Manyanya amesema kwamba serikali hapa nchini, itaendelea kushirikiana na madhehebu yote ya dini katika kuhakikisha kwamba amani na utulivu ni jambo ambalo, linapaswa kuwepo wakati wote kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.

Aidha ameitaka jamii kuona umuhimu wa kupeleka watoto wao shule, ili waweze kusonga mbele kimaendeleo na kulifanya taifa liweze kuondokana na tabaka la watu maskini.

Injinia Stella Manyanya.
Vilevile alisisitiza kwamba, serikali haitasita kuwachukulia hatua wazazi ambao wataonekana wanakwamisha jitihada za maendeleo ya mtoto shuleni ikiwemo kufikishwa kwenye vyombo vya kisheria kama vile mahakamani.

Injinia Manyanya alisema hayo leo alipokuwa mgeni rasmi, wakati akizungumza kwenye maadhimisho ya Jubilei ya kutimiza miaka 25 ya Upadri jimbo la Mbinga, yaliyofanyika katika Kanisa la Mtakatifu Killian lililopo mjini hapa.

Maadhimisho hayo yalihusisha mapadri 11 wa kutoka Parokia mbalimbali zilizopo jimboni humo, tangu walipopata upadirisho wao Septemba 13 mwaka 1991 katika utumishi wao wa kuwatumikia wakristo wenzao.

Mapadri hao ni Philibert Mbunda, Alfredy Komba, Aidan Nchimbi, Mendrad Nyandindi, Thadei Kinyero, Christopher Mapunda, Amon Nchimbi, Addo Mapunda, Thimoth Ndunguru, Joackimu Lipanga na Bosco Ndiu.


“Ndugu zangu wakristo, tuendelee kumuomba Mungu katika shughuli zetu za kimaendeleo,  bila kufanya hivi mambo yote tunayoyafanya hapa duniani ni sawa na bure, hatuwezi kufikia malengo yetu tuliyojiwekea pasipo kutekeleza hili”, alisisitiza Manyanya.

Awali akitoa hati za baraka kwa mapadri hao, zilizotolewa na Baba Mtakatifu Papa Francis wa Kanisa katoliki duniani mbele ya waumini waliohudhuria misa takatifu ya maadhimisho hayo, Askofu mstaafu wa Jimbo la Mbinga Dkt. Emmanuel Mapunda aliwataka mapadri hao waliotimiza miaka 25 ya utumishi wao wa kikristo kuacha kumpiga vita Askofu aliyekuwa madarakani, John Ndimbo.

Pia Dkt. Mapunda alisisitiza kwa kuwataka wampatie ushirikiano wa kutosha katika kutimiza majukumu yake ya msingi, ili kuweza kuendelea kudumisha ukristo katika jimbo hilo.


Hata hivyo Askofu huyo aliongeza  kuwa mapadri hao, wanapaswa kumuomba Mungu kwa mapungufu yao waliyoyafanya au yaliyojitokeza wakati wa ukuhani wao wa kulitumikia kanisa katika kueneza dini ya kikristo ili waweze kuwa na maisha marefu.

No comments: