Tuesday, August 2, 2016

MKUU WA WILAYA TUNDURU AAGIZA ZOEZI LA UHAKIKI WANAFUNZI HEWA MASHULENI LIANZE KUTEKELEZWA

Juma Homera Mkuu wa wilaya Tunduru mkoani Ruvuma, akisisitiza jambo katika baadhi ya vikao vyake vya kikazi wilayani humo.

Na Steven Augustino,       
Tunduru.

SERIKALI wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma imewaagiza Madiwani wake, kuhakikisha kwamba wanajenga ushirikiano wa pamoja kubaini wanafunzi hewa katika shule zake za msingi ili kuweza kupambana na walimu wasiokuwa waaminifu na wenye mpango wa kuiibia fedha zake, ambazo hutolewa kila baada ya miezi mitatu kwa ajili ya kuhudumia wanafunzi mashuleni.

Aidha katika kuhakikisha kwamba jambo hilo linafanikiwa, imeahidi kuunda tume itakayofuatilia utekelezaji huo kwa kufanya uhakiki kwa shule zote za msingi wilayani humo ili kujiridhisha uhalali wa matumizi ya fedha hizo.

Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Juma Homera alisema hayo wakati alipokuwa akitoa salamu za serikali kwenye kikao cha baraza la madiwani kilichoketi katika ukumbi wa Klasta ya walimu tarafa ya Mlingoti mjini hapa.


Homera alifafanua kwamba serikali wilayani hapa inazo taarifa kwamba, wapo walimu ambao sio waaminifu wamekuwa wakipeleka orodha ya majina ya watoto wasiolingana na idadi halisi ya wanaosoma katika shule husika, ili waweze kujipatia fedha hizo za ziada kwa ajili ya kujinufaisha matumbo yao.

Kufuatia hali hiyo Mkuu huyo wa wilaya aliwataka madiwani kwenda kuhakiki shule zilizopo kwenye maeneo yao, ili wajiridhishe juu ya madai hayo yaliyopo ambayo husababisha fedha za serikali kupotea pasipo kufanya kazi iliyolengwa.

Takwimu kutoka ofisi za idara ya elimu msingi wilayani Tunduru zinaeleza kuwa wilaya hiyo ina jumla ya shule 150 za msingi, ikiwemo ndani ya shule hizo moja inamilikiwa na mtu binafsi.

No comments: