Thursday, August 4, 2016

WALEMAVU WATAKIWA KUJIUNGA NA BIMA ZA AINA MBALIMBALI



Na Muhidin Amri,      
Songea.

SHIRIKA la Bima Zanzibar limetoa mafunzo ya umuhimu wa watu wenye ulemavu katika wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, kujiunga na mifuko ya bima za aina mbalimbali ili waweze kunufaika katika maisha yao.

Watu wenye ulemavu wapatao 100 kutoka wilayani humo walipatiwa mafunzo hayo, ambayo yalifanyika kwenye ukumbi wa Chama cha akiba na mikopo cha walimu uliopo mjini hapa.

Mafunzo hayo yalishirikisha watu wenye ulemavu wa aina mbalimbali na walimu wanaofundisha wanafunzi wenye ulemavu wilayani hapa.

Akizungumza wakati alipokuwa akifungua mafunzo hayo Mkuu wa wilaya ya Songea, Palolet Mgema amelipongeza shirika hilo kwa uamuzi wake wa kutoa mafunzo hayo kwa watu hao wenye ulemavu huku akieleza kwamba ulemavu sio ugonjwa kwa kuwa wenye ulemavu, wanaweza kusoma na kujifunza kama watu wengine wasiokuwa na ulemavu.


“Natoa wito kwa jamii ni marufuku kuwaficha watoto wenye ulemavu wa aina yeyote ile majumbani kwao, hawa wenzetu wanayo haki ya kupata elimu kama wengine zipo shule za elimu maalum kwa ajili yao, tunahitaji wapelekwe huko wakasome”, alisisitiza Mgema.

Alisema kuwa serikali inaowajibu mkubwa wa kuhakikisha kwamba kundi hilo tete, linasaidiwa wakati wote kwa kila alichoeleza kuwa wapo wengine wenye ulemavu ambao wanaweza kujishughulisha hata katika shughuli za kilimo na kwamba aliahidi kuwa katika msimu ujao wa kilimo atahakikisha kwamba wanapewa msaada wa pembejeo za kilimo ili waweze kuzalisha mazao yao shambani.

Pia alisema ofisi yake itaendelea kushirikiana na vyama vya watu wenye ulemavu wilayani Songea, ikiwemo kuwasaidia kwa kuwapatia ardhi ili waweze kuzalisha mazao ya aina mbalimbali.

Kwa upande wake akitoa mada ya elimu ya bima na faida zake kwa watu wenye ulemavu ambazo hutolewa na shirika la bima Zanzibar, Meneja wa shirika hilo Kanda ya Nyanda za juu Kusini, Asha Alli amewataka walemavu hapa nchini kujiunga na bima, ili waweze kuondokana na changamoto zinazowakabili katika maisha yao kama vile matibabu pale wanapougua.

Asha amezitaja baadhi ya changamoto ambazo zinawapata watu wenye ulemavu kama vile, hatari ya kugongwa na vyombo vya moto wanapokuwa barabarani, kuibiwa na nyumba zao kuungua moto.

Kadhalika amezitaja bima ambazo hutolewa na shirika hilo kuwa ni bima za magari ya aina zote, vyombo vya moto, ujenzi, bima za wizi, fedha kwa ajili ya huduma mbalimbali, wafanyakazi na vyombo vya baharini.

Kwa mujibu wa Meneja huyo alisema kuwa mafunzo hayo yamewajengea uwezo watu wenye ulemavu katika wilaya ya Songea, ambapo baadhi yao wameamua kujiunga na bima mbalimbali zinazotolewa na shirika hilo.

No comments: