Monday, August 29, 2016

DIWANI ACHANGIA MAENDELEO KATIKA KATA YAKE AWATAKA WAZAZI KUSHIRIKIANA NA WALIMU

Na Julius Konala,      
Songea.

KATIKA kuhakikisha kwamba agizo la serikali linatekelezwa juu ya ujenzi wa vyoo bora vya kisasa katika shule za msingi na sekondari hapa nchini, diwani wa kata ya Msamala Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma Issack Lutengano kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) amechangia kiasi cha shilingi milioni 1,000,000 kwa ajili ya ukamilishaji wa ujenzi wa choo cha walimu, shule ya msingi Msamala iliyopo mjini hapa.

Mchango huo ulikabidhiwa juzi kwa Mwalimu mkuu wa shule hiyo, Mariam Kinyunyu baada ya kutoa ombi hilo kwa diwani huyo ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mahafali ya 34 ya shule hiyo, ambapo alisema kuwa katika hatua ya kwanza ya ujenzi wa choo hicho tayari zimetumika shilingi milioni mbili huku makadirio yakiwa ni shilingi milioni tatu mpaka kukamilika kwake.

Akizungumza katika mahafali hayo diwani Issack alisema kuwa atahakikisha anashirikiana na halmashauri hiyo, wazazi na wananchi wa kata hiyo katika kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili shule yake ikiwemo pia ujenzi wa vyumba vya madarasa na matundu ya vyoo.


Vilevile amewataka wahitimu hao, kujitunza kipindi hiki wanachosubiri matokeo ya mitihani yao na kwamba ametoa onyo kali kwa wale wote wenye tabia ya kuwapa ujauzito wanafunzi, waache mara moja vitendo hivyo huku akiahidi kuwachukulia hatua kali za kisheria kwa yeyote atakayehusika kufanya hivyo.

“Natoa onyo kali kwa mzazi yeyote atakayegundulika kutompeleka mtoto wake shule wakati akijua mwanaye amefaulu na kukimbilia kumuozesha, katika hili sitakuwa na huruma nitawafikisha kwenye vyombo vya kisheria”, alisisitiza Issack.

Awali  Mwalimu mkuu wa shule hiyo, Mariam alimwambia diwani huyo kuwa shule ya msingi Msamala inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo utoro wa wanafunzi, wizi wa vifaa vya walimu, kung’oa miti iliyopandwa eneo la shule, ukosefu wa ofisi ya walimu, upungufu wa vyumba vya madarasa na matundu ya vyoo.


Kufuatia hali hiyo Kaimu Ofisa elimu wa Manispaa ya Songea Castor Mbano, amewataka wazazi kushirikiana na walimu katika kudhibiti utoro na kuondoa changamoto hizo ikiwemo kuongeza kiwango cha ufaulu wa wanafunzi na atakayekaidi achukuliwe hatua za kisheria ikiwemo kufikishwa Mahakamani.

No comments: