Tuesday, August 2, 2016

MKUU WA WILAYA TUNDURU AGEUKA AWA MBOGO AWATIA MBARONI VIONGOZI WALIOHUJUMU ARDHI YA WANANCHI




Askari akiwa amewakamata viongozi wawili wa serikali ya Kijiji waliokuwa wakituhumiwa kuhujumu viwanja vya wananchi.
Na Kassian Nyandindi,

Tunduru.

MKUU wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Juma Homera amewatia mbaroni viongozi wanne wa serikali ya vijiji kwa kosa la usimamizi mbovu wa ardhi katika vitongoji vya Umoja na Frank Weston vilivyopo katika kata ya Nanjoka wilayani humo.

Akisoma taarifa mbele ya Mkuu wa wilaya hiyo, Yahaya Abdallah alimweleza Mkuu wa wilaya Homera kuwa vitongoji hivyo vimekumbwa na mgogoro wa ardhi kwa muda mrefu kati ya wenyeji, wageni na wafanyakazi wa halmashauri ya wilaya Tunduru.

Abdallah alisema kuwa serikali kupitia idara ya ardhi na maliasili wilayani humo iliwapimia ardhi wananchi wake tokea mwezi Agosti 2014 lakini ikabainika kwamba mpaka kufikia mwezo Juni mwaka huu, bado wananchi wa maeneo hayo hawakupewa ardhi yao huku orodha ikionesha kuwa baadhi ya wafanyakazi wa halmashauri pamoja na wageni wapo kwenye orodha ya wananchi wanaopaswa kugawiwa viwanja hivyo.

Akihutubia kwenye mkutano huo wa hadhara uliyofanyika katika shule ya msingi Umoja, Homera aliwaeleza wananchi kuwa wasiwe na shaka kwa sababu serikali ipo upande wao na hakuna atakaye dhulumiwa haki yake.


Ilibainika kuwa kuna baadhi ya watumishi wa idara ya ardhi na maliasili wilayani humo, ambao wamefanya ujanja ujanja kinyume cha sheria kwa kuwaweka watoto wao kwenye orodha ya majina ya wale wanaotakiwa kupewa viwanja.

Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Homera alisema hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao ili kuweza kuondoa mgongano uliopo ambao unatishia usalama wa wananchi hao.

Pia ilielezwa kuwa kumekuwa na baadhi ya viongozi wanatuhumiwa kukusanya fedha  za wananchi wapatao 522 na kutowapatia risiti, jambo ambalo imeleezwa kuwa ni hujuma za wazi za kuikosesha halmashauri ya wilaya hiyo mapato yake.

Kufuatia hali hiyo aliwataka wafanyakazi wa idara ya ardhi na maliasili wilayani humo, kujieleza ni kwa nini wamegawa viwanja kwa watu ambao sio wahusika jambo ambalo linadhihirisha wazi kuwa ni udanganyifu mkubwa ambao haupaswi kufumbiwa macho.

Kwa upande wake Mkuu wa idara ya ardhi na maliasili wilayani Tunduru, Japhet Mnyagala alikiri kufanya makosa hayo na kumhakikishia Mkuu wa wilaya hiyo, ndani ya wiki moja wananchi wataanza kugawiwa viwanja vyao na kero hiyo itakuwa imekwisha.

Hali ilibadilika baada ya muda mfupi ambapo Mkuu wa wilaya, Homera aliwaagiza askari wake wakamate viongozi waliokuwa wasimamizi wa upimaji wa maeneo hayo katika vitongoji vya Umoja na Frank Weston ambao ni Mohamed Dumsala, Matola Limelime, Halid Daud na Tekla Damas.

No comments: