Tuesday, August 2, 2016

DED MBINGA: WATENDAJI WASIOWAJIBIKA IPASAVYO WAJIANDAE KUFUKUZWA KAZI


Mkurugenzi mtendaji halmashauri wilaya ya Mbinga, Gumbo Samanditu akifafanua sheria mbalimbali za ardhi wakati wa mafunzo ya siku moja ya kuwajengea uwezo Madiwani wa halmashauri hiyo juu ya namna ya kuibua vyanzo vipya vya mapato na ukusanyaji wake kutoka kwenye vyanzo hivyo na kwamba Madiwani hao walifurahishwa na ubunifu mkubwa unaofanywa na mkurugenzi huyo, kwa mipango mizuri ya kimaendeleo ikiwemo suala la upimaji ardhi katika vijiji na miji midogo ya wilaya ya hiyo.

Na Kassian Nyandindi,         
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa Watendaji ambao wamepewa dhamana ya kukusanya mapato katika halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, endapo kama watakosa uaminifu katika kutekeleza ipasavyo majukumu waliyopewa, wajiandae kuchukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kufukuzwa kazi.

Aidha kwa wale ambao wanatabia ya kuwa wadanganyifu na kushirikiana na wafanyabiashara wajanja kutorosha mapato ya halmashauri hiyo, kwa lengo la kujinufaisha matumbo yao nao wanatafutiwa mwarobaini wao.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Gumbo Samanditu alisema hayo hivi karibuni wakati alipokuwa akizungumza na Madiwani wake kwenye ukumbi wa umati uliopo mjini hapa, juu ya uwekaji mikakati thabiti ya ukusanyaji mapato kwa halmashauri hiyo.


“Ndugu zangu Madiwani, nataka niwaambie kwamba watendaji wa namna hii tukiwabaini mimi nitawatumbua tu, sina mchezo katika hili na sihitaji kufanya mzaha wa aina yoyote ile katika majukumu yetu tuliyopewa na serikali”, alisema Samanditu.

Samanditu alisisitiza kuwa, ili kuweza kufikia malengo waliyojiwekea kuna kila sababu sasa kwa watumishi waliopewa kazi ya kutekeleza jukumu hilo kuwa waaminifu kwa kujenga ushirikiano wa pamoja wakati wa utekelezaji wa jambo hilo, kuanzia ngazi ya vijiji hadi kata.

“Kwenye suala la udhibiti tushirikiane kwa pamoja kwenye maeneo yale ya vijiji hadi kata, hatuhitaji kusikia mtu anakwepa kulipa ushuru tukimkamata tutampiga faini na Mahakamani atapelekwa ili hatua za kisheria ziweze kufuata mkondo wake”, alisema.

Aliongeza kuwa serikali ya awamu ya tano ambayo inaongozwa na Rais Dkt. John Magufuli, haipendi kuona mambo yanakwenda hovyo na endapo kama kutakuwa na kero yoyote ofisi yake ipo wazi, apewe taarifa haraka ili aweze kuchukua hatua.

No comments: