Monday, August 29, 2016

SHINDANO LA KUMSAKA MREMBO LAWANUFAISHA WAZEE SONGEA

Na Julius Konala,        
Songea.

WAANDAAJI wa shindano la kumsaka mrembo wa Miss Ruvuma mwaka huu, kutoka Rona Promotion ya Jijini Dar es salaam kupitia ufadhili wa Kampuni ya Bayauck ya nchini Japan, wametoa msaada wa nguo mbalimbali kwa baadhi ya wazee wasiojiweza katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 1,000,000.

Msaada huo ulitolewa juzi kwa wazee hao na washiriki wa shindano hilo kupitia shirika la kuhudumia wazee (PADI) lililopo mjini hapa ambapo Mkurugenzi mtendaji wa Kampuni ya Rona promotion Nassib Mahinya, alisema kuwa wameamua kufanya hivyo baada ya kuguswa na changamoto mbalimbali zinazowakabili wazee.

Mahinya alisema kuwa lengo kuu ni kuwafundisha washiriki wa mashindano ya warembo, kujitoa katika kusaidia jamii na makundi mengine yasiyojiweza huku akifafanua kuwa mapato yatakayopatikana siku ya shindano hilo litakalofanyika Agosti 27 mwaka huu, asilimia 10 itaelekezwa kusaidia jamii.


Naye mmoja wa washiriki wa shindano hilo Irene Msabaha, alisema amezitaka taasisi, mashirika na watu binafsi wenye mapenzi mema kuunga mkono juhudi hizo za kuwasaidia wazee kwa madai kuwa, bado wanakabiliwa na changamoto nyingi katika maisha yao.

Kwa upande wake mwakilishi toka shirika la kuhudumia wazee (PADI) Ndaisaba Jackson aliwashukuru waandaaji wa shindano hilo, kwa kuona umuhimu wa kuwasaidia wazee hao huku akidai kuwa kundi hilo bado linakabiliwa na changamoto ya afya, chakula, mavazi na malazi.

Akizungumza kwa niaba ya wazee wenzake Paulo Kaunda mkazi wa mtaa wa Mabatini mjini Songea, amewashukuru waandaaji wa shindano la kumsaka mrembo mkoani Ruvuma mwaka 2016 kwa kuona umuhimu wa kuwakumbuka wazee hao.


Pamoja na mambo mengine, washindi watatu wa mwanzo watakaopatikana katika shindano hilo watashiriki kwenye shindano la Kanda ya nyanda za juu kusini ambalo linatarajiwa kufanyika Septemba 9 mwaka huu kwa kushindana na warembo toka mikoa ya Iringa, Mbeya, Rukwa, Katavi na Njombe.

No comments: