Wednesday, August 31, 2016

JESHI LA POLISI RUVUMA LINAWASAKA WALIOHUSIKA NA MAUAJI NYASA

Na Kassian Nyandindi,            
Songea.

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma linawasaka watu wanaodaiwa kuhusika kuwashushia kipigo kikali kwa kuwapiga kwa mapanga, mawe na marungu watu wawili sehemu mbalimbali za miili yao ambao ni wakazi wa kijiji cha Ndumbi na Lituhi, wilaya ya Nyasa mkoani humo na kuwasababishia vifo papo hapo.
Zubery Mwombeji.

Mauaji hayo yalitokana na watu hao wakituhumiwa kwamba ni washirikina ambapo walimpoteza kimazingara, kijana mmoja aliyefahamika kwa jina la Baraka Mahundi (28) katika ziwa Nyasa.

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, Zubery Mwombeji amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba amewataja waliouawa kuwa ni Jackob Mahundi (90) mkazi wa kijiji cha Ndumbi na Vicent Ngatunga (63) wa kijiji cha Lituhi wilayani humo.


Alifafanua kuwa tukio hilo limetokea Agosti 24 mwaka huu majira ya usiku katika kijiji cha Ndumbi kata ya Mbaha wilayani humo, ambapo inadaiwa siku hiyo ya tukio watu wote wawili hao walipigwa wakiwa huko pamoja na kupoteza maisha yao.

Mwombeji alieleza kuwa chanzo cha tukio hilo kinatokana na madai ya kutuhumiwa kuhusika na vitendo vya ushirikina vilivyosababisha kumpoteza kijana Baraka Mahundi, ambaye alikwenda katika ziwa Nyasa kuvua samaki Agosti 16 mwaka huu na kwamba mpaka sasa kijana huyo hajapatikana.


Alisema kuwa juhudi za kukisaka kikundi cha watuhumiwa walioshiriki katika tukio hilo la mauaji, zinaendelea kufanywa ili watuhumiwa waweze kupatikana na kufikishwa kwenye vyombo vya dola kujibu tuhuma inayowakabili mbele yao.

No comments: