Monday, August 22, 2016

MADIWANI SONGEA WAPEWA ONYO KALI

Na Kassian Nyandindi,             
Songea.

MKUU wa wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, Palolet Mgema ameonya vikali dhidi ya kikundi cha baadhi ya Madiwani wa Manispaa ya Songea mkoani humo ambao walitaka kuleta fujo wakati wa kikao cha baraza la madiwani kilichoketi juzi mjini hapa, ambapo amesema kwamba endapo kama watarudia tena atawachukulia hatua za kisheria.

Aidha Mgema alisema kuwa kamwe hataweza kuvumilia kuanzia sasa kuona tabia hiyo inajirudia tena na kwamba, akijitokeza mtu yeyote na kusababisha kuleta vurugu zinazoashiria uvunjifu wa amani atakiona cha mtemakuni.

Mgema alisema hayo kwenye kikao cha baraza la madiwani kilichofanyika katika ukumbi wa Manispaa mjini Songea, kufuatia kutokea kwa mvutano mkali kati ya baadhi ya kikundi cha madiwani wachache wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)  na Meya wa halmashauri hiyo, Abdul Mshaweji kuhusiana na hoja ya mabasi ya kupakia abiria kuanzia stendi kuu ya zamani iliyopo mjini hapa kwenda Msamala iliyopo mbali na mji huo.

Hali hiyo ilizua tafrani ndani ya kikao hicho na kuwafanya baadhi ya wananchi waliohudhuria kuwazomea madiwani ambao walikuwa wakipindisha hoja hiyo kwa nguvu na kuwaunga mkono, Meya Mshaweji pamoja na Mbunge wa Songea mjini Leonidas Gama ambao walionyesha wazi kuwasaidia wananchi kutatua kero hiyo ya muda mrefu ya ombi lao la mabasi kuanzia stendi hiyo ya zamani.


Wakati wa kujadili hoja hiyo kikundi cha baadhi ya madiwani wachache walionekana kutoridhishwa na maamuzi ya madiwani wengi, ambao waliwatetea wananchi kwa kukubali mabasi ya abiria yaanzie katika stendi hiyo ili kuweza kuwaondolea wananchi adha waliyokuwa wakiipata kwa muda mrefu ya kwenda kupanda mabasi eneo la Msamala ambalo lipo mbali na mji wa Songea.

Mkuu huyo wa wilaya alifafanua kuwa kama diwani anahoja yake muhimu binafsi anapaswa kufuata taratibu husika, kwa kuwasilisha hoja hiyo katika mfumo ulio rasmi na sio kukurupuka ndani ya kikao na kutaka kusababisha vurugu zisizokuwa na msingi wa aina yoyote ile.

Kwa upande wake Meya wa Manispaa ya Songea, Mshaweji baada ya kuona madiwani hao hawamsikilizi huku baadhi yao wakisimama ndani ya kikao na kuchangia hoja bila kufuata taratibu, aliwaonya na kumuomba Mkuu wa wilaya hiyo, Mgema kuingilia kati kutoa karipio la kutaka kuwatoa nje ya ukumbi ndipo baadaye waliweza kutulia.


Akichangia hoja wakati wa kikao hicho naye diwani wa kata ya Ruvuma, kupitia tiketi ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Rashid Mososa alisema  yeye haoni dhambi mabasi hayo kupakia na kushusha abiria katika stendi hiyo ya zamani.

No comments: