Sunday, August 14, 2016

CHAMA CHA WALIMU MKOA WA RUVUMA CHAMPONGEZA RAIS DOKTA MAGUFULI



Na Muhidin Amri,
Songea.

CHAMA Cha Walimu Tanzania (CWT) mkoani Ruvuma, kimepongeza juhudi kubwa zinazofanywa na serikali ya wamu ya tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli kwa kukusanya kodi, kupambana na vitendo vya wizi, ufisadi na uzembe mahali pa kazi.

Aidha chama hicho kinaamini kwamba, hatua hiyo itasaidia kupatikana kwa fedha ambazo zitalipa madeni mbalimbali wanayoidai walimu serikali, ambapo kipindi cha nyuma ulipaji wake ulikuwa ukisuasua na kuwavunja moyo watumishi hao waliopo katika sekta ya elimu.
 
Hayo yalisemwa jana na Katibu wa CWT mkoani hapa, Shaibu Mohamed alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu ofisini kwake mjini Songea.

Mohamed alisema kuwa licha ya serikali kuanza kuchukua hatua dhidi ya watumishi wasiofaa ambao kwa muda mrefu wameliingizia taifa hili hasara kubwa, bado kuna umuhimu wa kuendelea na msako huo hata kwa watumishi wa ngazi ya juu ambao baadhi yao wanatumia vyeti na majina bandia kujipatia ajira katika idara na taasisi za umma.


Pia Katibu huyo ameishauri serikali kushughulikia tatizo la vyeti bandia  hata kwa wanafunzi wa  vyuo mbalimbali hapa nchini, ikiwemo vyuo vya ualimu kwa kuwa tatizo hilo limeshamiri kwa wanafunzi wa vyuo vingi vya ualimu hapa nchini.

Alifafanua kuwa katika kushughulikia tatizo hilo, wamiliki wa vyuo watungiwe sheria itakayowabana wamiliki husika kupeleka kwanza vyeti vya wanafunzi hao wanaojiunga katika baraza la mitihani la taifa, ili wachunguzwe kama wanavyeti halali au la.

“Serikali ikifanya hivyo itasaidia wanafunzi wanaoingia na wale wanaomaliza kwenye vyuo hivyo kuwa na sifa ya kushika nafasi mbalimbali za uongozi, wataweza kuwa waadilifu na wachapakazi ambao watakuwa tayari kuwatumikia Watanzania wenzao”, alisema Mohamed.

Aliongeza kuwa CWT inasikitishwa na kuzagaa kwa veti bandia pamoja na vitendo vya watumishi hewa ambao wengi wao, hawana sifa ya kuongoza au kufanya kazi katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Kadhalika alieleza kuwa hata mpango wa kutoa elimu bure kuanzia  shule za msingi hadi sekondari utafanikiwa tu, endapo serikali itamaliza kulipa madeni ya walimu, kitendo ambacho kitasaidia kurudisha moyo wa utendaji kazi zao za kila siku.

Alibainisha kwamba hadi kufikia mwezi Julai mwaka huu, walimu wa shule za msingi mkoani Ruvuma wanaidai serikali kiasi cha shilingi milioni 403.3 za mishahara, huku walimu wa sekondari nao wakidai shilingi milioni 114 mbali na madeni mengine kama vile  uhamisho na kupanda kwa madaraja.

No comments: