Thursday, August 25, 2016

WANANCHI MBINGA WAFURAHIA UPIMAJI ARDHI

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Gombo Samandito akizungumza juzi na wakazi wa kata ya Maguu wilayani humo wakati wa zoezi la uhamasishaji wananchi kwa ajili ya kazi ya kupima ardhi itakayofanywa na wataalamu wa idara ya ardhi katika vijiji, kata na miji midogo yote iliyopo wilayani hapa.
Na Kassian Nyandindi,          
Mbinga.

HATIMAYE zoezi la uhamasishaji upimaji ardhi ya wananchi katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, limepokelewa kwa mikono miwili katika vijiji, kata na miji midogo iliyopo wilayani humo ambapo wakazi waliopo katika maeneo husika kwa nyakati tofauti wamefurahia mpango huo na kuutaka uongozi wa wilaya hiyo kuanza mara moja kazi ya upimaji wa ardhi yao, ili waweze kunufaika nayo katika kusukuma mbele maendeleo yao.

Mafanikio hayo yametokana na elimu iliyokuwa ikitolewa na timu ya wataalamu ambayo iliundwa na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Gombo Samandito ambapo ilikuwa ikipita katika kila kijiji, kata na miji midogo iliyopo wilayani humo kuhamasisha juu ya umuhimu wa upimaji ardhi kisheria na kuwafanya wakazi waliopo katika maeneo husika wasiweze kujenga kiholela.

Zoezi hilo la uhamasishaji limetekelezwa kwa siku saba, ambapo lilianza rasmi Agosti 15 mpaka 21 mwaka huu likiongozwa na Mkurugenzi huyo, ambapo  imeelezwa kuwa hatua hiyo itasaidia wananchi kumiliki ardhi yao kisheria sambamba na kupewa hati ambazo watazitumia kwa ajili ya  shughuli mbalimbali za kiuchumi, kwa kupata mikopo kutoka taasisi za kifedha kama vile benki.

Jumla ya vijiji 118, kata 29 pamoja na miji minne ya Ruanda, Matiri, Kigonsera na Maguu ndiyo ambayo inatarajiwa kupimwa wilayani Mbinga ili wananchi hao waweze kunufaika na kwamba upimaji huo unatarajiwa kuanza kufanyika wakati wowote kuanzia sasa, kufuatia zoezi hilo la utoaji elimu kwa wananchi kukamilika taratibu zake.


Akizungumza kwa nyakati tofauti katika maeneo mbalimbali yaliyokuwa yakitolewa elimu hiyo juu ya umuhimu wa upimaji huo, Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Samandito alisema kuwa utekelezaji huo ni agizo la Rais Dkt. John Magufuli ambapo amezitaka halmashauri zote za wilaya, miji na manispaa hapa nchini kuhakikisha kwamba zinapima ardhi yake ili kuweza kuondoa migogoro inayoendelea kufukuta katika jamii na wamiliki husika waweze kulipa kodi kwa urahisi kwa ajili ya shughuli za maendeleo ya wananchi.

Alisema kuwa gharama za upimaji wa ardhi itakuwa shilingi 100,000 kwa ekari moja maeneo ya  vijijini na kwamba katika miji midogo itakuwa shilingi   200,000 kwa ekari  moja badala ya shilingi 300,000 ilivyokuwa hapo awali katika kipindi cha miaka ya nyuma, huku  kodi  ya ardhi kwa mwaka mmiliki halali atapaswa kulipia shilingi mia nne kwa ekari moja.

Naye mthamini wa ardhi katika halmashauri hiyo, Gabriel Kameka aliwaeleza waandishi wa habari kuwa endapo watafanikiwa kupima ardhi yote ya wilaya ya Mbinga katika miji midogo na wilaya kwa ujumla, wataweza kukusanya kodi shilingi bilioni 6.7 kwa mwaka ambayo itatokana na heka 67,000 zitakazokuwa zimepimwa.

“Hili suala ni lazima tulivalie njuga sisi sote, tujenge ushirikiano tuweze kufanikiwa, kama hatutakuwa pamoja ni sawa na kutwanga maji kwenye kinu na mafanikio tunayoyatarajia hayatakuwepo”, alisema Kameka.

Alifafanua kuwa siku zote ardhi iliyopimwa mwananchi ananufaika nayo kwa njia mbalimbali ikiwemo kwanza ni dhamana kwake, kufuatia hati aliyonayo inamfanya aweze kukopa kwenye taasisi za kifedha na kumwezesha kufanya shughuli zake za maendeleo.

Pia aliongeza kuwa zoezi hilo litaenda sambamba kwa serikali kutenga maeneo muhimu kwa ajili ya shughuli za kijamii kama vile shule, viwanja vya michezo, huduma za afya, barabara, miundombinu ya maji na maeneo ya kuzikia.

Evalina Ndimbo ambaye ni mkazi wa kijiji cha Lukiti kata ya Linda wilayani hapa alisema kuwa mpango huo endapo utafanikiwa utasaidia kuepusha migogoro mingi ya ardhi iliyopo katika vijiji, kata na miji huku wananchi waliopo katika maeneo husika wakizingatia kufuata sheria na taratibu zilizowekwa.


Kwa ujumla Wananchi wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, walisema kuwa wamefurahishwa na mpango huo wa kimaendeleo unaotekelezwa na wataalamu wake, hivyo waliahidi kujenga ushirikiano wakati zoezi hilo la upimaji mara litakapoanza ili liweze kuleta ufanisi mzuri katika jamii.

No comments: