Monday, August 22, 2016

MADIWANI WALALAMIKIA WIZI WA MADAWA HOSPITALI HALMASHAURI MJI WA MBINGA

Dkt. Robert Elisha Mganga Mkuu hospitali ya Halmashauri mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,             
Mbinga.

HALI ya upatikanaji wa madawa kwa ajili ya kutibu wagonjwa katika hospitali ya Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, imeelezwa kuwa ni tatizo sugu ambalo linaendelea kuitesa jamii hivyo serikali imeombwa kuingilia kati kutatua tatizo hilo ili wagonjwa wanaopata huduma katika hospitali hiyo waweze kuondokana na kero hiyo.

Kadhalika imefafanuliwa kwamba upungufu huo wa madawa unatokana na baadhi ya watumishi wa idara ya afya kutokuwa waaminifu, ambapo inadaiwa kuwa dawa hizo wamekuwa wakiiba na kuziuza kupitia maduka yao ya dawa muhimu yaliyopo mjini na vijijini huku wagonjwa wakilazimika kwenda kununua kwenye maduka hayo.

Hayo yalisemwa katika kikao cha baraza la madiwani wa halmashauri ya mji huo kilichofanyika juzi mjini hapa ambapo licha ya kuwepo kwa changamoto hiyo, madiwani hao pia walilalamikia baadhi ya wauguzi kuwatolea lugha mbaya wagonjwa ambao wanakwenda hospitalini hapo kupatiwa matibabu.


Pamoja na mambo mengine, diwani wa kata ya Mbinga mjini B kupitia tiketi ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Emmanuel Widambe alililamikia huduma ya jengo maalumu la kulaza wagonjwa daraja la kwanza (Grade One) lililopo katika hospitali ya mji wa Mbinga, kwamba sio nzuri kutokana na jengo hilo kujengwa chini ya kiwango ambapo nyakati za masika limekuwa likivuja na kuleta adha kubwa kwa wagonjwa.

“Mheshimiwa Mwenyekiti jengo hili halifai kwa matumizi ya wagonjwa, limekuwa likivuja hasa pale mvua zinaponyesha na pia miundombinu yake ya ndani kama vile mfumo wa maji safi na salama, katika baadhi ya vyumba imejengwa chini ya kiwango”, alisema Widambe.


Akijibu hoja hiyo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya mji huo Ndunguru Kipwele alifafanua kuwa katika msimu wa fedha wa mwaka 2016/2017 serikali itafanya ukarabati wa jengo hilo, huku akisisitiza kwamba suala la upotevu wa madawa hospitalini hapo litafanyiwa kazi ili wahusika waweze kuchukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kufukuzwa kazi.

No comments: