Thursday, November 19, 2015

DOKTA TULIA NAIBU SPIKA WA BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

Dokta Tulia Mwansasu.


BUNGE la Jamhurio ya Muungano wa Tanzania, limepitisha jina la Dokta Tulia Mwansasu kuwa Naibu Spika wa Bunge, kwa kura 250 sawa na asilimia 71.2 dhidi ya mpinzani wake, Magdalena Sakaya aliyepata kura 101 sawa na asilimia 28.8.

Idadi ya Wabunge inayotakiwa ni 394, waliosajiliwa 369, akidi ni 184 na waliohudhuria ni 351 na hakukuwa na kura iliyoharibika.

MAJALIWA NDIYE WAZIRI MKUU WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

Kassim Majaliwa.

HATIMAYE Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, muda mfupi uliopita limepitisha jina la Mbunge wa Jimbo la Ruangwa, Kassim Majaliwa kuwa Waziri Mkuu wa kwanza wa serikali ya awamu ya tano baada ya jina lake kupelekwa Bungeni na Rais wa Tanzania, Dokta John Magufuli.

Majaliwa amepitishwa kwa kura 258 sawa na asilimia 73.5 ya kura zote za ndio.

Tuesday, November 17, 2015

KATIBU WA SIASA NA UENEZI MKOA WA RUVUMA ALALAMIKIWA NA WAGOMBEA


Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

MPASUKO mkubwa huenda ukajitokeza na kukikumba Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kufuatia Katibu wa siasa na uenezi wa mkoa huo, Benedict Ngwenya kuonekana wazi akiweka mikakati ya kupanga safu za wagombea wa nafasi ya Mwenyekiti wa Halmashauri ya mji wa Mbinga wilayani humo.

Kigogo huyo wa CCM ambaye pia naye ameomba kugombea nafasi hiyo, anadaiwa kupita katika maeneo mbalimbali mjini hapa na kuwatisha baadhi ya wagombea wenzake kwamba, yeye ndiye mwenye uwezo wa kuongoza nafasi hiyo na sio mwingine.

Kufuatia kuwepo kwa malalamiko hayo, imeelezwa kuwa kitendo hicho kinachofanywa na Ngwenya, ni utovu wa nidhamu ndani ya chama ambapo viongozi wenye mamlaka ya uteuzi majina ya wagombea wa nafasi hiyo ngazi ya mkoa, endapo hawatazingatia taratibu husika huenda kukatokea mpasuko mkubwa kwa madiwani wanaotarajia kuunda Halmashauri hiyo mpya, ya mji wa Mbinga.

MKUU WA WILAYA MBINGA ALIA NA WATENDAJI WAKE

Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga.


Na Muhidin Amri,
Mbinga.

SERIKALI wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, imewaagiza watendaji wake wa Halmashauri ya wilaya hiyo kuandaa mkakati madhubuti wa kuongeza vyanzo vya mapato, vitakavyowezesha halmashauri hiyo kupata fedha nyingi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Rai hiyo ilitolewa juzi na Mkuu wa wilaya hiyo, Senyi Ngaga alipokuwa akizungumza  na mwandishi wetu ofisini kwake mjini hapa.

Ngaga alisema, Halmashauri ya Mbinga kwa kiasi kikubwa bado inaendelea kutegemea ruzuku kutoka serikali kuu kutokana na kukosa vyanzo vikubwa vya mapato na hata vilivyokuwepo, kumekuwa na udhaifu mkubwa wa usimamizi jambo ambalo linalotoa nafasi kwa wajanja wachache kutumia nafasi hiyo kujinufaisha.

MBINGA YAKABILIWA NA UPUNGUFU WA VIFAA TIBA



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

IMEELEZWA kwamba, upatikanaji hafifu wa vifaa tiba, vitenganishi na upungufu wa watumishi wenye taaluma katika kitengo cha huduma za afya ya uzazi na mtoto wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, kunaathiri utoaji wa huduma husika kwa wagonjwa.

Vilevile uhaba na ubovu wa magari, katika vituo vya afya kwa ajili ya kubebea wagonjwa ili kuwezesha rufaa ya wazazi na watoto, nalo limekuwa tatizo sugu na changamoto kubwa inayoikabili sekta hiyo ya afya wilayani humo.

Hayo yamebainishwa katika taarifa ya utekelezaji ya huduma za afya ya uzazi na mtoto wilayani Mbinga, kwa mwaka 2015 ambapo wilaya ina jumla ya vituo 63 vya huduma.

MTOTO ALIYEPIGWA KITU KIZITO KICHWANI MBINGA AMEFARIKI DUNIA



Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

MTOTO Moses Ndunguru (3) aliyekuwa akiishi na wazazi wake mtaa wa Tangi la Maji A Mbinga mjini mkoani Ruvuma, ambaye alijeruhiwa vibaya kwa kupigwa na kitu kizito kichwani na kukimbizwa Hospitali ya Misheni Peramiho wilaya ya Songea mkoani humo, amefariki dunia na kuzikwa leo katika makaburi ya Misheni yaliyopo mjini hapa.

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela.
Aidha kufuatia ukatili huo aliofanyiwa mtoto huyo, wenzake wawili ambao nao walifanyiwa hivyo walifariki dunia papo hapo usiku wa Novemba 15 mwaka huu, na miili yao kuzikwa katika makaburi yaliyopo mtaa wa Misheni Mbinga mjini.

Watoto hao wawili ambao walipoteza maisha katika tukio hilo ni, Lulu Chang’a (14) na Furaha Ndunguru (7) ambaye ni wa darasa la kwanza shule ya msingi Nyerere iliyopo mjini hapa.

Sunday, November 15, 2015

HAKI YA MKOPAJI KABLA YA KUUZA MALI YAKE

Na Bashir Yakub,
 
NILIWAHI kuandika  kuwa, mkopo  sawa  lakini  haki  za  mkopaji  zilindwe. Nikasisitiza  kuwa  kushindwa  kurejesha  mkopo  wote  au  sehemu  yake  hakuondoi  haki   za  kisheria  alizonazo  mkopaji. Katika  hilo  nilizungumzia  taratibu  mahsusi  za  kisheria  zinazotakiwa  kufuatwa  wakati  taasisi  ya  fedha  inapofikia uamuzi  wa  kuuza  dhamana  ya  mkopaji, nyumba au kiwanja.  Mara  nyingi  ukiukwaji  wa  haki  za  mkopaji  hutendwa  na  taasisi  iliyotoa mkopo  au  kampuni  za  udalali (brokers)  ambazo  hupewa  kazi  ya  kunadisha  mali  ya  mkopaji.

https://encrypted-tbn1.gstatic.com/images?q=tbn:ANd9GcR6vbG_zj2kszyl4nRMiIT7DGplvujAw_cM_8Fq90OOXeZ6qapB-gWakati mwingine yawezekana  kabisa  taasisi  ya  fedha  ikawa  imefuata  taratibu  zote za  kisheria,  lakini  tatizo  likajitokeza  kwa  dalali (brokers)  aliyepewa  kazi  ya  mnada. Na  hivyo  ndivyo  ambavyo  imekuwa  ikijitokeza   na  hiyo  ni  kwasababu  moja  tu,  kwamba  hupenda  kujipatia  faida  kubwa  na  ya  haraka katika  mali  inayonadishwa. Ni  katika  kufanya  hivyo hujikuta wamekiuka  haki  na  taratibu  za  uuzaji  kwa  ujumla.   Kwa  ufupi  haki  na  wajibu  ni  vitu  vya  kuzingatia  sana katika  miamala  ya  mkopo,  hasa  ikizingatiwa  kuwa  jambo  hilo  huhusisha  fedha  na  mali  kama  nyumba  ambamo  wakati  mwingine  ndimo  yalimo  makazi yetu.

WAWILI WAFARIKI DUNIA TUNDURU KATIKA MATUKIO TOFAUTI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

MOHAMED Layi (29) ambaye ni mkazi wa kijiji cha Namiungo wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, amefariki dunia baada ya nyumba yake aliyokuwa akiishi huku akiwa amelala kuchomwa moto, na watu wasiofahamika.

Tukio lilitokea majira ya usiku Novemba 12 mwaka huu, baada ya kufungiwa kwa kufuli nje ya nyumba yake na watu hao.

Akizungumza kwa taabu kabla ya kufariki dunia marehemu, Mohamed ambaye alikimbizwa katika Hospitali ya wilaya hiyo kwa matibabu zaidi alisema kwamba  kabla ya kukumbwa na mkasa huo, alisikia sauti za watu wawili wakizungumza nje ya nyumba yake.

HATIMAYE MIILI YA MAREHEMU WALIOUAWA LEO KIKATILI YAZIKWA KATIKA MAKABURI YA MISHENI MBINGA


Na Mwandishi wetu,

Mbinga.

HATIMAYE miili ya watoto wawili waliouawa kikatili kwa kupigwa na kitu kizito kichwani na mkazi mmoja wa kijiji cha Zomba wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Dickson Lupogo (28) imezikwa leo katika makaburi yaliyopo mtaa wa Misheni mjini hapa.

Watoto hao wawili ambao walipoteza maisha katika tukio hilo ni, Lulu Chang’a (14) na Furaha Ndunguru (7) ambaye ni wa darasa la kwanza shule ya msingi Nyerere iliyopo mjini hapa, na kwamba mazishi hayo yamefanyika majira ya saa 11:30 katika makaburi ya mtaa wa Misheni.

Kadhalika Dickson Lupogo ambaye ndiye aliyefanya unyama huo, na mwili wake kuchomwa moto na watu wenye hasira kali na kupoteza maisha, naye amezikwa kijijini kwao Zomba, baada ya ndugu zake kuwasili katika Hospitali ya wilaya hiyo na kuuchukua mwili wake.

SERIKALI YAOMBWA KUJENGA JENGO LA MAABARA MBINGA


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

SERIKALI hapa nchini, imeombwa kujenga jengo jipya la kitengo cha maabara katika Hospitali ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, kutokana na jengo linalotumika sasa, halitoshelezi mahitaji husika.

Aidha kitengo hicho hivi sasa, kinakabiliwa na mapungufu ya vitendea kazi ikiwemo vifaa tiba na dawa jambo ambalo husababisha wataalamu wa maabara katika hospitali hiyo, wakati mwingine kushindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

John Chihapula ambaye ni Mkuu wa kitengo cha maabara wilayani Mbinga, alisema hayo alipokuwa akihojiwa na waandishi wa habari ambao walitembelea hospitalini hapo, kwa lengo la kujionea changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo.

WATATU WAUAWA KIKATILI MBINGA MMOJA MWILI WAKE WACHOMWA MOTO


Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, mtu mmoja ambaye ni mkazi wa kijiji cha Zomba wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Dickson Lupogo (28) ameuawa kikatili kwa kushushiwa kipigo kikali na baadaye mwili wake kuchomwa moto na watu wenye hasira kali, baada ya kufanya mauaji ya watoto wawili na kumjeruhi mmoja.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela.
Mwandishi wa habari hizi ambaye aliwasili eneo la tukio, majira ya asubuhi leo Novemba 15 mwaka huu, alishuhudia mauaji hayo yaliyofanyika katika mtaa wa Tangi la maji A Mbinga mjini na kuelezwa kwamba, Lupogo alifanyiwa  unyama huo kutokana na kitendo chake cha kuwaua kikatili watoto hao na mmoja kumjeruhi vibaya.

Kadhalika Adrian Ndunguru ambaye ni mjomba wa Lupogo, alisema kuwa marahemu huyo alifanya mauaji hayo Januari 14 mwaka huu, majira ya usiku ambapo alienda nyumbani kwa Paulo Ndunguru katika mtaa huo wa Tangi la maji na kumweleza kwamba hawezi kurudi kijijini kwao Zomba, badala yake atalala hapo au ampeleke Polisi kwa maelezo kwamba akihofia atauawa endapo kama angerejea nyumbani kwake.

Saturday, November 14, 2015

UTARATIBU WA KISHERIA UNAPOTAKA KUNUNUA ARDHI YA KIJIJI



Na Bashir Yakub,

TULIPOANDIKA namna  bora  na  taratibu  maalum  za  kufuata unapotaka  kununua  ardhi,  tulisema  pia taratibu  za  ununuzi  wa  ardhi  huwa  zinatofautiana kutegemea  na   mazingira  ya  kila  ardhi. Tukasema  unaponunua  ardhi  kwa  msimamizi  wa  mirathi,  ni  tofauti  na  unaponunua  kwa  mmiliki  mwenyewe.

Unaponunua  ardhi  ya  familia  ni  tofauti  na  unaponunua  isiyo  ya  familia. Vilevile  unaponunua  ardhi  ya  kijiji  ni  tofauti  na  unaponunua ardhi  isiyo  ya  kijiji. Taratibu  hutofautiana  na  hasa  tofauti  ipo  katika  nyaraka  ambazo  zinatakiwa  kuambatanishwa,  ikiwa  kama  ithibati  ya  ununuzi. Hata  uandishi  wa   mkataba  wa  manunuzi  pia  nao huwa na tofauti  katika  hili.

1. ARDHI  YA  KIJIJI  KWA  UWEKEZAJI.

Wako  watu  wamekuwa   wakinunua  ardhi  hasa  huko  vijijini,  lakini  baadae  wamekuwa  wakijikuta  katika  migogoro  mikubwa  na  wenyeji. Mwamko  wa  kununua  maeneo  kama  Bagamoyo, Kisarawe, huko  Chanika  Dondwe na  maeneo  mengine  umekuwa  mkubwa  sana. Hata  hivyo  mwamko  unavyoongezeka  ndivyo  na  migogoro  inavyoongezeka. Kubwa katika  migogoro  hii  ni  hatua  ya  wanunuzi  kutokufuata  utaratibu  wa  ununuzi aidha  kwa  kujua, kutokujua  au  kupotoshwa.

Wakati  mwingine  ni  uelewa mdogo  miongoni  mwa  wenyeji,  lakini  zaidi  ni  hili  la  kutofuata utaratibu. Mara  zote  huwa  tunasema  ni  bora  zaidi  mgogoro  unapotokea  halafu  ukukute  ulifuata  taratibu  wakati  wa  manunuzi. Bila  shaka hautakuwa  na  athari  kubwa  kwako,  lakini  ni  mbaya   zaidi  ukitokea  halafu  ukukute kuna  taratibu  hukufuata kwa  bahati  mbaya  au  bila  kujua. Unakuwa  katika  hatari  ya  kupoteza. Unapokwenda  kununua  ardhi  ya  kijiji  kwasababu  yoyote  ile  hasa uwekezaji,  upo  utaratibu maalum wa kufuata  nitakaoeleza.

AFARIKI KWA AJALI YA GARI TUNDURU


Na Steven Augustino,

Tunduru.

MTU mmoja amefariki dunia na wengine 11 kujeruhiwa vibaya wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, kufuatia ajali iliyohusisha basi la kampuni ya, Asante Raby lenye namba za usajili T 136 AVA na Lory la kampuni ya Sinohydro ambayo inajenga barabara kwa kiwango cha lami wilayani humo.

Mihayo Msikhela.
Mashuhuda wa ajali hiyo walisema kuwa chanzo cha tukio hilo, kilisababishwa na dereva wa Lory aina ya Steya lenye namba za usajili T 368 BUU kuzuia basi hilo wakati likitaka kupita, ambapo baada ya ajali kutokea alikimbia na kutokomea kusikojulikana.

Akizungumzia tukio hilo wakati alipowatembelea majeruhi hao na kuwapa pole, Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Mihayo Msikhela alimtaja aliyepoteza maisha katika ajali hiyo kuywa ni, Khatib Juma Paswele (35) ambaye ni mkazi wa mjini hapa.

UJENZI WA MRADI MBINGA WAKAWAMA MKAKO NA LITOHO WAKOSA MAJI SAFI NA SALAMA



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WANANCHI wanaoishi katika kijiji cha Mkako na Litoho, Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, hawana maji safi na salama kutokana na serikali kushindwa kukamilisha ujenzi wa miradi miwili ya maji, iliyopo katika vijiji hivyo.

Aidha hali hiyo, imesababishwa na ukosefu wa fedha shilingi bilioni 1,082,199,509 ambazo mpaka sasa serikali haijazipeleka katika maeneo hayo, kwa ajili ya kuweza kufanya kazi ya ujenzi wa miradi hiyo.

Mhandisi wa maji wilaya ya Mbinga, Vivian Mndolwa alibainisha kwamba mkandarasi husika ambaye alipewa miradi hiyo kwa ajili ya ujenzi, amefikia kiwango cha asilimia 60 cha ujenzi na sasa imesimama kutokana na ukosefu huo wa fedha.

MBINGA KUNUFAIKA NA MPANGO WAKALA WA MISITU NA NYUKI



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WANANCHI wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, watanufaika na mpango uliowekwa na Wakala wa misitu na nyuki wilayani humo, wa kuwagawia mbegu za miti na kwenda kuotesha katika vitalu maalumu, ili baadaye iweze kupatikana miche ya miti ambayo itapandwa katika maeneo mbalimbali ndani ya wilaya hiyo.  

Vicent Mwafute.
Mpango huo, umekuwa ukitekelezwa kupitia vikundi ambavyo vimesajiliwa kisheria ambapo hupewa mbegu na kwenda kuzalisha miche ambayo baadaye husambazwa kwa wananchi, kwa ajili ya kwenda kuipanda katika mashamba yao.

Ofisa misitu wa wilaya hiyo, Vicent Mwafute alisema hayo alipokuwa akihojiwa na waandishi wa habari juu ya suala la utunzaji wa mazingira na misitu wilayani Mbinga.

Alisema kuwa tayari kilo 120 za mbegu ya miti rafiki ya maji, zimenunuliwa na kupelekwa kwenye vikundi husika, ili waweze kuzalisha katika vitalu na baadaye isambazwe kwa wananchi tayari kwa kupanda.

Friday, November 13, 2015

NAMNA YA KISHERIA KUZUIA MSHAHARA WA MFANYAKAZI KULIPA DENI LAKO



Na Bashir Yakub,

UNAPOMDAI  mtu  kupitia  Mahakama  na  hukumu  ikatolewa  kuwa  ni  kweli  unamdai  na  anastahili  kukulipa, basi  mtu  huyo  hustahili  kulipa.  Lakini  mara  kadhaa  hutokea  mtu  kusema  sina  hela  ya  kulipa  au  vinginevyo,  ilimradi  tu  asilipe  deni.

Lakini  pia  madai  hapa  si  lazima  iwe  hela  tu,  inayotokana  na  kukopeshana.  Yapo  pia  madai  ambayo  hutokana  na  mtu  kushinda  kesi. Kwa  mfano   mwanamke  alifungua  kesi  dhidi ya mme  wake  akitaka  matunzo  yake  na  ya mtoto/watoto.

Au shauri  limekwisha  na  mtu  aliyeshindwa  ametakiwa  na  Mahakama  kulipa  gharama. Au malipo  ya  fidia  na  mengineyo  yote  ambayo  huamriwa  na  Mahakama  kuwa  yalipwe. Haya  yote  unaweza   kuyafanya  yalipwe  kwa  kukamata  mshahara  wa  mhusika  kwa  njia  za  kisheria.

Hatua  hii imeelezwa katika amri  ya 21  ya kanuni  ya 47 sura  ya  33 sheria  ya  mwenendo  wa  mashauri  ya  madai.

Thursday, November 12, 2015

VIONGOZI TUNDURU WATAKIWA KUJENGA USHIRIKIANO NA WANANCHI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

VIONGOZI waliopo katika vijiji na kata wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wameaswa kujenga ushirikiano kwenye vikao vyao vya maamuzi mbalimbali ya kimaendeleo, ili waweze kuisaidia wilaya hiyo kufikia malengo na utekelezaji wa ahadi zilizoahidiwa na viongozi wao, wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ambao umefanyika Oktoba 25 mwaka huu.

Hayo yalisemwa na Madiwani wateule kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambao wamepewa ridhaa ya kuingia katika baraza la madiwani la halmashauri ya wilaya hiyo, wakati walipokuwa wakitoa shukrani zao kwa kuchaguliwa katika sherehe zilizofanyika kata ya Matemanga wilayani humo. 

Diwani mteule kutoka kata ya Marumba, Msenga Said Msenga alisema kuwa endapo wananchi hawatashiriki ipasavyo katika shughuli za maendeleo, mafanikio yatachelewa kuwafikia katika maeneo yao hivyo wanapaswa kujenga ushirikiano wa kutosha, ili kuweza kufikia malengo husika. 

Saturday, November 7, 2015

JE UMEACHISHWA KAZI AU WEWE NI MFANYAKAZI ZIJUE HAKI ZAKO ZA MSINGI



Na Bashir Yakub,

KUONGEZEKA  kwa  makampuni  na  taasisi  mbalimbali   kumeleta  wingi  wa  ajira  maeneo  mbambali  ya  nchi.  Mbali  na kuongezeka  kwa  ajira  kumekuwepo  na tatizo  kubwa  la  waajiriwa  kutojua  haki  zao  mbalimbali  wanapokuwa katika  maeneo  yao ya  kazi.  

Niseme  jambo  moja  tu  kuwa  hakuna  suala  la msingi  kama   muajiriwa  kujua  haki  zake. Hii  ni  kwasababu  kupitia  kujua  haki  zake  ndipo  anapoweza kupata  ujira  stahiki, posho  stahiki, masurufu stahiki, mafao stahiki, malipo stahiki  ya  kuachishwa  kazi  ikiwa  ni  pamoja  na  ujumla  wa  kufanya  kazi  kwa  misingi  ya  kazi.  

Ni  muhimu  kila  mfanyakazi  kupitia  haki  zake  mara  kwa  mara ili  kujua  nini  anapata  na  nini hapati. Uwe  kazini  au  umeachishwa  bado  ipo  nafasi  ya  kudai  haki  hizi  ili  upate kilicho  chako.

Ukitegemea  mwajiri  ndio  akwambie  haki  zako,  utakuwa  unajidanganya  kwasababu  yawezekana  kabisa  faida  kubwa ya  mwajiri  ipo  kati ya  wewe  kutokujua  haki  zako. Ni  hasara  kubwa  kufanya  kazi  bila  kujua haki  zako, kutokana  na  hilo  leo  nitaeleza   baadhi  ya  haki  za  mfanyakazi.

Friday, November 6, 2015

MWALIMU AKUTWA KWENYE MTARO AKIWA AMEFARIKI DUNIA



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

HENRY Millinga (34) ambaye ni mwalimu wa shule ya sekondari Msamala katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, amefariki dunia na mwili wake ukiwa umetupwa
ana mjini Songea na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Mihayo Msikhela zimeeleza kuwa tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia Novembkwenye mtaro wa maji machafu.

Katika tukio hilo imeelezwa kuwa pembeni ya mwili wa mwalimu huyo, amekutwa akiwa na vipande vya chupa za bia, huku katika paji lake la uso akiwa na majeraha makubwa.

Habari zilizopatika 5 mwaka huu, katika eneo la Nane nane lililopo Msamala mjini hapa.

Inadaiwa siku ya tukio hilo, Mkuu wa Polisi wilaya ya Songea alipokea taarifa kutoka kwa raia wema kwamba huko katika eneo la Nane nane Msamala kuna mtu mmoja ameonekana akiwa ametupwa katika mtaro wa maji machafu na amepoteza fahamu, ndipo jitihada za Polisi kufika eneo la tukio zilifanikiwa na baadaye kwenda katika eneo hilo kumkuta mtu huyo akiwa ndani ya mtaro huo amefariki.

Kamanda Msikhela alieleza kuwa askari Polisi wakiwa kwenye eneo la tukio, huku umati mkubwa wa watu wakijitokeza kushuhudia ndipo baadhi yao waligundua kuwa mwili wa marehemu huyo, ni mwalimu wa shule ya sekondari Msamala.

MBINGA KWAFUKUTA NAFASI YA MWENYEKITI HALMASHAURI YA MJI



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KAMPENI za chini kwa chini zinaendelea kufukuta katika Jimbo la Mbinga mjini, wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, ambazo zinalenga kumpata Mwenyekiti wa Halmashauri ya mji wa Mbinga atakayeweza kuendesha baraza la madiwani la halmashauri hiyo. 

Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi umebaini kuwa, baadhi ya Madiwani waliochaguliwa katika uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25 mwaka huu wameanza kuvutana hapa na pale, juu ya kumpata mwenzao atakayeweza kuendesha gurudumu hilo katika baraza lao.

MAGUFULI AMUAPISHA JAJI MASAJU KUWA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI

Rais Dokta John Magufuli leo asubuhi akimuapisha, George Mcheche Masaju kuendelea kutumikia nafasi ya Mwanasheria mkuu wa Serikali, katika hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam.

Thursday, November 5, 2015

MAGUFULI AANZA KAZI AMTEUA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI



Na Waandishi wetu,

Dar.

SAA chache baada ya kuapishwa rasmi kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dokta John Magufuli ameanza kazi kwa kasi ambapo leo ameanza kwa kumteua mwanasheria Mkuu wa serikali yake ya awamu ya tano, na kuitisha bunge.

Akizungumza na waandishi wa habari, kwa niaba ya serikali katika viwanja vya Ikulu Jijijini Dar es salaam Katibu mkuu kiongozi, Balozi Ombeni Sefue amesema Rais Magufuli ameanza kazi leo hii kwa kumteua Mwanasheria mkuu wa serikali ambaye ni, George Mcheche Masaju aliyewahi kushikilia nyadhifa hiyo katika serikali ya awamu ya nne chini ya uongozi wa Rais mstaafu, Dokta Jakaya Mrisho Kikwete.

USINYANYASWE NDUGU FANYA HAYA UWAPO MIKONONI MWA POLISI



IMEANDALIWA  NA  MAWAKILI WETU

( 1 )Askari  akikuweka   chini ya ulinzi  muulize  kitambulisho  ni  haki yako.

( 2 )Askari akikukamata akuoneshe  kitambulisho chenye muhuri wa mahakama  kama anasema ametumwa na mahakama kukukamata, ni haki yako.

( 3 )Askari akikukamata akwambie kwa nini anakukamata  na anakupeleka kituo gani, ni haki yako.

( 4 )Unaruhusiwa  na ni sheria kukataa kukamatwa hata kutumia nguvu kama hukuambiwa  sababu  ya  kukamatwa.

( 5 )Askari anapokiuka taratibu za ukamataji anageuka na kuwa  mhalifu  ni haki  yako kujikinga naye.

MBINGA WANUNUA MTAMBO WA KUNYONYA MAJI TAKA

Gari ambalo limenunuliwa kwa ajili ya kunyonya maji taka, mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

HALMASHAURI ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, imeweza kuondokana na mfumo wa kukodi gari la kunyonya maji taka kutoka Manispaa ya Songea mkoani humo, baada ya kununua gari lake ikiwa ni mikakati yake ya kuhakikisha kwamba wakazi wa mji huo wanaondokana na kero hiyo.

Gari hilo ambalo ni aina ya FAW lenye namba za usajili, SM 11483 limenunuliwa kwa fedha za kitanzania, shilingi milioni 164,654,000.

Akizungumza na mwandishi wetu, Mkurugenzi mtendaji Halmashauri ya mji wa Mbinga, Oscar Yapesa alisema kuwa lengo la kununua gari hilo ni mpango uliowekwa muda mrefu, ili kuweza kuboresha makazi na mazingira ya mji huo kuwa katika hali nzuri.

Wednesday, November 4, 2015

NDUGU JITETEE HIVI UWAPO MAHAKAMANI




IMEANDALIWA  NA  MAWAKILI WETU


( 1 ) Kama  unahojiwa na  Wakili mahakamani  usijibu  bila kutafakari alichokuuliza.

( 2 ) Wakili  asikuogopeshe kwa ukali  anapokuuliza  kwani  ukali hulenga kuleta paniki na kukusahaulisha  ulichopanga kusema.

( 3 ) Usilazimishe  kujibu kitu ambacho hukijui ni bora kusema  sijui kuliko kulazimisha kujibu.

( 4 ) Penda sana kujiamini  kwakuwa kujiamini  hupunguza  uwezo wa  Yule anayekuuliza, hata awe Jaji/Hakimu.

( 5 ) Jitahidi  kupata ushauri  wa wanaojua  sheria  kwa  kila hatua unayopiga  katika  kesi.

( 6 )Kama we  ni  shahidi hakikisha unajadiliana  vya kutosha  na Yule unayemtolea ushahidi  kabla  hamjaingia mahakamani.

DED MADABA AWATAKA WATENDAJI KUWAJIBIKA KATIKA MAENEO YAO YA KAZI



Na Mwandishi wetu,
Madaba.

MKURUGENZI Mtendaji Halmashauri ya wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma, Robert Mageni amewataka watendaji wa vijiji, mitaa  na kata  katika wilaya hiyo kushughulikia matatizo ya wananchi katika maeneo yao ya kazi, na sio kuwaacha wakitaabika peke yao bila kupatiwa ufumbuzi wa haraka.

Mageni alitoa rai hiyo alipokuwa akizungumza na  Madiwani wapya na Mbunge mteule wa Jimbo la Madaba, Joseph Mhagama wakati wa hafla fupi ya kuwakabidhi vyeti vya utambulisho pamoja na kupeana mikakati ya utekelezaji wa mipango mbalimbali  yenye lengo la kuongeza kasi ya maendeleo na ufanisi wa kuwatumikia wananchi, iliyofanyika mjini hapa.

UWT MBINGA YALALAMIKIA WANACHAMA WAKE

Baadhi ya akinamama wa UWT Mbinga mkoani Ruvuma, wakiwa katika picha ya pamoja na mganga mfawidhi wa Hospitali ya wilaya hiyo, Dokta Robert Elisha walipotembelea hospitalini hapo kuona wagonjwa hivi karibuni.


Na Muhidin  Amri,
Mbinga.
 
JUMUIYA ya Umoja wa Wanawake Chama cha Mapinduzi (UWT) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma imesema, haitawavumilia wanachama wa umoja huo ambao walikisaliti chama katika uchaguzi mkuu  uliofanyika Oktoba 25 mwaka huu, ambapo kinaweka mikakati ya kuwachukulia hatua wale wote walioonekana kwenda kinyume na matakwa husika, ikiwa ni lengo la kulinda heshima na maadili ya chama hicho.

Pendo Ndumbaro ambaye ni Mwenyekiti wa umoja huo wilayani humo, alitoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na wanachama wake katika mkutano wao, uliofanyika ukumbi wa jumba la maendeleo mjini hapa.

Alisema baadhi ya wanachama, walishindwa kukisaidia chama katika mchakato mzima wa uchaguzi mkuu huku wengine wakipigia debe vyama vya upinzani, ili CCM kisiweze kupata ushindi katika uchaguzi huo.

NALICHO NAMTUMBO AKEMEA WANAOHUJUMU MIUNDOMBINU YA BARABARA



Na Muhidin Amri,
Namtumbo.

MKUU wa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Chande Nalicho amekemea tabia ya baadhi ya watu wasiojulikana kuhujumu miradi  ya barabara  ikiwemo kung’oa alama za barabarani, ambazo husaidia watumiaji kutambua vizuri wanapokuwa barabarani  na kuepusha ajali zisizokuwa za lazima.

Nalicho ametoa kauli hiyo kufuatia kuwepo kwa baadhi ya watu, kuanza kuharibu alama zilizowekwa barabarani katika barabara mpya ya Namtumbo  hadi Songea ambayo ujenzi wake, umekamilika na kuanza kutumika.

Alisema kuwa licha ya uharibifu huo unaofanywa na watu hao, wamekuwa pia wakiiba baadhi ya vifaa kama vile mabomba na alama nyingine ambazo husaidia watumiaji wake kutambua na kuwa waangalifu wanapokuwa barabarani, jambo ambalo husaidia kupunguza kiwango cha ajali hasa kwa watembea kwa miguu.

UWANJA WA SHERIA: KUMLAZIMISHA SHAHIDI KUFIKA MAHAKAMANI

Na Bashir Yakub,

KESI /shauri  lolote  iwe  jinai  au madai  kuishinda kwake  mara nyingi  hutegemea  mambo  makuu  mawili. Kwanza  mashahidi, pili  ushahidi. Mashahidi  siku zote ni  watu. Hakuna  kitu  kinaweza  kuitwa  mashahidi  halafu  kisiwe  binadamu. Hii ni  tofauti  na  ushahidi. Ushahidi   si  lazima  wawe  binadamu.   Vitu hasa  vizibiti(exhibit)  ndivyo  huitwa  ushahidi. Nyaraka, mali,  vifaa,  na  kila  kitu  ambacho  mtu  anaweza kukitumia  mahakamani kuthibitisha  kile  anachokisema huitwa ushahidi. Yumkini  yawezekana  wakati  huohuo  mmoja  ukawa  na  vyote  yaani  ushahidi  pamoja na  mashahidi  hapo hapo. Hii  hutegemea namna mtu  alivyojiandaa  katika    kuwasilisha  kesi  yake.

1.SIFA  ZA  SHAHIDI.

Si  kila  mtu  ana  sifa  za  kuwa  shahidi. Shahidi  hutakiwa  kuwa  mtu  mkweli, muaminifu  na  muadilifu.  Lakini  pia  sifa  kuu  ya  shahidi  ni  kuwa  na  akili  timamu.  Mtu  asiye  na  akili  timamu  hawezi  kuwa  shahidi. Lakini  pia  mtu  mwenye  sifa   ya  uongo  hasa  huko  nyuma  kama  aliwahi  kutoa  ushahidi  wa  uongo  mahakamani  na  ikathibitishwa  kuwa  alitoa  ushahidi  wa  uongo   basi  naye  hupoteza  sifa  ya  kuwa  shahidi.   

Pia  sifa  nyingine  kuu  ya  shahidi   ni  muhimu  awe  ni  yule  aliyeona,  kuhisi  kwa  kutumia  moja  kati  ya  viungo  vyake,   au  kusikia .  Hii  ina  maana  shahidi  hutakiwa kuwa yule  anayelijua  tukio  kwa  kulishuhudia  na  si  vinginevyo.

Monday, November 2, 2015

UKAWA RUVUMA YAANGUKIA PUA YASHINDWA KUTAMBA MBELE YA CCM



Na Steven Augustino,
Ruvuma.

WAGOMBEA ubunge katika majimbo tisa kupitia  vyama vinavyounda umoja wa katiba ya wananchi (UKAWA) mkoani Ruvuma, wameangukia pua na kushindwa kufurukuta kwa wagombea wa nafasi hiyo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya kushindwa vibaya katika matokeo ya uchaguzi uliofanyika Oktoba 25 mwaka huu.

Kufuatia  hali hiyo mkoa huo, umeendelea kubaki kuwa ngome kubwa ya CCM kwani hata katika kura za urais mgombea wake, Dokta John Magufuli ameibuka kidedea kwa kumshinda mpinzani wake, Edward Lowassa wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ambaye aligombea kupitia  UKAWA.

Katika wilaya ya Tunduru yenye majimbo mawili ya uchaguzi, Mbunge wa jimbo la Tunduru Kaskazini, Mhandisi  Ramo Makani alifanikiwa kutetea nafasi yake baada ya kupata kura 29,841 dhidi ya kura 29,102 alizopata mgombea wa Chama Cha Wananchi CUF, Manjolo Kambili huku mgombea wa ACT wazalendo, Mohamed Khalifa akiambulia kura 838.

MADIWANI NA WABUNGE WATEULE MBINGA WATAKIWA KUSIMAMIA MAENDELEO


Na Steven Augustino,

Mbinga.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Mbinga  mkoani Ruvuma, kimewataka madiwani na wabunge wateule kufanya kazi za kuwatumikia wananchi,  ili kuondokana na tatizo la umaskini unaoendelea kutafuna wananchi wa wilaya hiyo.

Hayo yalisemwa na Katibu wa CCM wa wilaya ya Mbinga, Zainabu Chinowa alipokuwa akizungumza na viongozi hao wateule na baadhi ya wanachama wa Chama hicho kwenye sherehe fupi ya kuwapongeza iliyofanyika ukumbi wa Mbicu hotel uliopo mjini hapa.

Alisema yeye kama mtendaji mkuu wa chama ngazi ya wilaya, amefurahishwa na matokeo ya uchaguzi wa mwaka huu kwa sababu yameonesha bado chama hicho kinapendwa na wananchi, tofauti na baadhi ya watu wengine wanavyofikiri.