Thursday, October 2, 2014

WAKULIMA WA KAHAWA WAIANGUKIA SERIKALI, WAITAKA KUENDELEA KUIWEZESHA TaCRI

Meneja Kanda ya kusini wa Taasisi ya utafiti wa zao la kahawa kituo cha TaCRI - Ugano kilichopo makao yake makuu wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, Godbless Shao akitoa maelezo mafupi juu ya maendeleo ya zao la kahawa kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) walipokuwa katika kijiji cha Kilimani wilayani humo hivi karibuni.
Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

WAKULIMA wa kahawa wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wameitaka serikali kuendelea kuiwezesha taasisi ya utafiti wa zao hilo hapa nchini (TaCRI) kwa lengo la kuboresha uzalishaji kwa wakulima binafsi na waliopo katika vikundi, ili waweze kuzalisha miche ya kahawa kwa wingi.

Sambamba na hilo pia wameshauri halmshauri za wilaya mkoani humo ambazo hujishughulisha na kilimo cha kahawa, kuongeza maeneo ya uzalishaji kwa kufuata kanuni bora za kilimo, ikiwemo matumizi ya aina mpya ya miche ya kahawa (vikonyo) ambayo haishambuliwi na wadudu waharibifu kwa urahisi.

Rai hiyo ilitolewa na wakulima hao walipokuwa wakizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti, ambao waliwatembelea kuona changamoto wanazokabiliana nazo na faida wanazopata baada ya TaCRI kutoa huduma zake.

Mkulima Festo Mapunda wa kijiji cha Sepukila wilayani Mbinga alisema, umefika wakati sasa ni muhimu kuendelea kuunga mkono jitihada zinazofanywa na taasisi hiyo kwani yeye na wakulima wenzake baada ya kupata elimu ya uzalishaji wa kahawa bora, wameweza kuongeza uzalishaji kutoka robo kilo kwa mti mmoja hadi kufikia kilo mbili au zaidi.

Godbless Shao akiwa katika bustani mama, ya kuzalishia miche ya kahawa TaCRI - Ugano iliyopo wilayani Mbinga.
“Kiuchumi tulikuwa chini sana, lakini hivi sasa kwa kuzingatia kanuni bora za kilimo cha zao hili tunaweza kupata kahawa nyingi na yenye ubora unaokubalika ambayo tukishapeleka mnadani kwa mauzo, tunapata fedha na maisha yetu kiuchumi yanazidi kusonga mbele tofauti na miaka ya nyuma”, alisema Mapunda.

Naye Ernest Komba wa kijiji cha Mtama wilayani humo ambaye pia ni mjumbe wa TaCRI, alifafanua kuwa changamoto kubwa wanayokabiliana nayo wakulima wa wilaya ya Mbinga ni upatikanaji wa aina mpya ya miche ya kahawa huku akiishauri serikali kuongeza nguvu kwa taasisi hiyo, ili iendelee kutoa elimu kwa wakulima namna ya kuzalisha miche hiyo na sio kuiachia kazi hiyo peke yake.

“TaCRI ni msaada mkubwa sana kwa sisi wakulima katika kuendeleza zao hili la kahawa, ni vyema serikali iongeze ruzuku kwa taasisi hii ili miche izalishwe kwa wingi kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho”, alisema Linus Komba mkulima wa kijiji cha kilimani.

Pamoja na mambo mengine Meneja wa taasisi hiyo kituo cha Ugano Kanda ya kusini Godbless Shao, alieleza kuwa wamekuwa wakifanya kazi katika Halmashauri 12 zilizopo kwenye mikoa ya Iringa, Njombe na Ruvuma ambazo huzalisha kahawa.

Shao alisema wamekuwa wakielimisha wakulima katika mikoa hiyo juu ya uzalishaji wa miche ya vikonyo, ambapo bustani mama za kuzalishia miche hiyo zimejengwa katika kila halmashauri ikiwa ni lengo la kuongeza uzalishaji wa kahawa.

“Kila halmashauri zinao wajibu wa kuhakikisha bustani hizi za kuzalishia miche ya kahawa zinatunzwa vizuri, endapo tutazingatia hili uhaba wa upatikanaji wa miche hii utapungua”, alisema.

Kadhalika alieleza kuwa mwitiko wa wakulima kupanda aina hiyo mpya ya kahawa ambayo haishambuliwi na wadudu kiurahisi umekuwa mkubwa, hivyo kinachotakiwa ni kwamba wataalamu wa ugani katika halmashauri husika kuendelea kutimiza majukumu ya kazi zao za kila siku ipasavyo ili kuweza kuongeza kasi ya uzalishaji.

Katika hatua nyingine Meneja huyo alishukuru jitihada zinazofanywa na Jumuiya ya nchi za watu wa ulaya (EU) katika kuwawezesha ufadhili wa fedha za kuendesha shughuli za TaCRI kwa manufaa ya wakulima wanaozalisha zao la kahawa na Taifa kwa ujumla.

No comments: