Sunday, June 8, 2014

ASASI ZISIZO ZA SERIKALI WILAYANI MBINGA LAWAMANI

Ofisa maendeleo ya jamii Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Paschal Ndunguru akisisitiza jambo alipokuwa akifungua mkutano wa Wadau mapambano dhidi ya UKIMWI uliofanyika kwenye ukumbi wa shule ya sekondari Kigonsera uliopo wilayani humo. Katikati ni Mwenyekiti wa Mamlaka ya mji mdogo wa Mbinga Steven Matesso na upande wa kulia ni Ofisa maendeleo ya jamii Henry Digongwa, anayeshughulikia kitengo cha UKIMWI na tiba. (Picha na gwiji la matukio mkoani Ruvuma)



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

IDARA ya Maendeleo ya Jamii katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, imezinyoshea kidole baadhi ya asasi zisizo za kiserikali wilayani humo kwamba, hazitekelezi majukumu yake ya kazi ipasavyo.

Sambamba na hilo imeelezwa kuwa taarifa za kazi inazofanya hazitolewi kabisa juu ya nini asasi husika inafanya, jambo ambalo ni kinyume na taratibu zilizowekwa wakati zinasajiliwa na kupewa majukumu ya kwenda kuyafanya.

Kauli hiyo ilitolewa na Ofisa maendeleo ya jamii Henry Digongwa anayeshughulikia kitengo cha UKIMWI na tiba, katika halmashauri hiyo alipokuwa kwenye mkutano wa siku mbili na Wadau wa mapambano dhidi ya ugonjwa huo, uliofanyika ukumbi wa shule ya sekondari Kigonsera iliyopo wilayani humo.


“Ndugu zangu kazi ya asasi ni kuisaidia serikali katika kutekeleza majukumu yake, taarifa hazitolewi kabisa juu ya nini mnakifanya nahitaji mbadilike”, alisema Digongwa.

Digongwa alisisitiza kuwa hivi sasa umewekwa utaratibu kwamba, asasi ambayo itakuwa haiwajibiki ipasavyo katika maeneo yake ya kazi na kutoa taarifa zake kwa wakati, zitafutiwa usajili wake.

Awali akifungua mkutano huo, Ofisa maendeleo ya jamii wa wilaya ya Mbinga, Paschal Ndunguru naye alizitaka asasi zisizo za kiserikali wilayani humo kujenga ushirikiano wa kazi zao na serikali, na sio kusubiri mpaka wasukumwe.

“Tuwajibike kwa yale ambayo tumejiwekea sisi wenyewe, kazi yenu ndugu zangu mnatakiwa kupembua matatizo ambayo jamii inayowazunguka inakabiliana nayo”, alisema.

Hata hivyo aliongeza kuwa kazi ya serikali ni kuona asasi hizo, zinaendelea kuelimisha jamii katika kupambana na ugonjwa wa UKIMWI ili kuweza kupunguza kasi ya maambukizi ya ugonjwa huo.


No comments: