Sunday, July 19, 2015

TINGA TINGA NA MIKAKATI YA MAENDELEO KATA YA MTIPWILI NYASA

Stanford Nyambo (Tinga tinga)
Na Dustan Ndunguru,

MWAKA huu unatarajiwa kufanyika uchaguzi mkuu ambapo Madiwani, Wabunge na Rais watachaguliwa na kuongoza kwa kipindi cha miaka mitano ijayo, ambapo uchaguzi huo utafanyika kwa kuvihusisha vyama ambavyo vimesajiliwa kisheria.

Chama Cha Mapinduzi (CCM) ndicho chama kinachoongoza nchi ya Tanzania kwa kipindi kirefu sasas, kwa kuhakikisha amani na utulivu kwa wananchi wake vinaendelea kuwepo.

CCM ni chama ambacho Watanzania wengi wanakiamini na kukichagua kushika dola tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992.

Watanzania hawa wameamua kwa dhati kuwachagua wagombea waliotokana na chama hiki tawala, kutokana na kuridhishwa na sera zake nzuri ambazo kimsingi zimekuwa zikilenga kuwaletea maendeleo wananchi, ikilinganishwa na sera za vyama pinzani.


Udiwani ni moja kati ya nafasi ambayo wanachama wa CCM, watakuwa na haki ya kuchagua au kuchaguliwa kama katiba ya chama inavyosema ambapo wakati ukifika kura za maoni ndani ya chama zitafanyika na kupatikana wagombea ambao wataingia kwenye kinyang’anyiro cha uchaguzi mkuu ambako pia wapinzani nao watasimamisha wagombea wake.

Kila chama cha siasa kimejiwekea utaratibu wake wa kuwapata wagombea, ambao watasimama siku hiyo ambayo utafanyika uchaguzi mkuu huku wananchi wakiwa na wajibu wa kuwapigia kura wale ambao wanaimani nao kwamba, wakishinda watashirikiana nao vyema katika kujiletea maendeleo.

Chama cha mapinduzi, kinao utaratibu wake ambao kimejiwekea ikiwa ni njia ya kuwapata wagombea wake watakaosimama kwa niaba ya chama, ili wapigiwe kura na wananchi.

Utaratibu uliowazi kwa sasa ni ule wa upigaji kura za maoni, wanachama wa chama hicho watawapigia wagombea watakaojitokeza kuomba nafasi za udiwani, ubunge na urais ambapo kwa wale ambao watasimamishwa na chama wataweza kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi huo. 

Majimbo na kata mbalimbali za uchaguzi hapa nchini, wanachama wa chama hiki tawala wamekuwa wakijitokeza na kutangaza nia yao ya kugombea kwa nafasi hizo, ambapo watachujwa katika kura za maoni ndani ya chama kabla ya uchaguzi mkuu kufanyika.

Kata ya Mtipwili iliyopo mkoani Ruvuma, ni moja kati ya kata ambayo wanachama wa chama hicho wamejitokeza na kutangaza nia ya kugombea kwa nafasi hiyo ya udiwani, ambapo kata hivi sasa inajumuisha vijiji vya Matenje, Mtipwili, Chiulu na Malini.

Stanford Nyambo kwa jina maarufu Tingatinga, ni mmoja kati ya wanachama wa chama cha mapinduzi ambaye ametangaza nia yake ya kugombea nafasi hiyo na kuelezea  mikakati yake atakayoitekeleza endapo kama wananchi wa jimbo hilo watampatia ridhaa ya kuwaongoza.

Nyambo  anasema kimsingi wananchi wake wamekuwa wakijihusisha na shughuli za uvuvi, kilimo cha kahawa ikiwa ni njia kuu ya uchumi pamoja na uchimbaji mdogo wa madini huku wengine wakijishughulisha, na uzalishaji wa mazao mbalimbali ya chakula.

Kupitia uvuvi na kilimo anasema atahakikisha anatafuta zana za kisasa za kufanyia shughuli zao, kwa lengo la kuimarisha shughuli za uvuvi kwa wavuvi, ili waweze kupata mapato makubwa na hatimaye wajikwamue kiuchumi.

Anasema anaamini kwamba kama atachaguliwa kuwa mwakilishi wao atashirikiana na wakulima, kuzalisha mazao bora ya chakula na biashara ambayo yatapata bei nzuri sokoni.

Kwa upande wa kilimo atahakikisha uzalishaji wa korosho na mazao mengine kama vile ufuta na mpunga, vinapewa kipaumbele kutokana na ukweli kwamba mazao hayo hustawi vizuri katika kata ya Mtipwili.

Kuhusu masoko ya mazao yatokanayo na uvuvi, kilimo anaelezea kuwa atahamasisha uundaji wa vikundi vya ujasiriamali, ambavyo wataalamu wa kilimo wataweza kuwafikia wanachama husika kwa urahisi na kuwapa elimu ya uzalishaji bora wa mazao yao.

Anasema kauli mbiu yake ya “Pambazuko jipya la maendeleo” katika kata ya Mtipwili itasaidia kufikia mafanikio wanayotarajia kuyapata wananchi na kwamba amedhamiria kuisimamia kwa dhati kauli mbiu hiyo, katika kipindi chote cha utawala wake kama atapewa ridhaa na wananchi kuwaongoza.

Anafafanua kuwa zipo changamoto mbalimbali, ambazo wazalishaji wa mazao wanakabiliana nazo hivyo yeye binafsi atahakikisha anashirikiana nao kikamilifu, katika kuzikabili changamoto hizo.

Kuhusu mazao mengine anasema kuwa atahamasisha wakulima wazingatie maelekezo ya wataalamu husika, ili waweze kuzalisha kwa wingi hasa ikizingatiwa yapo mazao kama vile mahindi, ulezi, matunda na mengineyo yanastawi vizuri katika maeneo mbalimbali ya jimbo hilo.

Nyambo anazungumzia pia sekta ya elimu, afya, maji na miundombinu ya barabara kwamba atashirikiana na serikali na wananchi kwa ujumla, ikiwa ni lengo  la kuboresha sekta hizo muhimu.

Anasema miundombinu katika baadhi ya maeneo ya kata hiyo ni mibovu, jambo ambalo wananchi hupata shida hasa nyakati za masika wakati wa kusafirisha mazao yao na hata huwawia vigumu kuwafikisha wagonjwa katika hospitali ya wilaya ya Nyasa pale wanapotakiwa kupatiwa matibabu.

Anasema atahakikisha kila eneo katika kata,  linafikika kwa urahisi kwa kuondoa vikwazo vyote akihakikisha serikali inajenga madaraja ya kudumu na vivuko vya uhakika ambavyo vinapitika wakati wote.

Iwapo kama atapata ridhaa ya wananchi kuwaongoza kata hiyo,  atakuwa na vikao vya mara kwa mara na wananchi kabla na baada ya vikao vya baraza la madiwani,  ili kupata maoni ya wapiga kura wake na kuimarisha umoja na upendo.

Tingatinga anabainisha kuwa kata ya Mtipwili ina fursa nzuri ya kuharakisha maendeleo na uchumi kwa ujumla hasa ikizingatiwa kata hiyo ina mazingira mazuri, ambayo kama yatafanyiwa kazi ipasavyo vipato vya wananchi vitaongezeka.

Anasema wananchi wanalojukumu kubwa la kubadilisha mtazamo wao ili waweze kufikia kiu ya maendeleo waliyonayo sasa na kuondokana na umaskini jambo ambalo linahitaji kiongozi makini, ambaye ana uchungu wa dhati juu ya wananchi wa kata yake.

Tingatinga  anasema kuwa kinachotakiwa sasa kwa wanachama wa chama cha mapinduzi, kuhakikisha wanakuwa makini kuwachagua viongozi ambao watawapa maendeleo ya kweli na wajihadhari na wagombea ambao wanamawazo mgando ikiwemo hutumia fedha kununua uongozi.

Anasema kuwachagua wagombea kwa sababu ya fedha walizonazo huku uwezo wa kuongoza ni mdogo, haina maana kwani mwisho wa siku watajikuta mwakilishi wao akijilimbikizia mali.

Kuhusu chama cha mapinduzi anasema yeye anatambua wazi kuwa ni mwanachama halali wa CCM, hivyo kama atachaguliwa kuwa mbunge atahakikisha anarejesha matunda kwa chama chake ambapo kwa kushirikiana na wanachama kila tawi litakuwa na ofisi yake ya tawi na kuongeza idadi ya wanachama.


Tingatinga ambaye pia ni katibu wa itikadi na uenezi wa wilaya ya Nyasa anasema pamoja na wadhifa huo pia amewahi kuwa Mwenyekiti wa tawi la Mtipwili, wa CCM wa kata hiyo na wa baraza la migogoro la kata ambapo katika kipindi chake cha uongozi wa chama alihimiza pia kufungua matawi ya Mtulima, Likalo B, Tembwe na Mtulivu wilayani Nyasa.

No comments: