Sunday, July 5, 2015

BIBIYE AGONGWA NA LORI AFARIKI DUNIA

Na Steven Augustino,
Tunduru.

MFANYABIASHARA mmoja ambaye ni maarufu kwa kuuza viazi vitamu, katika kitongoji cha Ng’apa kijiji cha Namiungo wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, Bibiye Yasin Mkao (43) amefariki dunia baada ya kugongwa na lori.

Chanzo cha ajali hiyo kimeelezwa kuwa kimetokana na dereva aliyekuwa akiendesha gari lenye namba za usajili, T 442 CBM ambalo ni mali ya kampuni ya kichina Synohdro, inayojenga barabara kwa kiwango cha lami kutoka wilaya ya Tunduru kwenda Mangaka mkoani Mtwara.

Diwani wa kata hiyo, Nurdin Mnolela alisema marehemu huyo aligongwa na lori hilo la kichina aina ya Howo Syno truck ambalo lilikuwa likiendeshwa na dereva, Noel Beda ambaye mpaka sasa ametokomea kusikojulikana.


Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela alisema kuwa wamejipanga kumsaka mtuhumiwa wa tukio hilo, kwa lengo la kumfikisha Mahakamani ajibu tuhuma inayomkabili.

Dokta Joseph Ng’ombo ambaye aliufanyia uchunguzi mwili wa marehemu Mkao, alisema kuwa chanzo cha kifo hicho kilitokana na kutokwa na damu nyingi, baada ya kupasuka fuvu la kichwa.


Sambamba na hilo, marehemu alipata pia mivunjiko katika maeneo mbalimbali ya mwili wake ikiwemo miguu, mikono na mbavu.

No comments: