Thursday, January 18, 2018

SERIKALI YASITISHA UUZAJI WA MALI ZA CHAMA CHA USHIRIKA KILIMANJARO WABADHIRIFU KUCHUKULIWA HATUA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Na Mwandishi wetu,             
Tarime.

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira kusitisha uuzwaji wa mali za Chama cha Ushirika cha Kilimanjaro (KNCU).

Majaliwa alitoa agizo hilo jana wakati alipokuwa akihutubia wananchi katika mkutano wa hadhara, uliofanyika kwenye uwanja wa Serengeti Wilayani Tarime Mkoani hapa.

Hatua hiyo imekuja baada ya KNCU kutangaza kuuza shamba lake kwa ajili ya kuiwezesha benki yake ya KCBL kutimiza sharti la mtaji la Benki Kuu ya Tanzania (BOT).

Wednesday, January 17, 2018

JUHUDI LITUMBANDYOSI MBINGA KUANZISHA DUKA LA PEMBEJEO ZA KILIMO CHA KOROSHO

Baadhi ya wanachama wa kikundi cha Juhudi, kilichopo katika kijiji cha Litumbandyosi kata ya Litumbandyosi wakiwa kwenye kitalu cha miche bora ya mikorosho ambayo Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga, kwa kushirikiana na wanakikundi hao wamezalisha miche hiyo kwa ajili ya kuwagawia bure wakulima wa korosho katika kata hiyo ili waweze kuipanda kwenye mashamba yao katika msimu wa mwaka huu.


Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

WANACHAMA wa kikundi cha Juhudi waliopo katika kijiji cha Litumbandyosi kata ya Litumbandyosi Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma, ambao wanajishughulisha na kilimo cha zao la korosho wanatarajia kuanzisha duka la pembejeo la zao hilo ili waweze kupata pembejeo kwa urahisi.

Mhasibu wa kikundi hicho, Athanas Nyimbo aliwaeleza Waandishi wa habari kuwa kuanzisha kwa duka hilo wanatarajia kuanza na mtaji wa shilingi milioni mbili, fedha ambazo watapewa na Serikali kutokana na mgawo wa asilimia 30 baada ya kazi waliyofanya ya uzalishaji wa miche bora ya korosho ambayo itaanza kusambazwa kwa wakulima wa kijiji hicho.

Alisema kuwa kuanzishwa kwa duka hilo itakuwa ni msaada mkubwa kwao katika kijiji hicho na maeneo mengine ya jirani na kata ya Litumbandyosi, kwani hivi sasa wamekuwa wakilazimika kufuata huduma ya pembejeo za korosho umbali mrefu Wilayani Tunduru.

HALMASHAURI MJI WA MBINGA WATAKIWA KUPANDA MITI RAFIKI YA MAJI



Na Kassian Nyandindi,    
Mbinga.

WANANCHI wanaoishi katika Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani Ruvuma, wametakiwa kuendelea kupanda miti rafiki ya maji kwa wingi hasa kipindi hiki ambacho ni cha mvua za masika katika maeneo yenye vyanzo vya maji, ili kuweza kuondokana na tatizo la upungufu wa maji katika kipindi cha kiangazi.

Mwito huo umetolewa jana na Meneja wa Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira (MBIUWASA) katika Mji huo, Patrick Ndunguru wakati wa zoezi ambalo mamlaka hiyo inaendelea nalo la upandaji miti kuzunguka vyanzo mbalimbali vya maji ndani ya mji huo.

“Mkakati tulionao wa mamlaka hii ni kurudisha uoto wa asili katika vyanzo vya maji ambavyo vimeanza kupotea kutokana na baadhi ya wananchi kuendesha shughuli zao ikiwemo kilimo”, alisema.

TBA YAENDELEA NA UJENZI WA OFISI YA DC NA DED NYASA


Na Muhidin Amri,     
Nyasa.

WAKALA wa majengo Tanzania (TBA) kupitia kikosi chake cha ujenzi Mkoani Ruvuma, ameanza kazi ya ujenzi wa miradi minne ya majengo ya Serikali Wilayani Nyasa Mkoani humo ambayo miradi hiyo inagharimiwa na Ofisi ya Mkuu wa mkoa huo pamoja na Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo.

Meneja wa TBA Mkoani hapa, Mhandisi Edwin Mnunduma alifafanua kuwa miradi yote minne inatekelezwa kwa kutumia rasilimali zilizopo Serikalini kupitia wataalamu waliopo katika Ofisi ya Mkuu wa mkoa, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Ofisi ya Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya na Wakala wa majengo TBA.

Aidha alisema kuwa kikosi cha ujenzi huo kinajenga majengo yake kwa kutumia njia ya kubuni na kujenga kwa pamoja ili kuweza kutekeleza miradi ya Serikali kwa gharama nafuu.

Tuesday, January 16, 2018

YANGA YALAMBA DILI LA BILIONI MBILI



MABINGWA watetezi wa ligi kuu Tanzania Bara Yanga, leo wamesaini mkataba wa miaka mitatu na kampuni ya utengenezaji wa vifaa vya michezo, Macron wenye thamani ya shilingi bilioni mbili.

Katika mkataba huo uliosainiwa kwenye makao makuu ya klabu hiyo, Yanga itatoa haki zote za utengenezaji na usambazaji wa jezi zao huku pia nembo ya kampuni ya Macron, itaanza kuonekana kwenye jezi za Yanga SC.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Yanga, Charles Mkwasa amewaonya wote wanaouza jezi za klabu hiyo bila kuwepo kwa makubaliano watawachukulia hatua za kisheria kwa sababu sasa yupo mwenye haki ya kufanya hivyo. 

WANACHAMA BIMA YA AFYA WALALAMIKIA KUBAGULIWA



Na Mwandishi wetu,

BAADHI ya Wananchi ambao wamejiunga na mfuko wa Bima ya afya katika Halmashauri ya Busokelo Wilayani Rungwe Mkoa wa Mbeya wamelalamikia wauguzi kwenye vituo vya afya katika halmashauri hiyo, kuwabagua wagojwa wanaokwenda kutibiwa wakiwa na kadi za bima ya afya na kutoa kipaumbele kwa wagonjwa wanaolipa fedha taslimu hali ambayo wamedai kuwa inakwamisha jitihada za Serikali kuhamasisha wananchi kujiunga na bima za fya nchini.

Wananchi hao wametoa malalamiko yao mbele ya Mbunge wa jimbo la Busokelo, Atupele Fred Mwakibete wakati walipokuwa kwenye mkutano wa hadhara baada ya Mbunge huyo kufika katika kijiji cha Matamba kwa lengo la kukagua ujenzi wa zahanati ya kijiji hicho.

Akizungumza na wananchi hao, Mwakibete ameahidi kuyafanyia kazi malalamiko hayo huku akiwahimiza wananchi hao kuungana pamoja kukamilisha ujenzi wa jengo la kisasa la zahanati hiyo ambalo kutokana na ubora wake linaweza kubadilishwa na kuwa kituo cha afya.

CHIKAMBO AWAPA SOMO WANAWAKE RUVUMA


Na Muhidin Amri,         
Songea.

MBUNGE wa Viti maalum Mkoa wa Ruvuma, Sikuzan Chikambo amewataka wanawake wa mkoa huo kujituma na kufanya kazi kwa bidii ili waweze kujiletea maendeleo katika familia zao na kuweza kuondokana na umaskini.

Aidha Chikambo amewakumbusha wanawake hao kutumia fedha wanazopata kuanzisha vikundi vya ujasiriamali na kutumia kwa ajili ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa nyumba bora za kuishi na kupeleka watoto wao shule.

Mbunge huyo alitoa wito huo mwishoni mwa wiki wakati akizungumza na wanachama wa Jumuiya  ya Wanawake ya Chama cha Mapinduzi (UWT) Wilaya ya Songea  Mkoani hapa na kusisitiza kuwa wanawake hao wanao mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi.

DED MADABA AWAKARIBISHA WAWEKEZAJI KWENDA KUWEKEZA MADABA


Na Muhidin Amri,           
Madaba.

MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Madaba Mkoani Ruvuma, Shafi Mpenda amewataka wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kwenda kuwekeza katika maeneo mbalimbali Wilayani humo, kufuatia Halmashauri hiyo kutajwa kuwa miongoni mwa maeneo yenye fursa nyingi zinazofaa kwa shughuli za uwekezaji hapa nchini.

Mpenda alitoa wito huo juzi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na fursa  rafiki zilizopo huko ambazo bado hazijafanyiwa kazi licha ya Wilaya ya Madaba kutajwa kuwa ni sehemu nzuri kwa shughuli za uwekezaji.

Alisema kuwa Halmashauri hiyo bado kuna rasilimali nyingi ikiwemo ardhi nzuri yenye rutuba inayofaa kwa kilimo cha mazao mbalimbali kama vile kahawa, chai, korosho, mahindi tangawizi pamoja na uwepo wa mto Ruhuji wenye samaki wengi wazuri ambao hawapatikani sehemu yoyote hapa nchini na misitu mikubwa yenye wanyama kwa ajili ya shughuli za utalii na uwindaji.

KAMPUNI YA CHINA YASHINDA ZABUNI UJENZI BARABARA MANISPAA SONGEA KIWANGO CHA LAMI NZITO

Barabara za Manispaa ya Songea ambazo zinaendelea kujengwa.


Na Albano Midelo,        
Songea.

HATIMAYE Kampuni ya kimataifa ya China, inayofahamika kwa jina la China Sichuan International Co-operation imeshinda Zabuni ya kuendelea na ujenzi wa barabara za Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma kwa kiwango cha lami nzito.

Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Tina Sekambo alisema kuwa Kampuni hiyo inatarajia kuanza kazi hiyo mara baada ya kusaini mkataba baina ya Kampuni na Halmashauri ya Manispaa ya Songea.

Halmashauri hiyo ilivunja  Mkataba wa ujenzi wa lami nzito yenye urefu wa kilometa 8.6 kati yake na Kampuni ya Lukolo yenye makao makuu yake Jijini Dar es salaam, baada ya Kampuni hiyo kukiuka masharti ya mkataba wa miaka miwili  uliomalizika Juni 30 mwaka 2017.

Sunday, January 14, 2018

DOKTA NDUMBARO ANYAKUA JIMBO LA SONGEA MJINI

Na Kassian Nyandindi,     
Songea.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma kimeendelea kudhihirisha kukubalika kwake  na wananchi wa Wilaya hiyo, baada ya mgombea wake wa nafasi ya ubunge wa jimbo la Songea mjini Dokta Damas Ndumbaro, kupata ushindi wa kishindo katika kinyang’anyiro hicho.

Dokta Ndumbaro ambaye pia ni mwanasheria maarufu hapa nchini alipata kura 45,762 akifuatiwa na mgombe wa Chama cha CUF aliyepata kura 608, TADEA kura 471, Demokrasia makini kura 22, CCK 59, TLP 53, NRA 20, AFP 374, UDP 56 na Chama cha UPDP kimeambulia kura 30.

Kadhalika katika uchaguzi huo wananchi wengi hawakujitokeza kupiga kura, licha ya vituo vya kupigia kura kufunguliwa mapema majira ya saa moja kamili asubuhi lakini zoezi hilo lilifanyika kwa  kusua sua.

MADUKA 48 YA DAWA MUHIMU SONGEA YAFUNGWA

Mji wa Songea.
Na Albano Midelo,   
Songea.

MAMLAKA ya Udhibiti wa Chakula na Dawa (TFDA) chini ya idara ya afya na ustawi wa jamii katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, imeyafungia maduka ya dawa muhimu 48 kutokana na kushindwa kukidhi vigezo vya uendeshaji wa maduka hayo kisheria.

Mganga Mkuu wa Manispaa ya Songea, Dokta Mameritha Basike alisema kuwa idara ya afya imefanyakazi ya utambuzi wa maduka ya dawa muhimu ili kubaini iwapo maduka hayo, yanakidhi vigezo kulingana na mwongozo wa uendeshaji wa maduka ya dawa muhimu nchini.

Alisema kuwa kati ya maduka hayo yaliyofungiwa, maduka sita yamegundulika yanaendeshwa bila kibali na maduka 12 hayafanyi kazi kwa zaidi ya mwaka mmoja licha ya kuwa na vibali vya kuendesha katika kuuza dawa muhimu.

WAKULIMA WA KOROSHO MTWARA WALIPWA MILIONI 800

Na Mwandishi wetu,

DENI la zaidi ya shilingi milioni 800 ambalo lilikuwa likidaiwa na wakulima wa Korosho kwa msimu wa mwaka 2016/2017 kwa vyama vya ushirika (AMCOS) Mkoa wa Mtwara hatimaye limelipwa.

Mwenyekiti wa bodi ya chama kikuu cha ushirika cha Masasi, Mtwara Cooperative Union (MAMCU) Joseph Kidando alisema kuwa tayari kiasi hicho cha fedha kimeingizwa katika akaunti za vyama vya msingi kwa ajili ya  kugawanywa kwa wakulima.

Aidha Mwenyekiti huyo alifafanua kuwa wamelazimika kulipa deni hilo kutokana na wao kuwa walezi wa AMCOS na wakulima kwa ujumla na ametaja sababu za kuchelewesha kulipwa kwa fedha hizo ni upotevu wa fedha uliosababishwa na makosa ya viongozi wa AMCOS husika.

Saturday, January 13, 2018

RAIS MAGUFULI AWATAKA WATANZANIA KUPUUZA KUHUSU MJADALA WA KUONGEZA MIAKA YA URAIS

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 13 Januari, 2018 amekutana na kufanya mazungumzo na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM, Itikadi na Uenezi Ndg. Humphrey Polepole, Ikulu Jijini Dar es Salaam.

Baada ya mazungumzo hayo Ndg. Polepole amesema Mhe. Dkt. Magufuli amemuelekeza kuwajulisha wanachama wa CCM na umma wa Watanzania kuwa anasikitishwa na hafurahishwi na mjadala unaoendelea juu ya kuongezwa kwa kipindi cha Urais kutoka miaka 5 iliyowekwa kwa mujibu wa katiba, hadi miaka 7.

Ndg. Polepole amesema Mhe. Dkt. Magufuli amewataka wanachama wa CCM na umma wa Watanzania kwa ujumla kupuuza mjadala huo kwa kuwa haujawahi kujadiliwa katika kikao chochote cha chama, na ni kinyume na katiba ya CCM na katiba ya nchi.

SERIKALI ISAIDIE TaCRI KUBORESHA ZAO LA KAHAWA

Msafara wa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ulipowasili Januari 5 mwaka huu katika eneo la Kituo cha utafiti wa zao la kahawa (TaCRI) Ugano Wilayani Mbinga.

Mbele upande wa kulia Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwa ameongozana na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa zao la Kahawa (TaCRI) nchini upande wa kushoto, Deusdedit Kilambo katika eneo la Ugano Mbinga ambako miche ya kahawa aina ya vikonyo huzalishwa. 

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya utafiti wa zao la kahawa (TaCRI) hapa nchini, Deusdedit Kilambo kwa pamoja wakiwa wameshika mti wa kahawa wakati Mkurugenzi huyo wa TaCRI akitoa maelezo kwa Waziri Mkuu namna wanavyozalisha na kuboresha zao hilo. 
Na Kassian Nyandindi,    
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa Serikali itaona namna bora ya kusaidia Taasisi ya Utafiti wa zao la Kahawa (TaCRI) katika kituo chake cha Ugano kilichopo Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma, ili taasisi hiyo iweze kuzalisha miche kwa wingi na kuisambaza kwa wakulima wake.

Aidha licha ya Serikali kuzipatia halmashauri fedha nyingi hasa kwa sekta ya kilimo, lakini wameshindwa kuzalisha miche kama TACRI inavyofanya huku Watendaji wa idara ya kilimo wametakiwa kubadilika kwenda na kasi ya Serikali ya awamu ya tano.

Hivi karibuni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa alisema hayo Januari 5 mwaka huu wakati alipokuwa kwenye ziara yake Wilayani hapa na alipotembelea kituo hicho cha utafiti wa zao la kahawa.

RC RUVUMA AWATAKA WATUMISHI WA UMMA KUTEKELEZA WAJIBU WAO

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme.
Na Kassian Nyandindi,      
Songea.

MKUU wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme amewataka watumishi wa umma kutekeleza wajibu wao kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu ili kwa pamoja waweze kufanikisha malengo ya Serikali ya awamu ya tano ya kuwaondolea kero wananchi wa mkoa huo.

Mndeme alitoa agizo hilo hivi karibuni wakati alipokuwa akizungumza na baadhi ya watumishi, wakuu wa idara, wakurugenzi wa halmashauri  za wilaya, mji na  wakuu wa wilaya za mkoa huo katika kikao cha bodi ya barabara kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Manispaa ya Songea Mkoani hapa.

Alisema kuwa Serikali ya awamu ya tano kwa nia njema imeanzisha Wakala wa barabara mjini na vijijini (TARURA) ambaye amekwisha anza kazi na kuwezesha halmashauri kujikita katika usimamizi na utekelezaji wa shughuli nyingine za maendeleo.

SERIKALI KUTUMIA MILIONI 500 UJENZI WA OFISI HALMASHAURI YA MADABA

Na Muhidin Amri,      
Madaba.

SERIKALI imetumia jumla ya shilingi milioni 500 kati ya shilingi bilioni 1.2 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la Ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma.

Kaimu Afisa mipango wa Halmashauri hiyo, Mwandishi Nchimbi alisema hayo jana, alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu katika eneo ambalo ofisi hizo zinajengwa katika kitongoji cha Kifagulo kata ya Lituta Wilayani humo.

Nchimbi alisema kuwa jengo hilo linajengwa na Wakala wa majengo (TBA) mkoa wa Ruvuma na mara litakapokamilika litasaidia kwa kiasi kikubwa watumishi wa idara mbalimbali kuwa na ofisi zao kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu yao ya kazi za kila siku tofauti na ilivyokuwa hivi sasa ambapo wanalazimika kutumia jengo moja dogo la idara ya kilimo.

Friday, January 12, 2018

HALMASHAURI WILAYA YA MBINGA KUENDELEA KUBORESHA SEKTA YA ELIMU AFYA

Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri Wilaya ya Mbinga, Gombo Samandito akiwa hivi karibuni katika mkutano na baadhi ya wananchi wa kata ya Litembo kuhamasisha shughuli mbalimbali za kimaendeleo.


Na Muhidin Amri,      
Mbinga.

HALMASHAURI ya Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma, imepanga kukamilisha kazi ya ujenzi wa vyumba vya madarasa  116 katika shule za msingi na vyumba 19 kwa upande wa sekondari, katika kipindi cha mwaka 2017/2018.

Aidha halmashauri hiyo  imejenga nyumba 29 za walimu wa shule za msingi na nyumba 12 kwa upande wa sekondari hatua inayotajwa kuwa itaweza kumaliza tatizo la upungufu wa nyumba za kuishi walimu katika halmashauri hiyo.

Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya Wilaya hiyo, Gombo Samandito alisema pia halmashauri hiyo imekamilisha ujenzi wa matundu ya vyoo 58 katika shule za msingi na matundu manne kwa shule za sekondari.

MKOA WA RUVUMA WAFANIKIWA KUWA NA CHAKULA CHA ZIADA AINA YA WANGA TANI 893,887

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme.
Na Kassian Nyandindi,        
Songea.

MKOA wa Ruvuma  umefanikiwa kuvuna chakula aina ya wanga tani 1,232,776 katika msimu wa kilimo wa 2016/2017 wakati  mahitaji halisi ya wakazi wa mkoa huo ni tani 338,889 hivyo kuwa na ziada ya chakula tani 893,887.

Mkuu wa mkoa huo, Christine Mndeme alisema hayo hivi karibuni wakati wa kikao cha  Kamati ya ushauri cha mkoa (RCC) kilichofanyika mjini Songea.

Aidha  alisema kuwa ununuzi wa mahindi katika msimu wa 2016/2017 mkoa wa Ruvuma umepangiwa kununua tani 11,483 za mahindi toka kwa wakulima kwa bei ya shilingi 500 kwa kilo kupitia kwa Wakala wa  Taifa wa Hifadhi ya chakula (NFRA).

MAGINGO MKONGOTEMA MADABA WAFANIKIWA KUJENGA ZAHANATI

Na Muhidin Amri,    
Madaba.

WANANCHI wa vijiji viwili vya Magingo na Mkongotema Halmashauri ya Wilaya ya Madaba Mkoani Ruvuma, kwa kushirikiana na Serikali wamefanikiwa kujenga zahanati ili waweze kupata huduma bora  za matibabu karibu na makazi yao.

Aidha imeelezwa kwamba ujenzi wa zahanati hiyo utasaidia kwa kiasi kikubwa huduma za watoto na akina mama wajawazito kuweza kujifungua sehemu salama na kupata huduma nyingine za uzazi katika mazingira salama badala ya kutembea umbali mrefu kufuata huduma hizo.

Afisa Mtendaji wa kijiji cha Magingo, Kwinbert Mhoro alisema hayo juzi alipokuwa akizungumzia kuhusiana na ujenzi wa zahanati hiyo mbele ya waandishi wa habari.

UKOSEFU WA FEDHA UNAKWAMISHA UTEKELEZAJI MIRADI YA MAJI MADABA

Na Muhidin Amri,       
Madaba.

MBUNGE wa jimbo la Madaba Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma, Joseph Mhagama amesema kwamba ukosefu wa fedha za kutosha na  baadhi ya wananchi kutopenda kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa miradi ya maendeleo, ndiyo kikwazo kikubwa katika utekelezaji wa miradi ya maji katika baadhi ya vijiji ndani ya jimbo hilo.

Aidha alisema kuwa yeye akiwa ndiye Mbunge wa kwanza wa jimbo hilo kipaumbele chake cha kwanza tangu alipoingia madarakani miaka miwili iliyopita ni suala la upatikanji wa maji safi na salama ambapo alisema atahakikisha kwamba anatafuta fedha kwa ajili ya kumaliza kero hiyo ya maji.

Hayo yalisemwa juzi na Mbunge Mhagama wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu Ofisini kwake huku akisisitiza kuwa bila ushiriki wa wananchi ipasavyo katika ujenzi wa miradi hiyo itakuwa ni ndoto kwa Serikali kuweza kufikia malengo yake.

Thursday, January 11, 2018

WATUHUMIWA WANAODAIWA KUHUJUMU CHAMA KIKUU CHA USHIRIKA WA KAHAWA MBIFACU MBINGA WAPANDISHWA KIZIMBANI

Wa kwanza mbele upande wa kulia aliyevaa sweta rangi nyeusi ni, Frank Ndunguru ambaye ni Mhasibu wa Chama kikuu cha ushirika wa kahawa wilaya ya Mbinga (MBIFACU) Mkoani Ruvuma, leo akifikishwa katika Mahakama ya wilaya ya Mbinga mkoani humo kwa tuhuma ya wizi wa fedha za chama hicho shilingi milioni 6.
Aliyekuwa Meneja wa Chama kikuu cha ushirika wa kahawa wilaya ya Mbinga (MBIFACU) Damian Luena akipandishwa kwenye Karandinga la polisi leo katika Mahakama ya Hakimu mkazi wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma kwenda Mahabusu, baada ya kutuhumiwa kukisababishia chama hicho hasara ya shilingi milioni 18.7. 
Na Kassian Nyandindi, 


Mbinga.

HATIMAYE agizo la Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa la kutaka kukamatwa na kufikishwa Mahakamani Watuhumiwa wote waliohusika kuhujumu Chama Kikuu cha Ushirika wa Kahawa Mbinga (MBIFACU) Mkoani Ruvuma, limeanza kutekelezwa.

Mpaka sasa Watuhumiwa wawili wamekamatwa na kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu mkazi Wilaya ya Mbinga Mkoani hapa kwa tuhuma ya wizi wa fedha za chama hicho pamoja na uhujumu uchumi.

Kwa mujibu wa Mwendesha mashtaka wa Polisi, Inspekta Seif Kilugwe alidai mbele ya Hakimu mkazi mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya hiyo, Magdalena Ntandu kuwa mshtakiwa wa kwanza Frank Ndunguru ambaye ni Mhasibu wa MBIFACU, chini ya kifungu namba 258 na 265 kanuni ya adhabu sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 anatuhumiwa kutenda kosa la wizi wa fedha kiasi cha shilingi milioni 6 za chama hicho.

DED MADABA APIGA MARUFUKU UCHOMAJI MOTO KATIKA MASHAMBA

Na Muhidin Amri,      
Madaba.

MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Madaba Mkoani Ruvuma, Shafi Mpenda amepiga marufuku tabia ambayo inafanywa na baadhi ya wakulima wa Wilaya hiyo, wakati wa kuandaa mashamba yao kwa kuchoma moto kwani husababisha misitu mingi ya asili huteketea kwa moto.

Aliwataka wakulima katika jimbo la Madaba kuandaa mashamba kwa njia ya kisasa bila kuathiri mazingira pamoja na viumbe hai wengine hatua ambayo itawezesha kutunza na kuhifadhi mazingira kwa faida ya sasa na vizazi vijavyo.

Mpenda alisema hayo juzi wakati akiongoza operesheni ya kuwasaka watu wanaojihusisha na ukataji miti ovyo kwa ajili ya shughuli za mkaa, katika kijiji cha Mbangamawe ambacho kimeathirika kutokana na shughuli za uchomaji wa mkaa.

MAJALIWA: WIZARA INAYOHUSIKA NA MASUALA YA UTALII INAOWAJIBU WA KUANZISHA MAMLAKA ZA FUKWE KWENYE BAHARI NA MAZIWA

Baadhi ya Wavuvi wakiwa katika ziwa Nyasa wilaya ya Nyasa Mkoani Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,      
Nyasa.

SERIKALI imeagiza kuwa, Wizara inayohusika na masuala ya utalii inaowajibu wa kuanzisha mamlaka za fukwe kwenye bahari na maziwa, ili kuweza kuimarisha shughuli za utalii hapa nchini.

Agizo hilo lilitolewa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambapo alisema kuwa kuanzishwa kwa mamlaka hiyo kutasaidia kuboresha utalii maeneo ya fukwe na kuhamasisha watu mbalimbali waweze kufanya uwekezaji kwa kujenga hoteli kubwa kwenye fukwe hizo sambamba na kuwafundisha wananchi namna ya kuwapokea watalii kwa ukarimu ili waweze kurudi kutalii siku za mbele.

Majaliwa alisema hayo wakati wa uzinduzi wa Tamasha la utalii lililofanyika hivi karibuni ufukweni mwa ziwa Nyasa mjini Mbamba bay ambalo lilibeba ujumbe wenye kauli mbiu isemayo, Tangaza utalii na fursa za uwekezaji Nyasa kuelekea uchumi wa viwanda.

WATANZANIA WATAKIWA KUTEMBEA KIFUA MBELE

Na Muhidin Amri,     
Songea.

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa, amewataka Watanzania kutembea kifua mbele wakati huu ambao Serikali ya awamu ya tano inaendelea kumaliza kero, kutekeleza ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo na kuimarisha uchumi.

Majaliwa alitoa kauli hiyo hivi karibuni wakati akizungumza na  wakazi wa mtaa wa Unangwa kata ya Seed Farm katika Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, alipokuwa akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa njia kuu ya kusafirisha umeme wa gridi ya Taifa kutoka Njombe hadi Songea mkoani Ruvuma.

Alisema kuwa Serikali imetoa fedha nyingi kwa ajili ya mradi huo ambao tayari umeshaanza  kutekelezwa katika mkoa wa Njombe na sasa umefika  Ruvuma, kwa hiyo wananchi wajiandae kutumia fursa ya umeme wa uhakika ikiwemo kuanzisha viwanda vidogo na vikubwa ili  kukuza  kipato na uchumi wa nchi.

WAPONGEZA JITIHADA ZA RAIS AWAMU YA NNE KUIGAWA WILAYA YA MBINGA

Na Muhidin Amri,     
Nyasa.

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amempongeza Rais wa awamu ya nne, Dokta Jakaya Kikwete kwa uamuzi wa kuigawa Wilaya ya Mbinga  iliyopo Mkoani Ruvuma na kuzaliwa Wilaya ya Nyasa Mkoani humo kwa lengo la kusogeza huduma mbalimbali za kijamii karibu na wananchi.

Majaliwa alitoa pongezi hizo hivi karibuni alipokuwa akizungumza na mamia ya wananchi wa Wilaya Nyasa, wakati akifunga Tamasha  la utalii katika viwanja vya Bandari ya Mbamba bay wilayani hapa.

Waziri Mkuu amewataka wananchi wa Nyasa kuwa na tabia ya kuwaenzi viongozi na watumishi wanaofanya vizuri katika  kuwaletea maendeleo, ili kuepusha kuwakatisha tamaa jambo linaloweza kurudisha nyuma dhamira ya kimaendeleo waliyonayo viongozi hao.

Monday, January 8, 2018

OFISA KILIMO HALMASHAURI WILAYA YA SONGEA AONJA JOTO YA JIWE WAZIRI MKUU ACHUKIZWA NA UTENDAJI WAKE WA KAZI

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikabidhi miche ya kahawa kwa Mkulima wa kijiji cha Lipokela Halmashauri ya Wilaya ya Songea, Joseph Ngatunga inayozalishwa katika shamba la Mwekezaji mkubwa wa zao hilo Kampuni ya AVIV Tanzania Limited, hata hivyo Waziri Mkuu alichukizwa na idara ya kilimo Wilayani humo kwa kushindwa kuhamasisha wananchi kwenda kuchukua miche hiyo inayogawiwa bure na Kampuni hiyo ili waweze kupanda katika mashamba yao.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikabidhi miche ya kahawa kwa Mkulima wa kijiji cha Lipokela Halmashauri ya Wilaya ya Songea, Joseph Ngatunga inayozalishwa katika shamba la Mwekezaji mkubwa wa zao hilo Kampuni ya AVIV Tanzania Limited, hata hivyo Waziri Mkuu alichukizwa na idara ya kilimo Wilayani humo kwa kushindwa kuhamasisha wananchi kwenda kuchukua miche hiyo inayogawiwa bure na Kampuni hiyo ili waweze kupanda katika mashamba yao.
Na Kassian Nyandindi,     
Songea.

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amemjia juu Ofisa kilimo wa Halmashauri ya Wilaya ya Songea vijijini Mkoani Ruvuma, Helen Shemzigwa kwa kutosimamia ipasavyo kilimo cha zao la kahawa huku akimtaka Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Saimon Bulenganija ahakikishe kwamba anawasimamia maofisa hao kwa umakini mkubwa katika Wilaya hiyo ili waweze kutekeleza majukumu yao ya kazi kwa mujibu wa taratibu husika.

Akizungumza na wananchi na wafanyakazi wa Kampuni ya Aviv ambayo imewekeza katika uzalishaji wa zao la kahawa katika kijiji cha Lipokela wilayani humo, mara baada ya kutembelea shamba hilo alisema jukumu la maofisa kilimo ni kuhakikisha kwamba wanakwenda kwa wakulima vijijini na kuwapa elimu ya namna bora ya uzalishaji wa mazao mbalimbali na sio muda mwingi kurundikana maofisini.

“Halmashauri ya Songea vijijini mmesema ina watumishi saba ambao wanakaa ofisini naomba kuanzia sasa Mkurugenzi uhakikishe ofisini wanaobaki ni watatu tu na wengine waende kwa wakulima", alisema.

OFISI YA WAZIRI MKUU KUCHUNGUZA UJENZI MRADI WA MAJI MKAKO MBINGA

Na Mwandishi wetu,       
Mbinga.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema kuwa Ofisi yake itatuma tume ya kuja kuchunguza malalamiko ya ujenzi wa mradi wa maji wa wananchi uliopo katika kitongoji cha Mnazi mmoja, kijiji cha Mkako kata ya Mkako Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Aidha alisema kuwa mradi huo ulianza kujengwa Machi 28 mwaka 2014 chini ya ufadhili wa benki ya dunia, kwa gharama ya shilingi milioni 718,896,533 lakini ujenzi wake umekuwa ni wa chini ya kiwango na sehemu kubwa ya fedha za mradi huo zimekwisha tumika.

Waziri Mkuu, Majaliwa alibainisha kuwa aliyekuwa Mhandisi wa idara ya maji wa halmashauri ya Wilaya hiyo, Vivian Mndolwa alichukuliwa hatua akituhumiwa kushiriki na wenzake kuhujumu mradi huo, lakini ameshangazwa hakuna kitu kinachoendelea na badala yake amehamishwa kwenda mkoa mwingine.

SERIKALI YATUPILIA MBALI PENDEKEZO LA MADIWANI MBINGA UJENZI WA OFISI NDENGU

Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

SERIKALI hapa nchini imefuta mapendekezo ya ujenzi wa Ofisi za makao makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma, katika eneo la Ndengu lililopo kata ya Nyoni Wilayani humo ambayo yalipitishwa hivi karibuni na Baraza la Madiwani wa halmashauri hiyo.

Mapendekezo hayo yalifutwa juzi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa wakati alipokuwa akizungumza na Watumishi na Madiwani wa halmashauri ya Wilaya hiyo katika ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa.

Waziri Mkuu, Majaliwa alisema kuwa eneo hilo ambalo wanataka kujenga ofisi hizo, limetengwa na kuhifadhiwa kwa miaka mingi kwa ajili ya kutunza mazingira na vyanzo vya maji vilivyopo huko ambavyo ndiyo tegemeo kubwa kwa ajili ya kulisha wakazi wa mji wa Mbinga.

Sunday, January 7, 2018

WAKAZI MJI WA MBINGA WAMCHONGEA MKURUGENZI MTENDAJI ROBERT MAGENI KWA WAZIRI MKUU

Hili ni moja kati ya ghuba ambalo limejengwa katika mtaa wa Msikitini Mbinga mjini taka zikiwa zimetelekezwa kwa siku nyingi bila kuzolewa kama mpiga picha wetu alipopita hivi karibuni na kukuta taka hizo zikiwa zimezagaa.
Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida baadhi ya Wakazi wa Mji wa Mbinga Mkoani Ruvuma wamemchongea kwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya mji huo, Robert Kadaso Mageni na Watendaji wake ambao wamepewa dhamana ya kusimamia masuala ya usafi ndani ya mji huo kwamba hawawajibiki ipasavyo katika sekta ya usafi.

Tukio hilo la aina yake lilitokea juzi katika uwanja wa michezo uliopo Mbinga mjini, wakati Waziri huyo alipokuwa akisikiliza kero mbalimbali za wananchi.

Wakazi hao kwa nyakati tofauti walieleza kuwa kumekuwa na uzembe mkubwa wa kutosimamia masuala ya usafi kikamilifu katika mji huo, ikiwemo uzoaji taka kwenye maghuba yaliyopo mjini hapa ambapo wakati mwingine taka zimekuwa zikikaa kwa siku nyingi bila kuzolewa jambo ambalo ni hatari kwa afya zao.

WIZI WA MAMILIONI YA FEDHA ZA MSITU WA MBAMBI MBINGA KUCHUNGUZWA NA OFISI YA WAZIRI MKUU

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Na Kassian Nyandindi,         
Mbinga.

SAKATA la wizi na matumizi mabaya ya mamilioni ya fedha za mradi wa uvunaji wa msitu wa Mbambi katika Halmashauri ya mji wa Mbinga Mkoani Ruvuma, limechukua sura mpya baada ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa kueleza kuwa ataunda tume ambayo itakuja kuchunguza jambo hilo na wahusika watakaopatikana waweze kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

Majaliwa alisema hayo juzi wakati alipokuwa akizungumza katika mkutano wa hadhara na wananchi wa Mbinga mjini, huku akieleza kuwa tume hiyo wakati wowote kuanzia sasa itawasili katika halmashauri hiyo kwa ajili ya kuanza kufanya kazi hiyo.

"Tulipokea malalamiko yenu ya idadi ya miti na tathimini mliyoifanya katika msitu ule, lakini hata mapato ya fedha zilizotokana na msitu huo hayaeleweki yaliko,

WAKULIMA WA KAHAWA MBINGA KUSAJILIWA KWENYE MFUMO UTOAJI TAARIFA ZA MASOKO

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa akiwa katika eneo la Kiwanda cha kukoboa kahawa Mbinga wakati alipotembelea juzi kwa lengo kujionea maendeleo ya kiwanda hicho.
Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameitaka Bodi ya Kahawa Tanzania (TCB) kuwawezesha wakulima wanaozalisha zao la kahawa Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma, wajisajili kwenye mfumo wa utoaji wa taarifa za masoko ya dunia ili mauzo ya kahawa yao yaendane na soko hilo.

Agizo hilo la Waziri Mkuu, Majaliwa alilitoa juzi wakati alipokuwa ametembelea na kukagua Kampuni ya Kiwanda cha Kukoboa Kahawa Mbinga (MCCCO) iliyopo Wilayani humo.

Pia alisema kuwa ili kuwawezesha wakulima hao waweze kuuza kahawa yao moja kwa moja mnadani bila kupitia kwa mtu binafsi ni lazima waingizwe kwenye mfumo huo ili watambue soko la dunia lipoje.

SERIKALI KUKIFANYA KITUO CHA LILAMBO SONGEA KUWA KITUO KIKUU CHA UNUNUZI MAZAO

Na Muhidin Amri,      
Songea.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema, Serikali itaangalia uwezekano wa kukifanya kituo cha kuongeza thamani ya mazao kilichopo katika eneo la Lilambo kata ya Ruhuwiko Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, kuwa kituo kikuu cha ununuzi na uuzaji wa mazao.

Majaliwa alisema hayo juzi wakati alipokuwa akizungumza na wananchi wa kijiji cha Lipokela kata ya Lipokela wilayani Songea, baada ya kukagua mradi mkubwa wa shamba la kahawa ambalo linamilikiwa na Kampuni ya AVIV Tanzania Limited.

Alisema kuwa Mkoa huo ni kati ya mikoa saba hapa nchini ambayo inaongoza kwa uzalishaji wa mazao mbalimbali na kwamba Serikali kuanzia msimu ujao itatekeleza hilo ili mazao yanayolimwa mkoani humo yaweze kupata soko na kuwaondolea umaskini wakulima.

Saturday, January 6, 2018

SERIKALI IMEFUTA KUTOLEWA KWA VIBALI KWA MAKAMPUNI BINAFSI KUNUNUA ZAO LA KAHAWA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza Madiwani na Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga katika ukumbi wa Jumba la maendeleo mjini hapa. 
Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa amefuta vibali kwa makampuni binafsi yanayonunua zao la kahawa hapa nchini na kuwataka viongozi husika kutekeleza agizo hilo bila kuchelewa.

Majaliwa alisisitiza kuwa kuanzia sasa biashara yote ya zao la kahawa itafanywa na vyama vya ushirika vilivyosajiliwa na kutambuliwa kisheria na sio vinginevyo.

"Tunataka turekebishe ushirika mkuu wa wakulima wa kahawa MBIFACU uliopo hapa wilayani Mbinga, ili uweze kuwasaidia wakulima hawa na hatimaye wajikwamue na umaskini", alisema.

SERIKALI KUWASHUKIA WALIOHUJUMU MALI ZA MBIFACU

Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

SERIKALI hapa nchini imetoa agizo kwamba, kwa wale wote viongozi ambao watabainika kwa namna moja au nyingine walishiriki kufanya ubadhirifu katika Chama Kikuu Cha Ushirika wa Kahawa (MBIFACU) kilichopo Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma, watachukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kufikishwa Mahakamani.

Aidha kufuatia agizo hilo askari kutoka Jeshi la Polisi Wilayani humo wamezingira Ofisi za MBIFACU zilizopo mjini hapa na kufunga makufuli ili ukaguzi wa mali za wanachama wa ushirika huo uweze kufanyika.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa alitoa agizo hilo jana wakati alipokuwa kwenye ziara yake ya kikazi wilayani hapa akihutubia wananchi wa Mbinga.

TIMU YA UKAGUZI YAUNDWA KUCHUNGUZA UJENZI KITUO CHA AFYA KALEMBO

Ngoma mbalimbali za asili zikitoa burudani wakati Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipowasili kwenye uwanja wa michezo Mbinga mjini.

Wananchi wakiwa wameshika mabango yenye ujumbe mbalimbali wa malalamiko ambapo baadaye Waziri Mkuu aliweza kuyatafutia ufumbuzi.
Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

KUFUATIA Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani Ruvuma kutotekeleza kwa wakati uliopangwa juu ya kukamilisha ujenzi wa Kituo cha afya Kalembo, kilichopo katika kata ya Kihungu ndani ya halmashauri hiyo Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa amesema kuwa tayari Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Seleman Jafo ameunda timu ya ukaguzi kwa ajili ya kwenda kuchunguza mwenendo mzima wa ujenzi wa kituo hicho.

"Ofisi yangu inazotaarifa za kutosha juu ya mwenendo wa kusuasua kwa ujenzi huu lengo tunataka tupate thamani ya matumizi ya fedha iliyotumika, nataka tumikieni wananchi hawa kwa weledi na uaminifu ili mwisho wa siku tuweze kufanya kazi yenye bora kwa manufaa ya umma", alisisitiza.

Waziri Mkuu Majaliwa alibainisha hayo jana wakati alipokuwa kwenye ziara yake ya kikazi ya kutembelea miradi mbalimbali ya maendeleo ya wananchi.

Thursday, January 4, 2018

HALMASHAURI MADABA YATUMIA MILIONI 6.2 KUJENGA MATUNDU YA VYOO

Na Mwandishi wetu, 
Madaba.

HALMASHAURI ya Wilaya ya Madaba Mkoani Ruvuma, imetoa shilingi milioni 6.2 kwa ajili ya ujenzi wa matundu ya vyoo katika shule ya Sekondari Madaba iliyopo wilayani humo, ili kuweza kuwanusuru wanafunzi wanaosoma kwenye shule hiyo waweze kuwa katika mazingira salama.

Aidha imeelezwa kuwa hatua hiyo inafuatia baada ya vyoo wanavyotumia hivi sasa kuwa chakavu na vile vinavyohatarisha maisha ya watoto hao.

Mkuu wa shule hiyo, Humari Mapunda alisema kuwa anaishukuru Serikali kwa uamuzi huo uliochukuliwa na kwamba kwa upande wa ujenzi wa vyoo kwa ajili ya wanafunzi wa kike umekwisha kamilika na mavundi wanaendelea kukamilisha kwa ajili ya wavulana.

WAZIRI MKUU KUANZA ZIARA YA KIKAZI LEO MKOANI RUVUMA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa upande wa kulia akipokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme katika uwanja wa ndege Songea akiwa katika siku yake ya kwanza kati ya siku tatu ya ziara yake ya kikazi mkoani humo.
Na Muhidin Amri,    
Songea.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameanza ziara yake ya siku tatu kuanzia leo Januari 4 hadi 9 Mkoani Ruvuma, ambapo katika ziara hiyo atatembelea Wilaya ya Songea, Mbinga na Nyasa zilizopo mkoani humo.

Mkuu wa mkoa  huo, Christine Mndeme alisema kuwa katika ziara hiyo Waziri Mkuu ataweka mawe ya msingi na kufungua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na ile iliyotekelezwa ndani ya wilaya hizo.

Kwa mujibu wa Mndeme alifafanua kuwa miradi hiyo ni ile ambayo inalenga kuharakisha maendeleo na kuboresha huduma za kijamii kwa wananchi katika maeneo atakayotembelea.

DC: KUENDELEA KUSHAMIRI UCHAFU MJI WA MBINGA KUNATOKANA NA UZEMBE WA MKURUGENZI MTENDAJI


Mkuu wa Wilaya ya Mbinga, Cosmas Nshenye akizungumza na Waandishi wa habari jana (Hawapo pichani) juu ya hali ya mji wa Mbinga kuwa mchafu ambapo alilalamikia Mkurugenzi na Watendaji wa mji huo kutowajibika ipasavyo.
Hili ni moja kati ya ghuba la uchafu lililopo katika Mji wa Mbinga katika mtaa wa Msikitini katikati ya makazi ya watu ambalo wakazi wa mji huo hulamimikia hali hiyo kwa kukaa kwa muda mrefu bila kuzolewa taka na kuleta kero katika jamii.















Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa kitendo cha Mji wa Mbinga Mkoani Ruvuma kuendelea kushamiri uchafu, kunatokana na uzembe unaofanywa na Mkurugenzi mtendaji wa mji huo, Robert Kadaso Mageni au Watendaji wake ambao wamepewa dhamana ya kusimamia na kutekeleza jambo hilo.


Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Cosmas Nshenye alisema hayo jana wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake akitolea ufafanuzi juu ya kutozolewa uchafu kwa wakati, kwenye maghuba ya kuhifadhia taka yaliyopo mjini hapa.


“Ninakiri suala la mji kuwa mchafu, uhamasishaji wa watu kuuweka mji katika hali ya usafi umekuwa mdogo hivyo wanapaswa kuendelea kutekeleza hili hatutaki kuona maghuba yana uchafu, kiutendaji sio sahihi kila leo unapewa maelekezo”, alisema Nshenye.

Wednesday, January 3, 2018

LHRC YAITAKA SERIKALI KUHESHIMU KATIBA

Na Mwandishi wetu,
Dar es Salaam. 

KITUO cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimeviomba vyombo vya kimataifa vinavyohusika na uangalizi wa haki za binadamu kuingilia kati suala la uhuru wa kujieleza nchini.

LHRC pia imetaka Serikali kuheshimu Katiba kwa kutoingilia uhuru wa kujieleza.

Kauli hiyo imetolewa leo siku moja baada ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuvitoza faini vituo vya televisheni vya ITV, Azam Two, Startv, Channel Ten na EATV kwa kukiuka kanuni ya maudhui ya mwaka 2005.

Tuesday, January 2, 2018

MKURUGENZI MTENDAJI HALMASHAURI MJI WA MBINGA ATUHUMIWA KUKWAMISHA UKAMILISHAJI UJENZI MRADI WA KITUO CHA AFYA KALEMBO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dokta John Pombe Magufuli.

Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

AGIZO la Serikali la kutaka kujengwa na kukarabatiwa kwa vituo 172 vya afya kote nchini na kuhakikisha kwamba kazi hiyo iwe imekamilika ifikapo Desemba 30 mwaka huu, hali hiyo imekuwa kinyume kwa Halmashauri ya Mji wa Mbinga mkoani Ruvuma ambapo mpaka sasa ujenzi wa Kituo cha afya Kalembo kilichopo katika kata ya Kihungu ndani ya halmashauri hiyo haujakamilika.

Hilo limebainika kufuatia malalamiko yaliyotolewa na Diwani wa kata hiyo, Dustan Ndunguru na wananchi wake wakieleza kuwa licha ya kituo hicho kupewa fedha zaidi ya shilingi milioni 500 lakini hali ya maendeleo ya ujenzi wake imekuwa ikifanyika kwa kusuasua.

Diwani huyo na wananchi wake wamemlalamikia Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Robert Kadaso Mageni wakimtuhumu kwamba ndiye aliyesababisha na kukwamisha kutokamilika kwa ujenzi wa kituo hicho kwa wakati uliopangwa kulingana na agizo lilitolewa na Serikali.

Monday, January 1, 2018

MAMIA WAJITOKEZA KUMUAGA BABA WA ASKOFU NZIGILWA



MAMIA ya waombolezaji wamejitokeza kuaga mwili wa Alfred Nzigilwa, ambaye ni baba mzazi wa Askofu Msaidizi wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Eusebius Nzigilwa katika ibada iliyofanyika Parokia ya Roho Mtakatifu Segerea.

Mzee Nzigilwa (87) alifariki dunia Desemba 29,2017 nyumbani kwake Tabata Chang'ombe jijini Dar es Salaam.

Imeelezwa alikuwa akipata matibabu mara kwa mara katika hospitali za Muhimbili, Madonna na Regency kutokana na maradhi ya tumbo na moyo kutanuka.

SERIKALI KUENDELEA KUTOA KIBANO KWA VIONGOZI WA UMMA



Na Mwandishi wetu,

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Ofisi zote za maadili zilizopo hapa nchini, zimeagizwa kuhakikisha kwamba viongozi hawafanyi biashara na Ofisi za umma.

George Mkuchika.
Agizo hilo limetolewa jana na Waziri wa nchi, ofisi ya Rais, (Utumishi na utawala bora, George Mkuchika wakati alipokuwa akikabidhi fomu ya tamko la rasilimali na madeni kwa viongozi wa utumishi wa umma katika ofisi za maadili Kanda ya kusini mkoani hapa.

Alisema Wizara yake imekuwa ikipokea taarifa kwamba wapo madiwani, wabunge na wakuu wa mashirika ya umma hufanya biashara na halmashauri zao, kitendo ambacho ni kinyume cha sheria.