Monday, March 24, 2014

KIGONSERA AFYA ZAO ZIPO HATARINI, WANANCHI WATISHIA KULALA BARABARANI KUZUIA MSAFARA WA RAIS


Hivi ndivyo ilivyo katika chanzo cha maji Kigonsera ambako maji yametegwa kwa ajili ya matumizi ya binadamu, hali ni mbaya hatua husika zinapaswa kuchukuliwa mapema.(Picha na Gwiji la matukio Ruvuma)










Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

AFYA za wakazi wa kijiji cha Kigonsera kata ya Kigonsera wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, zipo mashakani kutokana na maji wanayotumia kwa ajili ya kuendeshea maisha yao ya kila siku kuwa machafu na kutofaa kwa matumizi ya binadamu.

Hali hiyo imesababisha wakazi hao kutoa tamko na kutishia kwamba siku ya ujio wa Rais Jakaya Kikwete, katika ziara ambayo anatarajia kuifanya hivi karibuni katika kipindi cha mwezi Mei mwaka huu mkoani humo hususani katika wilaya ya Mbinga, wapo tayari kulala barabarani kwa lengo la kushinikiza msafara huo usimame ili waweze kutoa kilio chao kwa kiongozi huyo wa kitaifa na kiweze kufanyiwa kazi haraka.

Walisema kufanya hivyo kunatokana na uongozi wa wilaya hiyo kuwa na kasi ndogo, ya uchukuaji wa hatua za kuwahamisha watu waharibifu katika eneo ambako chanzo cha maji kimejengwa na kugharimu mradi mzima wa maji uliosambazwa kijijini hapo kufikia shilingi milioni 479 kwa ufadhili wa benki ya dunia.


Kauli hiyo ilitolewa na baadhi ya viongozi wa kata ya Kigonsera kwenye mazungumzo mafupi yaliyofanyika katika ofisi za kata hiyo, yaliyojumuisha Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga Allanus Ngahy na viongozi wengine wa halmashauri ya wilaya hiyo.

Walisema chanzo cha maji hayo kuwa machafu kinatokana na uharibifu unaofanywa katika chanzo kikuu cha maji ambacho kimejengwa katika mlima Kigonsera uliopo katika kijiji hicho.

Walieleza kuwa watu wachache ambao wametakiwa kuhama wanaoishi karibu na chanzo hicho, wamekuwa na kiburi na kufikia hatua hivi sasa wanaendesha shughuli za kilimo cha mazao ya aina mbalimbali karibu na chanzo hicho jambo ambalo linasababisha kuwepo na uchafuzi wa mazingira na hata kutishia kutoweka kwa uoto wa asili.

“Wananchi tunaiomba serikali ituruhusu tuchukue hatua sisi wenyewe ya kuwahamisha wale watu kule milimani maana viongozi wetu wa wilaya inaonesha mmeshindwa, tunasema ujio wa Rais tunajiandaa kulala barabarani ikiwa ni ishara ya kilio cha kutaka wale watu wahame, kwa nini viongozi wetu wa wilaya hamchukui hatua za haraka”,? walihoji.

Kwa ujumla licha ya serikali kugharimia fedha nyingi kupitia ufadhili wa benki ya dunia kujenga mradi huo wa maji katika kijiji hicho cha Kigonsera, hali imekuwa tete kufuatia mradi huo chanzo cha maji yalikotegwa kuchafuliwa na kufikia hatua kuwa na uwingi wa tope na takataka ambazo zinahatarisha usalama wa maji hayo kuyatumia binadamu, kutokana na shughuli za kilimo zinazoendelea kufanywa huko hadi sasa.



No comments: