Friday, March 7, 2014

HOSPITALI YAPEWA MSAADA WA VIFAA TIBA



Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

HOSPITALI ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, imepewa msaada wa vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 5,530,000 kwa lengo la kusaidia utoaji wa huduma bora za matibabu kwa wagonjwa.

Vifaa hivyo vilitolewa na Mbunge wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo wakati alipokuwa ametembelea hospitalini hapo, kwa lengo la kujionea changamoto mbalimbali ambazo zinakwamisha utoaji wa huduma za matibabu.

Kayombo alikabidhi vifaa vya kitengo cha maabara ambavyo ni Darubini mbili, mashine za kupimia magonjwa ya sukari na moyo ambapo hospitali hiyo inakabiliwa na upungufu wa vifaa hivyo.


Awali Mbunge huyo alisema ni jambo la kusikitisha kuona hospitali inashindwa kutoa huduma zake ipasavyo kutokana na kukosekana kwa madawa au vifaa tiba, hivyo aliutaka uongozi husika kuhakikisha unatoa taarifa zake kwa wakati serikalini ili kuweza kuondokana na matatizo hayo.

Naye Mganga mfawidhi wa hospitali ya wilaya ya Mbinga, Elisha Robert alieleza kuwa hivi sasa wamekuwa wakijituma kufanya kazi kwa bidii ikiwemo kuzingatia taratibu zilizowekwa, wakihakikisha kwamba hospitali wakati wote inakuwa na vitendea kazi na madawa ya kutosha ili kuondoa kero mbalimbali kwa wagonjwa.

No comments: