Sunday, May 18, 2014

ASKOFU MKUU WA JIMBO KUU LA SONGEA ASIMIKWA, AWATAKA WATANZANIA KUDUMISHA MUUNGANO

Askofu Mkuu wa Jimbo kuu la Songea mkoani Ruvuma, Damian Dallu.



















Na Kassian Nyandindi,

Songea.

ASKOFU mkuu wa Jimbo kuu la Songea mkoani Ruvuma, Mhashamu Damian Dallu amewataka Watanzania kuuenzi na kudumisha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambao umedumu kwa miaka 50 sasa, kwa manufaa ya wananchi wa pande zote mbili.

Pia alisema Watanzania waliungana kwa moyo wao wenyewe na sio kwa karatasi, hivyo wanaohangaika kutafuta karatasi zenye maelezo ya muungano huo, wanapoteza muda na kwamba mchakato wa katiba mpya usipewe nafasi ya kuuangamiza taifa hili.

Kauli hiyo aliitoa leo mara baada ya kumalizika kwa ibada ya kusimikwa kuwa Askofu mkuu wa jimbo hilo, ambalo lilikuwa wazi baada ya kujiuzulu aliyekuwa Askofu wake Norbert Mtega mwaka mmoja uliopita.


Mhashamu Dallu alisema kila mtanzania anaowajibu mkubwa wa kuhakikisha anatenga muda wa kuliombea taifa lake hasa wakati huu ambao mchakato wa katiba mpya unaendelea, kwani bila kufanya hivyo kutakuwa na uwezekano mkubwa wa kuwapa mwanya maadui ambao kimsingi hawaonyeshi kulitakia mema taifa hili.

“Imepita miaka hamsini tukiwa pamoja hivyo tusikubali kuvurugwa na watu wachache, anayetafuta katiba mpya kwa manufaa yake binafsi hapaswi kuungwa mkono hata kidogo lazima katiba izingatie matakwa ya watanzania wote na sio kikundi cha watu wachache wanaodhani kupatikana kwa aina fulani ya katiba kutawanufaisha”, alisema Dallu.

Alieleza kuwa uwepo wa katiba mpya haimaanishi matatizo ya watanzania yatakuwa yamemalizika, hivyo iwe katiba ya zamani au inayoendelea kutafutwa kama wananchi hawatashirikiana na serikali yao kikamilifu katika kujiletea maendeleo hali itabaki ileile.

Aidha alisisitiza kuwa kanisa katoliki litaendelea kushirikiana na serikali katika kuendeleza shughuli za kijamii ambapo itaendelea kujenga zahanati, vituo vya afya, hospitali na shule ili jamii iweze kupata huduma hizo jirani kutokana na ukweli kwamba binadamu anamahitaji ya kimwili na kiroho.

Awali Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Anne Makinda, aliwaasa watanzania juu ya umuhimu wa kufanya kazi ili kuondokana na utegemezi ambao kimsingi umekuwa ni kikwazo katika kujiletea maendeleo, iwe ya pamoja au ya mtu mmoja mmoja.

Makinda alisema serikali inathamini mchango mkubwa unaotolewa na taasisi mbalimbali hapa nchini hususani za dini, hivyo itaendelea kutoa ushirikiano wa dhati ikiwemo kuandaa mazingira mazuri ambayo hayatakuwa kikwazo pale ambapo taasisi hizo zinataka kuwekeza kwa ajili ya kuwanufaisha wananchi.

Aliwataka watanzania kuwa makini na watu wenye tabia ya kuwashawishi wasijishughulishe kimaendeleo kwani kufanya hivyo itakuwa hawawatakii mema, kutokana na kauli zao zisizo za msingi kuwa serikali ndiyo yenye jukumu la kufanya kila kitu kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wake.

No comments: