Monday, May 26, 2014

VIONGOZI CCM WANAOFANYA KAMPENI KABLA YA WAKATI KUCHUKULIWA HATUA ZA KISHERIA

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, Josephat Ndulango, akisisitiza jambo wakati alipokuwa akizungumza na Waandishi wa habari ofisini kwake. (Picha na Gwiji la matukio Ruvuma)

Na Kassian Nyandindi,
Songea.

CHAMA cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, kimewataka viongozi wake kuacha kufanya kampeni kabla ya wakati na atakayebainika hatua kali za kisheria, zitachukuliwa ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Sambamba na hilo kimewataka kuepukana na makundi, na badala yake kupitia mikutano ya wananchi waeleze utekelezaji wa ilani ya CCM ili kuweza kujenga misingi ya kukiimarisha chama, na wananchi waweze kutambua nini kimewafanyia.

Rai hiyo ilitolewa na Katibu wa Chama cha Mapinduzi wilaya ya Songea, Josephat Ndulango alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake juu ya mikakati ya kukiimarisha chama hicho.

Ndulango alisema Watendaji katika maeneo mbalimbali wilayani humo baadhi yao wamekuwa kikwazo katika kusukuma mbele maendeleo ya wananchi, hivyo wamesisitizwa kuacha kujiingiza kwenye mambo ya kisiasa badala yake wazingatie majukumu yao ya kazi.


“Malalamiko mengi tuliyoyapata watendaji wengi ni kuwa wabadhirifu katika miradi ya wananchi, tumefuatilia na hatua zimeanza kuchukuliwa ili kukomesha hali hii isiweze kuendelea na wananchi waweze kunufaika na miradi yao”, alisema.

Pamoja na mambo mengine aliwaasa wananchi waache mambo ya ushabiki wa kisiasa, wawe tayari kuchangia nguvu zao katika miradi ya maendeleo kwa faida yao ya kizazi cha sasa na kijacho.

“Hatuko tayari kuona miradi ya maendeleo inashindwa kusonga mbele kwa sababu ya mambo ya kisiasa, ni wakati sasa wa kujituma na sio kukaa muda mwingi kulumbana pasipo faida yoyote”, alisema Ndulango.

Hata hivyo Katibu huyo alifafanua ni vyema katika uchaguzi ujao wa serikali za mitaa, wananchi waanze kufikiria kuanzia sasa juu ya kupata viongozi bora na waache tabia ya kuwaweka viongozi madarakani kwa majaribio.

No comments: