Sunday, December 28, 2014

TAMISEMI MKURUGENZI WENU WA MBINGA ANA MATATIZO CHUKUENI HATUA SASA KABLA KIDONDA HAKIJAWA SUGU

Hawa Ghasia, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI)
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MAPYA yanaendelea kuibuka katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, ambapo baadhi ya Wafanyakazi wenye mikataba ya ajira ya muda wamemlalamikia Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo Hussein Ngaga, kwamba amekuwa ni mtu wa kuwatolea lugha zenye kukatisha tamaa ya kufanya kazi na kutowalipa mishahara yao kwa wakati. 

Wakizungumza kwa nyakati tofauti huku wakiomba majina yao yasitajwe kwa kuhofia usalama wa kazi zao wakidai kufukuzwa kazi, walisema Mkurugenzi huyo amekuwa akiwatolea lugha zenye ukali hasa pale wanapokuwa wakidai madai yao ya msingi, kama vile fedha za malipo ya kazi walizofanya.

Wengine walifafanua kuwa hata mishahara yao ambayo inabidi walipwe tarehe husika za mwisho wa mwezi, kwa mujibu wa taratibu na sheria zilizowekwa na serikali, Ngaga amekuwa hafanyi hivyo badala yake amekuwa akiwalipa kwa kuchelewesha.


“Mkurugenzi huyu anakera sana, hata sisi wafanyakazi wa chini ambao tumeajiriwa kwa mikataba ya muda katika halmashauri hii, wakati mwingine mishahara yetu amekuwa akipitiliza tarehe za kutulipa, malipo amekuwa akiyatekeleza wakati mwingine kwa mwezi unaofuata tarehe 14 hadi 15”, walisema.

Kadhalika waliongeza kuwa katika kipindi cha nyuma kabla ya Mkurugenzi huyo kuhamia katika halmashauri hiyo ya Mbinga, walikuwa wakilipwa madai yao kwa wakati na kuwafanya wafanye kazi kwa moyo, licha ya kulipwa mishahara midogo kulingana na elimu waliyonayo.

Walidai kwamba hata mikataba ya nyuma kabla ya yeye kuwasili hapa Mbinga, ilikuwa inawaruhusu kukopa fedha katika taasisi za fedha kama vile benki, lakini alipoingia yeye amebadilisha utaratibu na sasa maisha yao yamekuwa magumu kutokana na kushindwa kumudu gharama za maisha.

Wafanyakazi wanaomlalamikia mkurugenzi Ngaga ni wa kada ya Madereva, Walinzi, na Wahudumu wa usafi (Mazingira) ambao baadhi yao wamekuwa wakifanya kazi kwa kuingia mikataba ya miezi mitatu mitatu na kwamba kila baada ya miezi hiyo, mwajiriwa hujaza makubaliano mengine.

Utafiti uliofanywa na mwandishi wa habari hizi umegundua hata katika mikataba hiyo ambayo nakala yake tunayo, inakataza kuwa Mwajiriwa huyo haruhusiwi kukopa fedha au kitu chochote katika taasisi yoyote ya fedha, kwa udhamini wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga.

Vilevile mwajiriwa katika kipindi cha kutekeleza mkataba wake, atakatwa fedha za mafao na Mfuko wa Pensheni ya Watumishi wa Serikali za Mitaa (LAPF) ambazo atalipwa baada ya kwisha au kusitisha makubaliano husika yaliyomo ndani ya mkataba, ambapo mwajiriwa atatakiwa pia kutoa taarifa ya kwisha kwa makubaliano yake katika mfuko huo na kuomba mafao yake.

Mkurugenzi mtendaji Halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Bw. Ngaga alipotafutwa ili aweze kutolea ufafanuzi juu ya malalamiko hayo wakati habari hizi zinaingia mitamboni, simu yake haikupatikana na taarifa zilizotufikia kutoka kwenye vyanzo vyetu vya habari vilituthibitishia kwamba yupo safarini nje ya wilaya hiyo.

No comments: