Thursday, January 2, 2014

GAUDENCE KAYOMBO ASIKITISHWA NA UJENZI WA BARABARA KIWANGO CHA LAMI KUTOKA SONGEA KWENDA MBINGA

Gaudence Kayombo.



















Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MBUNGE wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo amesema, ujenzi wa  barabara kiwango cha lami kuanzia eneo la Likuyufusi pacha ya Peramiho wilaya ya Songea hadi Mbinga, katika baadhi ya maeneo umejengwa kwa kiwango kisichoridhisha kutokana na barabara hiyo kuanza kuwekwa viraka kabla ya kukabidhiwa rasmi mikononi mwa serikali.

Kayombo alisema hayo alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini hapa, huku akisisitiza kuwa hali hiyo huenda ikatokana na wataalamu husika kutozingatia ipasavyo vipimo vya kimaabara na ndio maana barabara hiyo hubomoka na kulazimika kuweka viraka.

Alisema uzembe huo uliofanywa wa kutozingatia viwango husika ni hasara kubwa kwa serikali kutokana na fedha nyingi iliyotumika kujengea barabara hiyo kutofanya kazi yake kama ilivyokusudiwa.


“Barabara ya kutoka Songea kwenda Namtumbo imejengwa vizuri sana haina viraka, ni jambo la kusikitisha sana barabara hii ya kwetu toka Songea kwenda Mbinga bado haijakamilika ujenzi wake leo tunaanza kuweka viraka, kweli tutaweza kudumu nayo kwa miaka mingi ? ”,  alihoji Kayombo.

Kwa ujumla barabara hiyo ambayo ni ya kilometa 78 inagharimu kiasi cha shilingi bilioni 79.8 na sasa ipo katika hatua za mwisho kukamilika ujenzi wake.

Fedha za ujenzi huo ni miongoni mwa dola 698 za Kimarekani zilizotolewa nyakati za mwisho katika utawala wa Rais mstaafu George Bush, ikiwa ni sehemu ya msaada kwa ajili ya kujenga miradi mbalimbali ya kimaendeleo hapa nchini.
 
Kampuni ya Sinohydro Corporation Limited kutoka nchi ya China, ndiyo imekabidhiwa kazi ya ujenzi wa kiwango cha lami  na kwamba ujenzi wake ni wa miezi 27.

Hata hivyo ni mradi mkubwa wa pili hapa mkoani Ruvuma, wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami ambao umetanguliwa na mradi mwingine wa ujenzi wa barabara ya lami kutoka Songea hadi Namtumbo ikiwa ni utekelezaji wa maendeleo ukanda wa Mtwara.
 

No comments: