Saturday, August 9, 2014

ASILMIA 90 YA FAMILIA WILAYANI MBINGA HUTEGEMEA KILIMO NA UFUGAJI

Upande wa kulia Diwani wa kata ya mkako Ambrose Nchimbi akiangalia nyara mbalimbali za serikali katika banda la Maliasili na mazingira wilayani Mbinga, siku ya maonesho ya wakulima yaliyofanyika katika kilele chake kijiji cha Lusonga wilayani humo.

Mke wa Mbunge wa Jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma, Leah Kayombo akitoa maelezo juu ya shughuli zinazofanywa na umoja wa kikundi cha Mbalawala katika maonesho ya wakulima yaliyofanyika wilayani Mbinga katika kijiji cha Lusonga mkoani humo.


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa asilimia 90 ya familia wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, hutegemea kilimo na ufugaji katika kuendesha shughuli za kimaendeleo katika maisha yao ya kila siku.

Aidha kati ya hizo asilimia 50 zinazalisha zao la kahawa wilayani humo, na ndio zao kuu ambalo hutegemewa kwa kukuza uchumi wa wilaya hiyo.

Hayo yalisemwa na Kaimu mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Mbinga, Oscar Yaspesa alipokuwa akisoma taarifa ya maendeleo ya kilimo na mifugo kwa mgeni rasmi Diwani wa kata ya Mkako Ambrose Nchimbi alipokuwa kwenye maonesho ya wakulima (Nane nane) yaliyofanyika katika kijiji cha Lusonga wilayani humo.


Alisema mikakati ya kuendeleza sekta hiyo muhimu ni pamoja na kuwaendeleza vijana katika kilimo na ufugaji ili kuweza kuleta tija katika jamii.

Jumla ya Hekta 108,955 za mazao ya chakula zilizalishwa katika msimu wa kilimo 2013/ 2014 na kwamba uzalishaji huo, ulitokana na serikali kutoa vocha 55,350 za pembejeo za kilimo kwa wakulima.

Yapesa alisema pia huzingatia utoaji wa elimu ya kilimo bora kwa wakulima kupitia shamba darasa, ambapo kufikia mwishoni mwa mwezi Juni mwaka huu wilaya ina jumla ya vikundi 218 na maombi ya kuanzisha vingine yanaendelea kupokelewa.

Alizitaja changamoto wanazokabiliana nazo ni kutokuwa na soko la uhakika kwa mazao ya chakula yanayozalishwa wilayani Mbinga, ikiwemo suala la uhaba wa wataalamu wa ugani na mifugo.

Pia bei kubwa za pembejeo za kilimo nalo limekuwa tatizo sugu ambalo wakulima wengi wilayani humo, hushindwa kumudu gharama ya kuzinunua na hivyo kushindwa kutosheleza mahitaji yao ya msingi.

Kwa upande wake Diwani Nchimbi alisema umuhimu wa maonesho hayo ni kuwakutanisha wakulima, wadau wa kilimo, mifugo, uvuvi na ushirika hivyo serikali itaendelea kushughulikia suala la gharama kubwa ya pembejeo, ikiwemo kuwasiliana na taasisi mbalimbali nchini za mikopo ili ziwakopeshe wakulima kwa gharama nafuu.


No comments: