Saturday, August 30, 2014

BODI YA LESENI YA GHALA YATAKIWA KUTEKELEZA MAJUKUMU YAKE IPASAVYO



Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

WADAU wanaozalisha mazao ya chakula na biashara wilayani Mbinga na Nyasa mkoa wa Ruvuma, wameitaka bodi ya leseni ya ghala Tanzania kuhakikisha kwamba wanatekeleza mapema mfumo wa stakabadhi ghalani hususani kwa zao la kahawa, ili kuweza kuzuia uharibifu na upotevu wa mazao wilayani humo.

Walisema lengo la kufanya hivyo itasaidia walengwa wa mfumo huo ambao ni wakulima, wafanyabiashara na vikundi husika kuweza kujijengea uwezo na hatimaye waweze kuinua uchumi wao.

Ilielezwa kuwa mfumo wa stakabadhi ghalani endapo utatekelezwa kwa haraka katika wilaya hizo, utaleta fursa ya kufanyika kwa mnada wa zao la kahawa na kuuzwa katika kipindi hiki cha msimu wa mavuno ya zao hilo.


Hayo yalisemwa na Wadau hao walipokuwa kwenye mafunzo ya siku moja, yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Parokia Jimbo Katoliki la Mbinga uliopo mjini hapa ambayo yalishirikisha wakulima, makampuni, maofisa ugani, vikundi mbalimbali na wadau wa kahawa wa wilaya ya Mbinga na Nyasa.

“Lengo letu hapa ni kumkwamua mkulima aweze kupiga hatua moja mbele katika sekta ya kilimo, pia kutafuta soko na kuongeza thamani ya mazao yetu ili tuweze kunufaika”, walisema.

Aidha kwa upande wake Mratibu wa shirikisho la wakulima kutoka wilaya ya Nyasa (MVIWATA) Ludwig Kumburu alieleza kuwa, katika kufanikisha jambo hilo aliitaka bodi ya leseni ghalani hapa nchini kuwa karibu na maofisa ugani ili kuweza kuleta ufanisi mzuri katika kazi.

Kumburu alisema miundombinu ya kuwezesha mfumo wa stakabadhi ghalani kufanya kazi yake umekuwa mgumu, hivyo ni vyema serikali ikaona umuhimu wa kuweka sawa suala hilo ikiwemo upatikanaji haraka wa leseni ya umiliki wa ghala la kuhifadhia mazao husika.

Pamoja na mambo mengine mwakilishi kutoka bodi ya leseni ya ghala Tanzania, Grace Tarimo alisema elimu kwa wadau juu ya mfumo wenyewe unavyoendeshwa bado haujawafikia wahusika ipasavyo hivyo bodi itafanya jitihada za kuweza kuweka sawa jambo hili kwa kufikisha elimu kwa wadau husika.
    

No comments: