Thursday, October 17, 2013

MBUNGE KAYOMBO ASIKITISHWA NA HATUA YA SERIKALI KUPIGA MABOMU WANANCHI, ASEMA YUPO TAYARI KUFIKISHA MADAI YAO KWA MWANASHERIA ILI HAKI ZAO ZIWEZE KUPATIKANA

Mtambo ukiendelea na uchimbaji wa Makaa ya mawe katika mgodi wa Ngaka, huko katika kijiji cha Ntunduaro kata Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma.



Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.


HATUA iliyochukuliwa na Serikali kupiga mabomu kwa ajili ya kuwatawanya wananchi waliokuwa wakiandamana kwa amani katika kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda mkoani Ruvuma, Mbunge wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo, ameshusha lawama nzito na kusema hajafurahishwa na kitendo hicho.


Gaudence Kayombo amesema, nguvu iliyotumika ni kubwa na hapakuwa na sababu kwa serikali kufanya hivyo, kutokana na wananchi wa kijiji hicho madai yao wanayoyadai ni ya msingi na muda mrefu sasa, umepita hawajatekelezewa.


Mbunge huyo alisema hayo alipokuwa akihojiwa na Mwandishi wa habari hizi juu ya wananchi hao wamekuwa wakilalamika kwa muda mrefu, wakidai fidia zao katika eneo ambalo waliondolewa kwa ajili ya kupisha shughuli za mgodi wa Ngaka, ambapo huchimbwa makaa ya mawe.


”Kule imetumika nguvu kubwa ya polisi kupiga mabomu wale wananchi, hapakuwa na sababu badala yake serikali itoke mbele na ieleze hawa wanaodai fidia zao lini watalipwa”, alisema Kayombo.


Alisema kuwa kuna baadhi yao wengine hawajalipwa kabisa na wananchi karibu 400 ambao awali walilipwa fidia zao, ilionekana fedha walizolipwa ni kidogo hivyo nao walipewa ahadi ya kuongezewa malipo mengine, jambo ambalo hadi leo hii halijatekelezwa.


Kayombo alisisitiza akisema ni vyema serikali itimize wajibu wake, kwa kuelimisha wananchi na sio kutumia nguvu kubwa kwa kuwapiga mabomu ambayo yanaathiri jamii.

Monday, October 14, 2013

MJUMBE WA MKUTANO MKUU TAIFA CCM WILAYANI TUNDURU, AKAMATWA NA KIKOSI CHA OPARESHENI OKOA MALIASILI NA KUHOJIWA KWA MASAA NANE


















Na Steven Augustino,
Tunduru.

OPARESHENI Okoa Maliasili inayoendelea kufukuta na kupamba moto katika wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, imemkumba Mjumbe wa mkutano mkuu wa Chama cha Mapinduzi(CCM) Taifa, Sultani Ajili Kalolo na kuhojiwa kwa zaidi ya masaa nane akiwa anatuhumiwa kushiriki katika vitendo vya ujangili wa kuua Tembo.

Tukio la kukamatwa kwa Mneki huyo lilitokea Oktoba 13 mwaka huu huku wilaya hiyo, ikiwa na kumbukumbu ya kukamatwa kwa bunduki zaidi ya 300 na risasi 667 katika oparesheni zuia ujangili  iliyobatizwa jina la “Wazee wa tintedi”.

Katika tukio hilo Mjumbe huyo wa mkutano mkuu wa CCM taifa (Mneki) Ajili Kalolo alikamatwa akiwa nyumbani kwake eneo la shule  ya msingi Muungano wilayani Tunduru, na kuondoka naye huku.

Baadaye dhamana ilitolewa kwa masharti maalum ambapo hadi kufikia majira ya saa 12 jioni kikosi hicho maalumu kilichokmtia mbaroni, kiliweza kuruhusu ndugu zake wamdhamini kwa masharti ya kwenda kuripoti kituo cha Polisi wilayani humo, Jumatano ya wiki hii.

Akizungumzia tukio hilo kwa njia ya simu Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, Deusdedith Nsimeki pamoja na kudai kuwa yeye siyo msemaji wa Oparesheni hiyo Iakini alikiri kuwepo kwa tukio hilo na kuongeza kuwa watu wanaokamatwa ni wale waliohusika katika matukio hayo pamoja na madalali wa biashara ya meno ya Tembo.

“Unajua mimi siyo msemaji wa Oparesheni hiyo, lakini ninazotaarifa za
Kushikiliwa kwa muda kwa kiongozi huyo wa ngazi ya juu katika Chama
Cha Mapinduzi”, alisema Kamanda Nsimeki na Kuongeza kuwa hali hiyo imetokana na kiongozi huyo kutajwa kuwa ni miongoni mwa Majangili wa Tembo.

Alisema Opareshini hii inatekelezwa kisheria, hivyo haiwezi kumuonea aibu kiongozi ama mtu maarufu hivyo wote wanaokamatwa wamekuwa wakitajwa kuwa miongoni  mwa wahusika kwa namna moja na matukio ya vitendo vya kijangili hivyo oparesheni hiyo haitawaonea watu wasio husika.

Kamanda Nsimeki aliendelea kueleza kuwa Oparesheni hiyo iliyopewa jina la Okoa maliasili inayoendelea wilayani Tunduru, pamoja na kuenea karibu nchi nzima, kwa kujumuisha mikoa husika pia inaendelea katika wilaya ya Namtumbo katika Kijiji cha Likusenkuse na Liparamba wilayani Mbinga lengo ikiwa ni kukomesha vitendo vya ujangili wa mauaji ya Tembo na maliasili nyingine za Tanzania.

Alisema Oparesheni hiyo inahusisha vyombo mbalimbali vya majeshi ya ya ulinzi katika nchi yetu, wamo pia askari wa jeshi la wananchi wa Tanzania, usalama wa taifa, uhamiaji na Polisi ambao kwa pamoja wanapitia taarifa mbalimbali na kuwakamata watu wote ambao wanakuwa wakitajwa kujihushisha na matukio ya ujangili.

Kwa mujibu wa taarifa za oparesheni iliyofanyika Agosti mwaka 2012
iliyoendeshwa chini ya usimamizi wa serikali, kwa ajili ya kuzuia vitendo vya uhalifu na ujangili  iliyofanyika wilayani Tunduru mkoani Ruvuma jumla mali zenye thamani ya milioni 618.408, bunduki zaidi ya 300 na risasi  667 na maganda ya risasi 150 zilikamatwa baada ya kubainika kuwa zinamilikiwa kinyume cha sheria.   

TUNDURU MISHAHARA YA WALIMU NI TATIZO

Waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi, Shukuru Kawambwa.

























Na Steven Augustino,
Tunduru.


ZAIDI ya watumishi 250 wa halmashauri ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, hawajaenda kazini kwa muda wa wiki tatu sasa, wakiwa wanasubiria kupokea mishahara yao.


Hali hiyo imetokana na kuwepo kwa sintofahamu iliyodaiwa kusababishwa na ofisi za Hazina, baada ya kuwaingizia mishahara yao ya mwezi wa tisa mwaka huu huku ikiwa na nyongeza ya mapunjo ya mishahara yao ambayo inadaiwa kuwa majina ya watumishi hao hao kuwa ndio walioingiziwa fedha hizo, kupitia utaratibu huo katika mishahara yao waliyolipwa mwezi wa tisa mwaka 2012.


Wakizungumza na mtandao huu kwa nyakati tofauti baadhi ya watumishi hao pamoja na kuwatuhumu viongozi wa halmashauri ya wilaya hiyo kutofuatilia na kutatua tatizo hilo, katika ufuatiliaji wa haki zao hizo walisema kuwa hali hiyo imewafanya kuishi katika maisha duni na wengine kuwa ombaomba kwa watu ili waweze kuhudumia familia zao.


Walisema kutokana na hali hiyo pia watumishi hao wakiwemo walimu wanaofanya kazi zao nje ya mji wa Tunduru, wameshindwa kurejea katika vituo vyao vya kazi kutokana na kukosa hata fedha za kujikimu wakati wanasubiri hatima ya kupatikana kwa mishahara yao  ambayo pia ingewawezesha kupata nauli ya kuwawezesha kurejea ma kwao katika vituo vyao vya kazi.


Katibu wa Chama Cha Walimu(CWT) wilayani humo Lazaro Saulo alisema kuwa hali ya mahangaiko wanayopata sasa wanachama wake, hivi sasa yameweka ofisi yake katika mazingira magumu na kumfanya ahamishie shughuli zake katika ofisi za Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo hadi tatizo hilo litakapo tatuliwa.

Friday, October 11, 2013

SAKATA LA MAANDAMANO MGODI WA MAKAA YA MAWE, WATU SABA WAPANDISHWA KIZIMBANI

Washtakiwa ambao wanatuhumiwa kufanya maandamano haramu, wakiwa katika Mahakama ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma wakisubiri kusomewa mashtaka yao.  (Picha na Kassian Nyandindi)

Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

WATU saba wakazi wa kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya wilaya ya Mbinga mkoani humo kwa tuhuma ya kufanya maandamano haramu, kuziba barabara na kuharibu mali.

Katika mahakama hiyo mwendesha mashtaka msaidizi wa polisi Inspekta Nassibu Sued Kassim, alidai mbele ya Hakimu Joackimu Mwakyolo kuwa tukio hilo lilitokea Oktoba 10 mwaka huu majira ya saa 2 asubuhi.

Inspekta Kassim alidai mahakamani hapo kuwa watuhumiwa hao vilevile walishambulia kibanda cha walinzi wa kampuni ya Tancoal Energy, ambayo inafanya shughuli za uchimbaji wa makaa ya mawe kijijini hapo na kusababisha hasara ya shilingi milioni 2.

Aliwataja washtakiwa hao kuwa ni Siprian Mhagama, Jackson Nkwera, Ambrose Mhagama, George Nkondora, Theodos Komba, Angelus Mgaya na Martin Mapunda.

Kesi hiyo itakuja kutajwa tena Oktoba 24 mwaka huu na washtakiwa wamenyimwa dhamana baada ya Mwendesha mashtaka huyo kuiomba mahakama kuwa endapo watapatiwa dhamana, watuhumiwa hao wanaweza kuvuruga ushahidi kutokana na shauri hilo bado linaendelea kwa uchunguzi na baadhi ya watuhumiwa wengine bado wanatafutwa na jeshi la polisi kutokana na kutokomea kusikojulikana.

WANANCHI WAANDAMANA WAFUNGA BARABARA WAKIDAI HADI WALIPWE FIDIA ZAO, POLISI WAPIGA MABOMU

 
Gaudence Kayombo, Mbunge wa jimbo la Mbinga.

 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.
 
JESHI   la Polisi  mkoani Ruvuma  limelazimika kutumia nguvu ya kuwatawanya wananchi wenye hasira kali, kwa kuwapiga mabomu ya machozi ambao waliandamana wakidai fidia zao ambazo hawajalipwa kwa muda mrefu katika eneo la mgodi wa makaa ya mawe Ngaka, uliopo kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoani humo.
 
Wananchi hao walizuia magari ya mgodi huo ambayo yalikuwa yakibeba mkaa wa mawe, huku wakipaza sauti zao hadi walipwe kwanza fedha zao wanazodai kwa muda mrefu ndipo kazi ya uchimbaji na usafirishaji wa mkaa iweze kuendelea.
 
Kufuatia tukio hilo jeshi hilo la polisi linawashikilia  wanakijiji watano  wakiwemo mwenyekiti wa serikali  ya kijiji cha Ntunduwaro, afisa  mtendaji wa kijiji hicho na  afisa  mtendaji wa kata ya Ruanda kutokana na vurugu hizo.
 
Habari  zilizopatikana mjini Songea ambazo zimethibitishwa na  Kamanda  wa polisi wa mkoa wa Ruvuma Deusdedit  Nsimeki zimesema  kuwa tukio hilo lilianza  kutokea  juzi  majira  ya saa  za asubuhi, ambako  wananchi  wa kijiji cha Ntunduwaro walijipanga  na kufunga  barabara inayokwenda kwenye mgodi huo wa makaa ya  mawe ambao upo karibu na kijiji  hicho.

Thursday, October 10, 2013

SHEREHE ZA UZINDUZI MRADI WA KIKOSI KAZI WAFANA, MKUU WA WILAYA ASEMA POLISI ACHENI KUPIGA RAIA NA ENDAPO MTAFANYA HIVYO MTAONEKANA MNAJITAWALA WENYEWE

Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga, naye alisisitiza kwa kuwataka Polisi kuacha kupiga raia na endapo watafanya hivyo, wataonekana kama ni watu ambao wanajitawala wao wenyewe.

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, Deusdedit Nsimeki akisisitiza jambo siku ya uzinduzi wa mradi wa kikosi kazi (task force), kwa kuwataka wananchi kujenga ushirikiano na jeshi la polisi ili liweze kufanya kazi zake kwa ufanisi mkubwa.

Baadhi ya wananchi nao walihudhuria siku hiyo ya uzinduzi.

         Vikundi vya ngoma navyo havikuwa mbali katika kutumbuiza. (Picha zote na Gwiji la matukio mkoani Ruvuma)

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WITO umetolewa kwa Askari Polisi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kuacha kupiga raia na endapo watafanya hivyo, wataonekana kama ni watu ambao wanajitawala wao wenyewe.

Sambamba na hilo wametakiwa kujenga ushirikiano na wananchi ili kuweza kuleta ufanisi katika utendaji wa kazi zao kila siku, kwa lengo la kuimarisha usalama kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga, alisema hayo alipokuwa mgeni rasmi akizungumza kwenye uzinduzi wa mradi wa kikosi kazi (task force) tarafa ya Mbinga mjini.

Ngaga alisema mradi huo wa kikosi kazi ndani ya tarafa hiyo ambao umeanzishwa hapa wilayani, hauna budi uwe endelevu kwa lengo la kuimarisha kazi zinazofanywa na askari kata, mkuu wa tarafa na vikundi vingine vinavyofanya kazi za kila siku katika kushughulikia miradi mingine ya polisi jamii, ndani ya tarafa nyingine zilizopo mkoani humo.

Tuesday, October 8, 2013

ASKARI MGAMBO WANUSURIKA KUUAWA KATIKA VURUGU WILAYANI MBINGA

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
VURUGU zilizodumu kwa masaa matano zimejitokeza katika kijiji cha Lipilipili kata ya Mpepai wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, na askari wa nne wa Jeshi la mgambo wilayani humo akiwemo ofisa mtendaji wa kijiji hicho, wamenusurika kuuawa kufuatia wananchi wenye hasira kali, kuwashambulia wakiwa kwenye majukumu yao ya kazi.
 
Hali hiyo imejitokeza majira ya saa 1:30 asubuhi, Oktoba 7 mwaka huu ambapo mgambo na mtendaji huyo walikwenda kijijini hapo kutekeleza azimio la kikao cha kamati ya maendeleo ya kata hiyo, ambacho kilifikia uamuzi wa waliokataa katani humo kuchangia shughuli za ujenzi wa maabara na bweni la kulala wanafunzi katika shule ya sekondari Dokta Shein, wakamatwe na kuchangia kila mmoja shilingi 25,000 ya mchango husika.
 
Akizungumza na waandishi wa habari, ofisa mtendaji wa kata ya Mpepai Anssila Kumburu alisema, katika kikao cha kamati hiyo kilichoketi kijiji cha Luhangai Septemba 27 mwaka huu, Mwenyekiti wa kamati ambaye ni Diwani wa kata hiyo Francis Nchimbi ndiyo yeye aliyetangaza uamuzi huo wa kuleta mgambo, kwa ajili ya kusaidia kuwasaka wale wote  waliokataa kuchangia miradi hiyo ya maendeleo.
 
Kumburu alisema Septemba 30 mwaka huu ndipo mgambo hao walianza kutekeleza jukumu hiyo kwa kushirikikiana na maofisa watendaji wa vijiji vya kata ya Mpepai, kupita kwa kila kaya kukusanya michango husika ambapo kati ya vijiji vitano vya kata hiyo, vijiji vinne walivyopita hapakuwa na tatizo lolote lile wananchi wake waliitikia wito huo kwa kutoa michango waliyoelekezwa.

Saturday, October 5, 2013

MWAMBUNGU ALIAGIZA JESHI LA POLISI MKOANI RUVUMA KUWACHUKULIA HATUA MADEREVA WAZEMBE

Kamanda wa Polisi mkoani Ruvuma, Deusdedith Nsimeki.


























Na Muhidin Amri,
Songea.


JESHI la polisi mkoani Ruvuma, limeagizwa kuwachukulia hatua madereva wazembe wanaosababisha vifo vya watu wasiokuwa na hatia kunakotokana na matumizi mabaya ya barabara, kwa kuendesha vyombo vya moto huku wakiwa wanaongea na simu au kusikiliza muziki wawapo barabarani.


Hatua hiyo ya serikali inatokana na ongezeko kubwa la ajali za barabarani mara kwa mara, kunakosababishwa na madereva wazembe wasiozingatia sheria kwa kuongea na simu au kwa kusikiliza muziki kwa kuweka vifaa masikioni, hali inayomfanya dereva kukosa umakini katika matumizi ya barabara na chombo anachokiendesha.


Agizo hilo limetolewa juzi mjini Songea na Mkuu wa mkoa huo Said Mwambungu alipokuwa akifunga kozi  fupi za udereva, ufugaji bora wa kuku na urembo katika chuo cha VETA Songea, ambapo kozi hizo ni mara ya kwanza kutolewa katika vyuo vinavyomilikiwa na mamlaka  stadi ya  elimu na ufundi stadi(VETA) nyanda za juu inayojumuisha mikoa ya Iringa, Njombe na Ruvuma.

NGAGA AWAHIMIZA VIJANA KUJIKITA KATIKA SHUGHULI ZA KIMAENDELEO

Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga(aliyevaa suti nyeusi) akikagua gwaride  wakati wa kufunga mafunzo ya vijana zaidi ya 1000  katika kikosi cha 842 Kj Mlale JKT, kushoto ni mkuu wa gwaride Hilo Capt. Gerald William Rwenyagira. (Picha na Muhidin Amri)



Na Muhidin Amri,
Ruvuma.

VIJANA nchini wamehimizwa kujikita zaidi katika shughuli za maendeleo na kujiepusha kushiriki katika mambo yasiokuwa na manufaa kwao, ambayo yanaweza kuwaharibia mustakabali wa maisha yao ikiwemo  kushiriki kwenye maandamano ya vyama vya siasa ambayo mara nyingi yamekuwa na dhamira ya kuanzisha chuki na uhasama, kati ya serikali na wananchi.


Hayo yamesemwa  hivi karibuni wilayani Songea na Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Senyi Ngaga, wakati akifunga mafunzo ya miezi mitatu kwa vijana wa kujitolea  Operesheni miaka 50 ya JKT na miaka 50 ya vijana kwa mujibu wa sheria, Julai hadi Septemba mwaka huu katika kikosi cha 842 KJ Mlale JKT mkoani humo.


Mkuu huyo wa wilaya alisema vijana wana nafasi kubwa ya kulifanyia mambo mazuri taifa hili, tofauti na wao wanavyofikiria lakini inaonesha kwamba tatizo kubwa walilonalo ni kutojitambua ndiyo maana wanadiriki kushiriki katika mambo ambayo ni tofauti na umri walionao na hata kujikuta wakipoteza muda wao mwingi, katika vitu ambavyo  vinavyowapotezea muda.