Friday, October 11, 2013

WANANCHI WAANDAMANA WAFUNGA BARABARA WAKIDAI HADI WALIPWE FIDIA ZAO, POLISI WAPIGA MABOMU

 
Gaudence Kayombo, Mbunge wa jimbo la Mbinga.

 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.
 
JESHI   la Polisi  mkoani Ruvuma  limelazimika kutumia nguvu ya kuwatawanya wananchi wenye hasira kali, kwa kuwapiga mabomu ya machozi ambao waliandamana wakidai fidia zao ambazo hawajalipwa kwa muda mrefu katika eneo la mgodi wa makaa ya mawe Ngaka, uliopo kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoani humo.
 
Wananchi hao walizuia magari ya mgodi huo ambayo yalikuwa yakibeba mkaa wa mawe, huku wakipaza sauti zao hadi walipwe kwanza fedha zao wanazodai kwa muda mrefu ndipo kazi ya uchimbaji na usafirishaji wa mkaa iweze kuendelea.
 
Kufuatia tukio hilo jeshi hilo la polisi linawashikilia  wanakijiji watano  wakiwemo mwenyekiti wa serikali  ya kijiji cha Ntunduwaro, afisa  mtendaji wa kijiji hicho na  afisa  mtendaji wa kata ya Ruanda kutokana na vurugu hizo.
 
Habari  zilizopatikana mjini Songea ambazo zimethibitishwa na  Kamanda  wa polisi wa mkoa wa Ruvuma Deusdedit  Nsimeki zimesema  kuwa tukio hilo lilianza  kutokea  juzi  majira  ya saa  za asubuhi, ambako  wananchi  wa kijiji cha Ntunduwaro walijipanga  na kufunga  barabara inayokwenda kwenye mgodi huo wa makaa ya  mawe ambao upo karibu na kijiji  hicho.
 
 
Alisema  wanakijiji  hao  walikuwa  na lengo la kuishinikiza  serikali ili iwalipe nyongeza ya fidia  ambayo  wanadai  kuwa hapo awali walipunjwa wakati wanafanyiwa  tathmini ya mali zao  zilizokuwepo ndani ya maeneo yaliyochukuliwa  na mgodi huo kwamba serikali ilitumia sheria  ya zamani badala  ya sheria  iliyopo hivi sasa  ambayo inaonesha  kuwa ni kubwa.
 
Alifafanua  kuwa  kundi kubwa la  wananchi wakiwemo watoto  na akina mama waliokuwa  wamekaa mbele lililojipanga ni lile  lililolipwa mwanzo  kwa kutumia  sheria ya uthamini ya zamani  ambapo wanadai kuwa  wamekuwa  wakiahidiwa mara kwa mara  na serikali  kuwa  watalipwa kiasi cha fedha cha  fidia  kilichobakia lakini hadi sasa bado hawajalipwa.
 
Alieleza  kuwa kutokana na hali hiyo wanakijiji hao waliamua  kuchukua  uwamuzi wa kuzuia shughuli za magari yanayobeba  makaa ya mawe yasiingie kuchukua makaa  ya mawe wala  kutoka  kwenye  eneo hilo la mgodi.
 
Kufuatia kuwepo kwa vurugu hizo zilizosababisha  shughuli za mgodi  kusimama  kwa siku mbili, polisi baada ya kupewa taarifa hiyo walikwenda kwenye  kijiji hicho  wakiwa  wameongozana  na katibu tawala  wa wilaya ya Mbinga  Idd  Mponda ili kujaribu  kuongea  na wananchi, kuwasihi  waondoe kizuizi hicho  ili magari  yaendelee na kazi ya kusomba  makaa  ya mawe, lakini wananchi walikataa na walimweleza  katibu tawala huyo kuwa  hawamuhitaji kumuona yeye pamoja na watu wengine wala  Mkuu  wa wilaya hiyo kuwasikiliza  wanachotaka  walipwe fedha  zao wanazodai na si vinginevyo.
 
Aliongeza  kusema kuwa  mvutano huo wa mazungumzo kati ya katibu tawala  wa wilaya  hiyo  Mponda  na wanakijiji yalidumu kwa muda mrefu hadi juzi  majira  ya saa tatu  usiku polisi waliamua  kulilinda  eneo hilo na baadaye  walifanikiwa  kuwakamata watu watano  ambao  wanadaiwa  kuwa  ndio waliokuwa  viongozi wa vurugu hizo.
 
Amewataja  wanaoshikiliwa  kuwa ni Mwenyekiti wa serikali ya kijiji  cha  Ntunduwaro  John  Nyimbo, Matrida  Nchimbi ambaye  ni Afisa mtendaji wa kata ya Rwanda, Joachim Ngaponda ambaye  ni Afisa  mtendaji wa kijiji hicho, Mwenyekiti wa kamati ya miradi  ya  kijiji hicho Gallusi Komba  na  John  Joachimu Mahai mkazi wa kijiji cha Malindindo  tarafa  ya Mbuji wote  wanaendlea  kuhojiwa  na jeshi la polisi mkoani Ruvuma.
 
Aidha  Kamanda  Nsimeki alisema pamoja  na polisi kuwashikilia  viongozi hao na baadhi ya wananchi, mnamo jana (leo) majira  ya  saa  za asubuhi vurugu  zilirejea  tena  ambapo  polisi  walilazimika   kutumia  mabomu ya  machozi kuwatawanya  wanakijiji  hao ambao  waliendelea  kuyazuia  magari yaliyokuwa yamebeba makaa  ya mawe  huku  wananchi  wakijitahidi  kuyazuia  yasipite.
 

No comments: