Tuesday, October 29, 2013

UWT YAWATAKA WAZAWA WA NYASA KURUDI NYASA NA KWENDA KUWEKEZA

Ziwa Nyasa.


















Na Dustan Ndunguru,
Nyasa.


JUMUIYA ya Umoja wa wanawake Tanzania(UWT) wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma  imeanza kutoa elimu ya  ujasiriamali kwa wanawake,  ambapo imewataka  waunde vikundi ambavyo vitawasaidia kuwainua kiuchumi na kuwaongezea pato katika familia zao.


Mwenyekiti wa jumuiya hiyo wilayani humo Grace Millinga alisema wamechukua hatua hiyo ya kupita kuhamasisha wanawake wenzao kwa kuwapatia elimu ya ujasiliamali, ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya chama cha Mapinduzi  ya mwaka 2010 baada ya kubaini wanawake wa wilaya hiyo bado wanaishi maisha duni tofauti na wenzao wa wilaya nyingine mkoani humo.


Alisema pamoja na kuwapatia elimu ya ujasiriamali bado wamekuwa wakiwataka kuunda vikundi na kubuni miradi ambayo itawasaidia kuwapatia soko la uhakika, kwa kuuzia bidhaa zao na kuwa na akaunti benki kabla ya kusajili na kutambulika kisheria kama moja ya njia rahisi ya kuweza kukopa fedha, kwenye taasisi za kifedha.


Alisema kazi hiyo wameanza kwa kuifanya kwa kuanzia kwenye vijiji vya mwambao wa ziwa Nyasa, na wamebaini  wengi wao wamekosa elimu ya ujasiriamali ambapo hujikuta wakijiingiza  kwenye vitendo viovu vya uasherati  kwa lengo la kujipatia fedha, huku wakikabiliwa na uwezekano mkubwa wa kupata magonjwa.

Mwenyekiti huyo pamoja na kuisifu wilaya hiyo ndio inaongoza kwa wasomi wengi wakiwemo wanawake katika mkoa huo wa Ruvuma huku wengi wao wakiwa na madaraka ya juu ya uongozi  hapa nchini, lakini wameshindwa kuwasidia na badala yake wamehamisha makazi yao na kwenda kuishi nje ya mkoa huo huku akiwataka wazawa wa Nyasa waishio nje wakumbuke pia kuja kuwekeza wilayani kwao.

Alisema wilaya hiyo ina fursa nyingi hasa kwa upande wa kilimo ardhi yake inarutuba nzuri yenye mabonde  ambayo inastawisha vizuri minazi, korosho, matunda na mbogamboga za majani, lakini wamekosa wataalamu na watu wa kuwasemea na kuwaacha wanawake wakihangaika wakati fursa za maendeleo zipo ambazo zinaweza kuwainua kiuchumi na kuishi maisha mazuri.

Pia aliwataka watendaji wa serikali wakiwemo maofisa maendeleo ya jamii wa wilaya hiyo, kufanyakazi kwa weledi kwa kuzingatia misingi na taratibu husika badala ya kukaa ofisini na  kusubiri taarifa  kitu ambacho kimekuwa kikidumaza maendeleo ya wanawake hasa wanaoishi vijijini ambao hawafikiwi na viongozi mara kwa mara.


No comments: