Friday, October 18, 2013

UHARIBIFU WA VYANZO VYA MAJI KATIKA MJI WA MBINGA, TISHIO LA KUKAUKA VYANZO VYA MAJI SERIKALI YATAKIWA KUCHUKUA HATUA MAPEMA

Mwenyekiti wa kitongoji cha Mbuyula Issack Nduguru akichangia hoja katika kikao cha baraza la Mamlaka ya mji mdogo wa Mbinga mkoani Ruvuma, ambapo alikemea uharibifu wa vyanzo vya maji unaofanywa katika mji huo na kuitaka serikali kuchukua hatua za haraka kunusuru hali hiyo isiweze kuendelea.

Mkurugenzi wa Mamlaka ya mji mdogo wa Mbinga Oscar Yapesa akisikiliza kwa makini hoja mbalimbali zilizokuwa zikitolewa na wajumbe katika kikao hicho, katikati ni Mwenyekiti wa Mamlaka hiyo Steven Matteso na upande wa kulia ni Diwani wa kata ya Mbinga mjini Kelvin Mapunda.

Baadhi ya Wenyeviti wa vitongoji vya Mamlaka ya mji mdogo wa Mbinga wakifuatilia kwa makini hoja mbalimbali katika kikao chao kilichoketi ukumbi wa jumba lka maendeleo mjini hapa. (Picha zote na Gwiji la matukio mkoani Ruvuma)

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa vitendo vya uharibifu wa vyanzo vya maji katika eneo la Mamlaka ya mji mdogo wa Mbinga mkoani Ruvuma, endapo havitadhibitiwa mapema huenda vikashindwa kuendelea kutoa maji, kutokana na wakazi wa mji huo kuendesha shughuli za kilimo katika vyanzo hivyo.

Aidha uharibifu huo unatokana na wakazi hao kukata miti iliyorafiki ya maji ambayo ipo kwenye vyanzo, jambo ambalo nalo linahatarisha kutoweka kwa uoto wa asili.

Hayo yamejitokeza katika kikao cha Baraza la Mamlaka la mji huo, kilichoketi kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo mjini hapa, ambapo wajumbe wa baraza hilo walilalamikia hali hiyo na kuutaka uongozi wa wilaya kuchukua hatua mapema kabla ya tatizo kuwa kubwa.

“Hili suala inabidi tuliangalie kwa kina zaidi hapa wataalamu wanaosimamia mazingira tunao hatuelewi wanafanya nini, tufute mambo ya siasa turudishe uoto wa asili katika vyanzo vyetu ili tuweze kuepukana na tatizo linaloweza kutokea hapo baadaye”, alisema Issack Ndunguru Mwenyekiti wa kitongoji cha Mbuyula.

Naye Mwenyekiti wa Mamlaka hiyo Steven Matteso alisema itakuwa si busara kuongea kwa mzaha kuhusiana na suala hilo la vyanzo vya maji, ni vyema ushirikiano ufanyike katika hili kwa kuhakikisha vyanzo hivyo ambavyo huzunguka mji huo vinakuwa salama.

“Nina hakika baada ya miaka kumi baadaye mji wetu utaingia kwenye tatizo kubwa la upatikanaji wa maji, kutokana na vyanzo hivi kuendelea kuharibiwa”, alisema.

Naye Kandidus Komba Mwenyekiti wa kitongoji cha Tugutu, alisema ni vyema elimu itolewe kwanza kwa wananchi juu ya umuhimu wa kutunza vyanzo vya maji na suala hili lisiishie kuzungumzwa katika vikao.

Pamoja na mambo mengine Diwani wa Kata ya Mbinga mjini, Kelvin Mapunda alisema ni wakati sasa kwa serikali ya wilaya ya Mbinga kupanga utaratibu wa kuzalisha miti rafiki ya maji, na kuwagawia wananchi bure kwa ajili ya kupanda katika maeneo ambayo vyanzo vya maji vimeathiriwa.

No comments: