Thursday, October 10, 2013

SHEREHE ZA UZINDUZI MRADI WA KIKOSI KAZI WAFANA, MKUU WA WILAYA ASEMA POLISI ACHENI KUPIGA RAIA NA ENDAPO MTAFANYA HIVYO MTAONEKANA MNAJITAWALA WENYEWE

Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga, naye alisisitiza kwa kuwataka Polisi kuacha kupiga raia na endapo watafanya hivyo, wataonekana kama ni watu ambao wanajitawala wao wenyewe.

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, Deusdedit Nsimeki akisisitiza jambo siku ya uzinduzi wa mradi wa kikosi kazi (task force), kwa kuwataka wananchi kujenga ushirikiano na jeshi la polisi ili liweze kufanya kazi zake kwa ufanisi mkubwa.

Baadhi ya wananchi nao walihudhuria siku hiyo ya uzinduzi.

         Vikundi vya ngoma navyo havikuwa mbali katika kutumbuiza. (Picha zote na Gwiji la matukio mkoani Ruvuma)

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WITO umetolewa kwa Askari Polisi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kuacha kupiga raia na endapo watafanya hivyo, wataonekana kama ni watu ambao wanajitawala wao wenyewe.

Sambamba na hilo wametakiwa kujenga ushirikiano na wananchi ili kuweza kuleta ufanisi katika utendaji wa kazi zao kila siku, kwa lengo la kuimarisha usalama kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga, alisema hayo alipokuwa mgeni rasmi akizungumza kwenye uzinduzi wa mradi wa kikosi kazi (task force) tarafa ya Mbinga mjini.

Ngaga alisema mradi huo wa kikosi kazi ndani ya tarafa hiyo ambao umeanzishwa hapa wilayani, hauna budi uwe endelevu kwa lengo la kuimarisha kazi zinazofanywa na askari kata, mkuu wa tarafa na vikundi vingine vinavyofanya kazi za kila siku katika kushughulikia miradi mingine ya polisi jamii, ndani ya tarafa nyingine zilizopo mkoani humo.

“Polisi wakirahisishiwa kazi katika ngazi ya tarafa, ulinzi utakuwa ukiimarika kwa kiasi kikubwa, ikiwemo suala hili la utii bila shuruti nalo nina imani kubwa wananchi nao watakuwa na uelewa mkubwa zaidi”, alisema Ngaga.

Aidha alisisitiza Viongozi na wananchi kwa ujumla kuendeleza ushirikiano na hawatakiwi kurudi nyuma kwenye jambo hili, kwa kile alichoeleza kuwa kuanza kwa uzinduzi huo, ni mwanzo mzuri ambao unahitaji uwe endelevu na sio vinginevyo.

Naye Kamanda wa polisi wa mkoa wa Ruvuma Deusdedit Nsimeki kabla ya kufanya uzinduzi huo alisema, Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa Jeshi la polisi, lakini mpango wa kuendelea kuwashughulikia wahalifu hususani pembezoni(mipakani) na maeneo mengine ndani ya nchi, utabaki palepale.

“Ndugu zangu sisi kwa upande wa jeshi la polisi tumejipanga katika hili, wahalifu wengi ni vijana wetu huko katika kata zetu, kinachotakiwa hapa tuwaelimishe hawa vijana waachane na mambo haya”, alisisitiza Nsimeki.  

Awali akisoma taarifa kwa niaba ya Mkuu wa polisi wa wilaya ya Mbinga, Mkaguzi mkuu wa tarafa hiyo Inspekta Nassibu Kassim Sued alisema kuwa mradi huo wa kikosi kazi unajumuisha maafisa na askari husika ambao watakuwa na majukumu ya kiutendaji wa kipolisi katika tarafa, kiungo kati ya polisi na wananchi.

Kadhalika alieleza kuwa kuweka kumbukumbu za wahalifu sugu na wazoefu wa ndani ya tarafa, kukusanya taarifa za kiintelijensia kutoka kwa watoto na walimu mshuleni na hata, kutafuta mbinu za kuwashirikisha vijana katika miradi ya polisi jamii.

Nassibu alisema, ni ukweli usiopingika kwamba Polisi hawawezi kufikia malengo husika ya ulinzi shirikishi katika jamii, endapo hawatatimiza dhana ya kushirikisha wananchi hasa tukiamini kwamba jukumu la ulinzi katika nchi hii, ni la kila mwananchi kama ilivyoainishwa katika Ibara ya 28 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.

 Hata hivyo Mkuu huyo wa tarafa alieleza changamoto wanazokabiliana nazo katika utekelezaji wa mradi huu, ni pamoja na kukosa miundombinu kwa maana ya usafiri na vifaa vingine husika, ambavyo vingeweza kuwarahisishia polisi katika utendaji wao wa kazi za kila siku.

No comments: